Familia
takatifu chimbuko la utakatifu (2)
w Ndoa ni kazi ngumu, lakini muhimu
w Kwanini
wengine hawaoi au kuolewa ?
KATIKA Toleo lililopita, tuliliona
Shirika la Kutetea Uhai (PRO-LIFE), Tawi la Tanzania likisema kuwa, Familia
kama hifadhi takatifu ya uhai, haina budi kutambua kuwa, zawadi kubwa na yenye
thamani katika ndoa ni WATOTO. Ndiyo maana ulimwengu umepewa zawadi ya ukombozi
yaani, KUZALIWA KWA YESU KRISTO. Endelea :
Kristo, alipenda kuzaliwa na kukua katika Familia Takatifu ya
Yosefu na Maria. Hivyo, Kanisa si kitu kingine, bali ni FAMILIA YA MUNGU. Na
familia ni KANISA LA NYUMBANI.
Umuhimu
wa familia ni mkubwa kiasi kwamba, nafasi yake katika kujenga utamaduni wa
uhai, haiwezi kuchukuliwa na kitu kingine. Hivyo, jukumu la malezi si la mtu
mmoja ni la wote, ni la jamii nzima.
Kama
Kanisa la nyumbani, familia imeitwa kutangaza Injili ya Uhai. Kwa mantiki hiyo,
familia isali ili kumtukuza na kumshukuru Mungu kwa zawadi ya uhai. Haki za
familia zizingatiwe.
NDOA NA FAMILIA
“Mungu akaumba mtu kwa mfano wake, kwa mfano wa Mungu
alimuumba, mwanaume na mwanamke aliwaumba, Mungu akawabarikia, Mungu akawaambia
zaeni mkaongezeke…” (Mwa 1: 26-27)
“Sasa huyu ni mfupa katika mifupa yangu,
na nyama katika nyama yangu. Kwa hiyo mwanamume atamwacha baba yake na mama
yake naye ataambatana na mkewe, nao watakuwa mwili mmoja” (Mwa 2: 23-24)
Msingi wa familia unatokana na katika Maandiko
Matakatifu yanayoibua dhana zifuatazo, mwanaume na mwanamke wanaounganika na
kuunda familia, wameumbwa kwa mfano wa Mungu
Binadamu
ni kiumbe kilichobarikiwa na Mungu, uzao ambao ndio tunda la mwunganiko wa mume
na mke umebarikiwa
Watoto,
yaani uzao ni baraka itokayo kwa Mungu, ni baraka inayoendeleza tendo la
uumbaji ambalo binadamu anashiriki pamoja na Mungu
“Kutozaa
kwa makusudi, au kuzuia kuzaa bila sababu yoyote ni kuzuia tendo la uumbaji
ambalo binadamu amepewa na kubarikiwa na Mungu na kama lingefanyika katika
familia ya Maria na Yosefu, ulimwengu huu usingepata Mkombozi na badala yake,
ungeamia,” linasema Shirika hilo la kutetea uhai, tawi la Tanzania kupitia
Mwenyekiti wake, Bw. Emil Hagam.
Linasema,
Mke na mume huunda muunganiko usioweza kugawanyika; kila mmoja ni mali ya
mwezake, na kwa ajili ya mwenzake. Hawa, huunda familia ya pekee nje ya wazazi wao
wakishiriki agano lisiloweza kuvunjwa
Sasa,
katika dunia hii yenye mkanganyiko wa mawazo, dhana ya familia inaweza kuelezwa
kwa namna mbalimbali kutegemeana na mwelekeo wa taaluma na lengo la mfasiri.
Mwanamume
na mwanamke walioungana katika ndoa, pamoja na watoto wao ndio wanaounda
familia. Familia kama taasisi ipo hata kabla mamlaka za kijamii hazijaitambua
na ambazo zina wajibu wa kuitambua. Hii ndiyo tafsiri ambayo kwayo tafsiri
nyingine zozote zihusizo familia zitarejea.
Kwa
kuumba mwanamume na mwanamke, Mungu alikusudia kuunda familia ya binadamu na
kuitengenezea mazingira maridhawa ya makubaliano. Wanafamilia ni wale wanaokaa
na kushirikiana kijamii pamoja, lakini kila mmoja akiwa na hadhi yake.
Silika ya familia ya Kikristo
Agano la Kindoa
Wakati
wote familia imetambulika kama msingi na namna ya kueleza tabia ya kijamii ya
binadamu. Familia kwa hiyo ni muunganiko wa watu ambao namna yao ya kuishi na
kukaa pamoja ni kwa njia ya “Komunioni”- - muunganiko wa watu.
Ndoa
ni agano ambalo kwalo mwanaume na wanamke kila mmoja hujitoa kwa mwenzake na
kila mmoja anamkubali mwenzake kama mwenzi na mshirika wake wa maisha.
Muungano wa hiari wa mwanamume na mwanamke
Ni
binadamu tu mwenye uwezo wa kuamua kwa hiari juu ya kuunganika pamoja kwa
msingi wa uchaguzi wa hiari. Katika ndoa mwanamume na mwanamke wanaungana kiasi
cha kuwa mwili mmoja (Mwa. 2:24). Japo ni binadamu wawili walio tofauti wanao
uwezo wa kuishi pamoja katika ukweli na upendo.
Uzao wa binadamu
Muunganiko
unaotokana na ndoa huleta furaha na faraja ya uzao wa binadamu wapya. Kwa hiyo,
kwa tendo hilo wazazi hushiriki na Mungu Muumbaji katika kuumba na kuzalisha
kiumbe kipya. Mungu anashiriki katika ubaba wa mzazi wa kiume na umama wa mzazi
wa kike katika kuleta uhai mpya.
Sifa
za familia kwa kadiri ya barua ya Papa Yohane Paulo II: “Families of the World”
Familia
halisi ni taasisi ya msingi ya jamii, inayojengwa katika uhalisi wa binadamu,
na yenye kujikita katika muunganiko wa hiari wa mwanamme na mwanamke katika
agano la maisha ya ndoa kwa ajili ya Kushibisha hamu za moyo wa binadamu za
kutoa na kupokea upendo, Kuwapokea na kuwalea watoto katika maendeleo yao ya
mwili na akili
na Kushirikiana makazi ambayo huunda msingi
wa maisha ya kijamii, kielimu, kiuchumi na kiroho.
Mengine
ni Kujenga uhusiano na kupasisha kizazi kipya pamoja na Kutoa huduma kwa
wahitaji mbalimbali.
Familia kama Fumbo la Kanisa
Familia
ya Kikristo inajifunua wazi na kutambulika kama jumuiya na wanakanisa, na kwa
msingi huu familia ni kanisa la (mwanzo) nyumbani. Hii ni jumuiya ya imani,
matumaini na mapendo.
Familia
hii ni muunganiko wa watu, ishara na mfano wa muunganiko wa Baba na Mwana
katika Roho Mtakatifu. Katika uzazi wa watoto na kuwaelimisha tunarejeshwa
kutambua uumbaji wa Mungu Baba.
Kwa
hiyo, familia inaalikwa kuishi maisha ya sala na ya sadaka ya Kristo. Sala za
kila siku zinaimarisha upendo na hivyo kuwezesha kazi ya uinjilishaji na
umisionari kufanyika.
Familia
imepewa jukumu la kutoa huduma ya kujenga ufalme wa Mungu kama mshiriki katika
maisha na umisionari wa kanisa. Katika familia matendo ya kikanisa ya
uinjilishaji, ufundishaji na uelimishaji hufanyika.
Matendo
hayo hufanyika mithili ya mama kanisa anavyowezesha kizazi kuendelea kufundisha
na kujenga familia ya kikristu. Familia hutekeleza utume wake wa kikanisa ndani
na nje ya kanisa.
Katika
familia wanandoa wanaishi kisakramenti, na hivyo ndoa inayojenga msingi wa
familia inaonekana kama sakramenti ya kutakatifuza na kama tendo la ibada au
kuabudu.
Wajibu
wa familia
Familia
kama taasisi iliyo wazi na ya msingi ina wajibu mbalimbali miongoni kwa watu
wanaoiunda.
Mwandishi
wa Barua kwa Waefeso anatujulisha wajibu wa kila mmoja wa watu wanaounda
familia, mume, mke na watoto.
Mwandishi
anatukumbusha kuwa wajibu wa msingi ni ule wa uhusiano. “Kila mmoja amstahi
wenzake kwa sababu ya kumcha Kristo”. (Efe. 5: 21). Huu ndio wajibu wa msingi
kwani unatutambulisha na kutushirikisha maisha yetu na Kristo.
Baada
ya kueleza wajibu huo wa msingi, mwandishi wa barua hiyo anafafanua wajibu wa
mume, mke na watoto. Kimsingi wajibu zote zinaegemea tunu za upendo, utii na
heshima.
Familia
zinazojengeka katika misingi hiyo ndizo zinazodumu na kuwa imara. Wanafamilia
katika familia za namna hiyo hukubaliana, huchukuana, hujengana, kila mmoja kwa
manufaa ya mwenzake na kwa manufaa ya pamoja.
Wajibu
wa familia kwa jamii unaelezwa vizuri kwa kutambua uhusiano asilia uliopo kati
ya familia ambayo sehemu, na ndiyo inayouunda jamii kwa upande mmoja, na jamii
ambayo hundwa na mkusanyiko wa familia moja moja kwa upande mwingine. Kwa hiyo
bila familia hakuna jamii. Kwa upande mwingine familia inahitaji jamii kwa
ajili ya ustawi wake.
Haki za Binadamu ndani ya Utawala Bora Tanzania
TANZANIA
ni moja ya nchi zinazojali suala la Haki za Binadamu na Utawala Bora. Katika
kuhakikisha utekelezaji wake, tayari inayo Tume ya Haki za Binadamu na Utawala
Bora iliyoundwa kwa mujibu wa Katiba ya Nchi Ibara ya 129. Ungana na MWANDISHI WETU katika makala haya ujue mambo haya kwa undani zaidi.
Haki
za binadamu ni haki na uhuru muhimu anaokuwa nao binadamu kwa sababu yeye ni
binadamu.
Uhuru na Haki hizi mtu
hapaswi kuwa nazo kutokana na kuainishwa katika mikataba ya kimataifa, Katiba
au Sheria za nchi, bali ni haki na uhuru huo mtu anakuwa nao kwa sababu yeye ni
binadamu na hakuna mtu anayeweza kumny’ang’anya au kumwondolea.
Hata hivyo, jukumu la
kuulinda uhuru na haki hizo za binadamu, uko mikononi mwa dola ambayo ina
vyombo vyake kama Mahakama na Polisi.
Haki za binadamu zimekuwa
zikikua katika hatua zijulikanazo kama vizazi na katika hatua mbalimbali ikiwa
ni pamoja na haki za kiraia na kisiasa, haki za kiuchumi, kijamii na
kiutamaduni.
Katika utekelezaji wa haki za
binadamu kwa upande wa sheria, inaweza kuwa na manufaa kwa jamii pale tu,
inapoonesha muelekeo wa kutekelezeka.
Mkataba au sheria yoyote ile,
itakuwa haina maana kama haiwezi kutekelezeka. Hivyo basi, ili mkataba au
sheria iwe ya manufaa, lazima ieleze wazi taratibu za utekelezaji wake na
zizingatiwe na kuheshimiwa.
Hata hivyo katika Tanzania
yetu sasa, raia wengi wamekuwa hawazijui haki zao. Wengi wao wamekuwa
wakifikiri kuwa, hata palipo na haki yao ya msingi, basi huhisi kuwa labda
wanafanyiwa upendeleo wa aina fulani.
Hali inaonesha kuwa, bado
serikali ina kazi ya kupeleka elimu hiyo kwa raia wake, na pia kuunga mkono
juhudi za kuelimisha jamii kuhusu haki zao, kazi ambayo hivi sasa imekuwa
ikifanywa na asasi zisizo za Kiserikali (NGOs) na jumuiya za kidini, kwa
asilimia kubwa.
Mtazamo wa utofautishaji wa
uelewa wa haki za binadamu katika jamii unaonesha kuwa, utekelezaji wa haki
hizo pia, umekuwa tatizo hata pale ambapo jamii imekuwa ikielewa haki zake za
msingi.
Hali hiyo imekuwa ikichangiwa
na mfumo uliopo wa utawala katika sehemu husika kutokana na kukithiri kwa
rushwa na udhaifu wa watendaji.
Katika kulitafiti hilo, hali
ya kuwa na utawala bora na wenye kujali sheria, haki na kanuni za msingi katika
utawala bora na wenye demokrasia ya kweli, itamsaidia mwananchi wa kawaida
kuelewa vizuri haki zake za msingi na namna ya kuzipata kwa njia ya amani.
Kitabu cha KWANINI TUJALI
MANUFAA, USTAWI KWA WOTE kilichotolewa na Tume ya Haki na Amani ya Baraza
la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC) kinabainisha kuwa, Utawala bora una maana
pana kuliko inavyodhaniwa na wengi.
Kinasema kuwa, wananchi
wanayo nafasi ya kutambua kama utawala wao katika kipindi fulani ulikuwa ni
utawala bora ama la.
Hata hivyo katika hili,
Tanzania inaweza kujiuliza kama wananchi wake wana maoni gani juu ya hilo.
Lakini, ni wazi kuwa raia hao wanazijua kasoro nyingi zilizo bayana katika
utawala wa nchi yao. Hivyo, hawawezi kujidai kuwa wanao utawala bora.
Mara nyingi utawala bora
ambao unajulikana ulimwenguni kote, ni ule ambao unajali na kufuata sheria na
kanuni na unaojali na kuzingatia haki za binadamu daima.
Utawala huo unapaswa ufanye
juhudi za kukomesha vitendo vya rushwa na upendeleo wa aina yoyote ile.
Watawala pia wanapaswa kutawala kwa kuzingatia na kuheshimu sheria na kanuni.
Uwazi na uwajibikaji vinapaswa kuwapo, bila ya hivyo, ni rahisi kwa watawala
kuvunja sheria bila ya kuwa na wasiwasi wowote.
Hata hivyo, kitabu cha KWANINI
TUJALI MANUFAA, USTAWI KWA WOTE pia kinaeleza kuwa, “Utawala Bora ni ule
unaozingatia Demokrasia.” Kinasema, palipo na utawala bora, sifa zote za
demokrasia zinaonekana machoni pa umma.”
Kinaeleza kuwa, msingi muhimu
katika hilo ni DEMOKRASIA ambayo ni sawa na utawala wa watu.
Katika kuzingatia misingi
hiyo ya utawala bora, watawala wanapaswa kutoa uhuru na uhalali katika
kuendesha mambo hususani ya UCHAGUZI, kwa kupokea na kuheshimu maoni ya
watu.
Hali ya kuona na kuelewa
mambo, itasaidia kutumia njia za kupunguza ulimbikizaji wa madaraka kwa
wachache na pia, matumizi mabaya ya madaraka. Na kutatoa fursa kwa raia, kuwa
na wawakilishi wanaotetea maslahi ya wanaowawakilisaha hasa maskini na wanyonge.
Katiba ya Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania, inapanua maana ya Utawala Bora katika wajibu wa Kikatiba kwa
viongozi katika Ibara ya 9 inayosema, “Viongozi wanapaswa kuendeleza utajiri wa
Taifa, kuuhifadhi na kuutumia kwa manufaa ya wananchi wote.”
Falsafa ya vita dhidi ya uhai
KATIKA Ukurasa wa kwanza wa Gazeti hili
toleo lililopita, kulikuwa na habari toka Zanzibar ikimnukuu Askofu wa Jimbo
Katoliki la Zanzibar, Mhashamu Augustino Shao, akilaumu uovu na hatari zilizopo
sasa ikiwa ni pamoja na hatari ya kuhalalishwa kwa vituo vya kuangamiza uhai
kwa visingizio mbalimbali huku vyombo vya dola na jamii kwa jumla, vikitazama
na vingine kuhalalisha kwa kisingizio cha “uzazi wa majira”. Katika makala haya
MWANDISHI WETU, anatuangalisha kwa undani juu ya falsafa, kuanza na hata kuenea kwa utamaduni
wa KIFO dhidi ya UHAI na hatimaye, tutaangalia mahitimisho ya jumla kuhusu
makongamano juu ya idadi ya watu duniani. Fuatilia.
Nadharia na utekelezaji wa sera za udhibiti wa idadi ya watu
zina msingi wake katika falsafa na mtazamo wa utamaduni wa kifo. Kimsingi,
utamaduni wa kifo umeibuka kama upinzani
kati ya wema na ubaya. Wema na uhai ni mali ya Mungu; ubaya na kifo ni
mali ya Shetani/Ibilisi. Kwa asili yake, Ibilisi ni MWONGO NA MWUAJI (Yoh.
8:44)
Utamaduni
wa kifo ni matendo na maelekeo ya binadamu katika kuendeleza na kutetea hali
zinazosababisha binadamu apoteze UHAI wake, audhuru mwili wake, adhalilishe utu
wake na kuunfanya mwili wake kuwa bidhaa inayoweza kununuliwa kuuzwa na kuchezewa.
Kwa hiyo, chochote kinachopingana na uhai, kama vile mauaji,
utoaji mimba, kuua kwa huruma (yutanasia), chochote kinachodhoofisha afya ya
binadamu, kama vile mazingira duni ya kuishi, hali mbaya za kazi, ubakaji,
ulawiti, uporaji wa mali za watu walio hai au waliokufa vyote hivi, vinajenga
msingi wa utamaduni wa kifo.
Sifa
kuu katika utamaduni wa kifo ni kuwa, binadamu anakuwa amekufa kidhamiri na
hivyo kukosa uwezo wa kutambua, kupenda na kutetea uhai na utu wa binadamu.
Utamaduni wa kifo hufurahia matendo maovu na kuchukia matendo mema.
Katika
utamaduni wa kifo, UONGO hutukuzwa na UKWELI huogopwa na kupigwa vita. Uongo
katika utamaduni wa kifo huonekana katika kutoa takwimu za uongo na kuzitetea,
katika kuficha kwa makusudi madhara ya matokeo ya matendo fulani na matumizi ya
nguvu za kimabavu katika kutekeleza sera zake kwa kutumia nguvu za dola, miundo
yake, vyombo vya habari na taasisi mbalimbali.
Utamaduni
wa kifo huenea kwa kasi na kukubalika kwa sababu ya nguvu ya FEDHA. Mabilioni
ya fedha hutumika katika kutangaza na kuhamasishwa matumizi ya nyenzo za
umalaya na utasa, kama vile kondomu na vidhibiti mimba. Watetezi wa utamaduni
wa kifo, hujenga chuki ya wazi na bayana dhidi ya watu/taasisi/mashirika
yanayodiriki kufichua uovu unaofichika katika programu waziendeshazo.
IKUMBUKWE
KUWA, Utamaduni wa kifo umeibuka kama ukinzano wa wema na ubaya (Mwa 2:
16-17; 3:1-5); Uongo na hila ndizo sifa kuu za Ibilisi. Hivyo, ndivyo
anavyotunasa sisi wanadamu kwa mitego na lugha tamu. Matokeo yake ni kifo
(Mwa 3:8-19).
Sote
tutambue kuwa, tunaponaswa katika mitego ya Ibilisi, tunakoma (tunafuta) hali
ya kimungu ndani mwetu na tunauvaa ubaya.
Wivu,
chuki na hila hutokana na ubaya aliotupatia Ibilisi (Mwa. 4: 8-10).
Ubaya huu husababisha kifo. Chuki na tamaa ndivyo vilivyomkumba Herode hata
wakaua watoto wachanga, akidhani kuwa
katika kitendo hicho, atamwua Yesu (Mt.
2:1-18)
Hii
ndiyo chuki iliyopo sasa dhidi ya watoto wachanga wasiozaliwa. Baadhi ya watu
wanawaua watoto hao wakidhani kuwa, wakizaliwa watapunguza pato la maendeleo ya
jamii. Hao, wanatumia vidhibiti mimba
kuwazuia watoto kuzaliwa. Huu ni wivu usio na kifani, ni roho mbaya, ni ubaya
wa ajabu sana (Ufu 12:1-7; Hek 2:23-24; Yak 1:13-15)
Mwanzo wa itikadi na falsafa ya udhibiti wa
idadi ya watu
Itikadi
kuwa ukuaji wa idadi ya watu huzuia maendeleo sio mpya. Mapema katika Karne ya
Saba, Mshairi Myunani, Hesoid alilalamika vikali kuwa nchi yake,
Ugiriki ilielekea kujaa watu na kwamba hali ya maisha ilikuwa ngumu kuliko
ilivyokuwa miaka ya nyuma ambapo idadi ya watu ilikuwa ndogo.
Wakati
Hesoid analalamika, ni wakati huo huo wahamiaji wa Kiyunani walikuwa wanajenga
miji ya kibiashara kandokando ya Bahari ya Mediterranean. Karne mbili baadaye
ustaarabu wa Ugiriki ulifikia kilele chake, ambapo uzalishaji ulikuwa mkubwa, kazi za sanaa, uhandisi,
fasihi, falsafa, hisabati na sayansi vilistawi sana.
Karne
tano kabla ya kuzaliwa Yesu, Plato na Aristotle walipata wasiwasi
kuwa idadi ya watu nchini Ugiriki ilikuwa kubwa wakiangalia kukua kwa idadi ya
watu katika mji wa Athene.
Huko
China, Confucius na wanazuoni wenzake walihofu kuwa nchi yao
ingekuwa na idadi kubwa mno ya watu wakati walipoona miji yao inaongezeka idadi
ya watu.
Katika
Biblia tunasoma kuwa, watawala wa Wamisri waliona kuwa Waisraeli
walikuwa wakiongezeka kwa kasi kiasi
cha kutishia utawala wao. Watawala hao waliamua kuwa, busara itumike katika
kuwapunguza Waisraeli hao. Na ndipo Mfalme wa Misri alipoongea na wakunga na
kuwaamuru kuwaua watoto wa kiume wazaliwapo. (Kut 1:8-16).
Mwanakanisa
Tertullan akiandika katika karne ya pili baada ya Kristo,
alilalamika alipoona kuwa mjini Cathago, idadi ya watu ilikuwa inaongezeka kwa
kasi na kufikiri kuwa hilo ni tatizo kwa dunia. Aliomba majanga, njaa, vita na
matetemeko ya ardhi yaonekane kama ni matukio muhimu kama suluhisho la kupunguza idadi ya watu.
Katika
karne ya 4, Mtk. Hieronimo aliandika kuwa, dunia sasa tayari
imejaa na idadi ya watu ni kubwa mno kwa ardhi iliyopo. Alipendekeza kuwa
suluhisho la tatizo hili ni kwa vijana wengi kujiunga na utawa.
Kuimarika kwa itikadi za udhibiti wa idadi ya
watu kimataifa
Nadharia za Malthus (Malthusian Theses)
– 1766-1834: alidai kuwa ongezeko la watu linakwenda kasi zaidi
kuliko ongezeko la kiuchumi na mahitaji ya chakula. Nadharia hii bado inarudiwa
leo hii ingawa bila uthibitisho wa kisayansi. Aliamini kuwa, watu maskini
walikuwa mzigo kwa mali asili za dunia na hivyo hawapaswi kuishi.
Alipendekeza
watu maskini wanyimwe misaada na Kwamba,
ziachwe nguvu asilia zifanye kazi yake ya mchujo na hivyo, watu wenye uwezo
wataishi na wale wasio na uwezo
watakufa wenyewe.
Margaret Sanger (1883-1966) na Marie Stopes
-1880-195]
Margaret
Sanger alianzisha Shirika la “American National Birth Control League” mnamo
1914. Alipinga kuwapa watu maskini likizo ya uzazi. Alipendelea kufutilia mbali
watu weusi na wale wasio na akili ambao aliona walikuwa wanaongezeka kwa kasi.
Aliwaita watu hao “magugu”. Alipendekeza kuwatumia wachungaji weusi ili kuondoa
kizazi cha watu weusi.
Margaret Sanger na Marie Stopes
walipendelea upatikanaji wa upeo wa raha kwa mtu binafsi. Kwa kadiri
ya nadharia hii, mwenzi (partner) anakuwa muhimu tu kama analeta raha na faida.
Kwa hiyo, watetezi hawa wanahubiri mapenzi huria (free love); matumizi
ya vidhibiti mimba (contraception); watu kukanakana ndoa; wanapendelea
ubaguzi (racism) na uwepo wa kizazi bora (eugenics).
Mnamo
1920 Margaret Sanger alimnukuu Aristotle kwa kukubaliana naye kuwa walemavu
waachwe wafe. Alitaka iwe sheria kuwa,
kizazi kilicholaaniwa kisiachwe kuishi. Alisema kushindwa kwetu kuwatenga watu
tahira wanaoendelea kuzaana na kuongezeka, kunathibitisha kushindwa kwetu kuona
umuhimu wa jambo hilo.
Nadharia
za Margaret Sanger ziliungwa mkono na watetezi wa nadharia za kizazi bora
nchini Ujerumani. Adolf Hitler: kunako 1935 na kuendelea, alianza kutekeleza
nadharia za uzao wa kizazi bora kwa nguvu sana. Mnamo Septemba 1939 alitoa
waraka wa siri uliowataka watu wote wenye magonjwa yasiyotibika wauawe.
Kutokana na waraka huo katika idadi ya Wajerumani
milioni 80, watu milioni 1.4 kati yao
waliingia katika kundi hili. Mnamo Oktoba 1939 hadi Agosti 1941 kati ya watu
70,000 na 80,000 waliuawa katika programu iliyoitwa ‘T.4’.
Programu
za kizazi bora za Hitler zililenga kuondoa duniani watu wa kizazi hafifu –
walemavu, wagonjwa na matahira. Hitler aliendelea kuwaondoa watu hao kwa njia
mbalimbali, zikiwemo za kuwaua katika kambi maalumu [concentration camps] na
kuwafunga watu kizazi [sterilization]
Kutoka nadharia hadi utekelezaji
MARIE
STOPES
Mwaka 1921 Marie
Stopes alianzisha kliniki ya uzazi wa mpango (kudhibiti kizazi) huko Uingereza
katika eneo la watu maskini na baadaye shirika la kimataifa “Marie Stopes
International” lilianzishwa kwa jina lake. Kwa sasa shirika hili linafanya kazi
katika nchi 38 duniani, nyingi zikiwa nchi maskini, ikiwemo Tanzania. Shughuli
za Shirika hili ni kutoa mimba, kufunga kizazi, kugawa/kuuza kondomu na uzazi
wa mpango kwa kisingizio cha “afya ya mama na mtoto”.
Mjane wa Kiafrika anavyoteseka
l Ni kweli
wanahusika na vifo vya waume zao?
Wajane
wengi wa Kiafrika wamekuwa wakipata matatizo sana wanapoondokewa na waume zao.
Hii kwa kiasi kikubwa, inatokana na mila na desturi za Kiafrika zinazowafanya wanyanyaswe
na ndugu wa mume. Ungana na makala haya ya THECKLA SHIJA, uone
baadhi ya adha za mjane wa Kiafrika.
Nomvula Bhengu alikuwa mwanake mwenye mafanikio katika maisha
hadi wakati mume wake anafariki. Alijiona wazi hahangaiki tena na majonzi
aliyokuwa nayo, bali sasa anasumbuliwa na mila na desturi zilizowafanya
wazidishe kibano kwake ili azifuate akiwa mwanamke wa Kiafrika baada ya kufiwa
mume.
Anasema
“Mume wangu alikutwa amefariki ghafla kwenye gari lake bila sababu yoyote
inayoeleweka. Ilitokea kama mwaka mmoja uliopita. lakini ninaendelea bado
kufanya uchunguzi kwani uchunguzi wa polisi umeishia tu kuwaweka baadhi ya watu
ndani na hukumu bado haijatolewa.”
Anaendelea,
“Nakumbuka vizuri usiku Gerald alipofariki. Ilikuwa kama saa tisa za usiku
nilipoamka toka usingizini na kukuta watu wamejaa mlangoni kwangu. Kwa kawaida,
Gerald alikuwa anarudi nyumbani usiku sana na wakati ule hakuwepo ndani,
niliogopa sana.”
“Nilijua
lazima kutakuwa na tatizo. Nikachanganyikiwa na kukimbilia chumbani kwangu huku
nikilia. Mara, shangazi akafichua siri kwamba, Gerald amefariki.
Watoto
wangu Thambo aliyekuwa na umri wa miaka 12 wakati huo na Phumzike miaka 7,
walizipokea habari za kifo cha baba yao kwa msikitiko makubwa. Nilijaribu
kujikaza kwa heshima yao lakini, mambo yalizidi kwenda vibaya tokea hapo.”
Nilikazana
kuwa karibu na mama mkwe wangu aliyekuwa anaishi kati ya mji wa Johannesburg na
Bizana.” Mwanamke huyo wa Afrika Kusini, alikaririwa na jarida la FEMINA.
Akaendelea,
“Kwa kweli familia ya Gerald ilinitenga hata kabla mwanao hajazikwa kwani hata
shangazi niliyemtuma akatoe taarifa za msiba badala yangu, alijibu kwa shida
sana.
Nilikuwa
mshukiwa wa kwanza katika familia ya marehemu ya kwamba ni mimi, niliyemuua
Gerald kitu ambacho ni jambo la kawaida mjane kuhusishwa na kifo cha marehemu.
Ulikuwa ni ushukiwa wenye maumivu makali sana.
Nilibaki
kuwa mjane nisiye na haki wala upendeleo wakati awali, nilikuwa na maisha
mazuri ya ndoa na nilikuwa mama mwema. Sikuwa na la kusema hata ilipofikia
wakati wa kutoa mawazo kuhusu mazishi.”
Akizidi
kusimulia kwa uchungu mintarafu matatizo yanayowakumba wajane wa Kiafrika, Bibi
Bhengu anasema kuwa, uwezo aliokuwa nao ulikuwa wa kulipia shughuli zote za
mazishi kwani familia ya Gerald ilisema, haiwezi kugharamia mazishi.
“Lakini
bado mawazo yote ni wapi atazikwa walikuwa wanapanga viongozi wa familia yao.
Zilikuwa ni mila za kizamani lakini, kwa upande wangu ilikuwa kama ukatili
kuiga mila hizo,” anasema.
Anazidi
kuelezea akisema, “Ilinibidi niandae mazishi jambo ambalo nilikuwa sijwahi
kufanya maishani na katika kila hatua niliyokuwa nikiifanya, nilikuwa naongozwa
na familia ya Gerald. Alisha kuwa amepanga ni wapi azikwe lakini, yote hayo
yalikuwa yamezimwa na famlia yao na wakapanga wao wenyewe.
Ilinibidi
nichukue mwili wa marehemu kutoka Cape Town kwenda nyumbani kwao na kwa kipindi
chote hicho, sikuwa na mawasiliano ya karibu na mama mkwe wangu.
Hakunipigia
simu na ilibidi nimtumie shangazi yangu kama mjumbe. Yote haya, yalikuwa
muendelezo wa uhusiano wangu na yeye usioridhisha kwa muda mrefu. Nilipofika
hakunikaribisha vizuri. hii ilinionesha wazi kuwa, hakufurahia chochote
nilichokuwa ninafanya.”
“Kwenye
mazishi sala zote zilikuwa zikielekezwa kwa Gerald na mama yake na wala si
kwangu na watoto wangu. Niliumia sana na hata mjomba wake hakuwa akisikitika
pamoja nami.
Baadaye,
niliona banchi la maua yasiyo ya kawaida na niliposoma ujumbe ulikuwa
umeandikwa hivi, “Kutoka kwa binti yako.” Nilichanganyikiwa lakini
baadaye, nikadhani ni kutoka kwa kaka yake Gerald.
Mara
nikagundua mwanamke mmoja akiwa na mtoto mdogo na nilivyomtazama huyo mtoto,
alikuwa na sura iliyofanana na mume wangu. Nilipatwa na mfadhaiko wa ghafla,
kumuona mke mdogo wa mume wangu na mtoto wake katika mazishi wakipewa heshima
namna ile kuliko mimi.
Nilipigwa
na butwaa wala sio hasira kwani nakumbuka mume wangu muda wote alikuwa analala
nyumbani. Lakini, kilichonishangaza zaidi, mama mkwe alikuwa anamfahamu
mwanamke huyo na kumkubali.
Baadaye,
binamu wa mume wangu akanieleza kuwa, Gerald alishamkutanisha huyo mwanamke na
familia yake.”
Aliendelea
kulalamika akisema hivi sasa, alikuwa analaumiwa yeye kuhusiana na kifo cha
mumewe wakidai kuwa, aliyemuua Gerald ni mpenzi wa mwanamke huyo.
Mwanamke
huyu ni kiwakilishi cha wanawake wanaoteseka barani Afrika Tanzania ikiwamo
kutokana na mila na tamaduni mbovu dhidi ya wajane.
Nchini
Tanzania na hata kwingineko Afrika, utamaduni wa wazazi na ndugu wa mume
kumchagulia kijana mke wa kuoa, ni mionhoni mwa vyanzo vya matatizo
yanayowakabili wanawake wanaofiwa waume zao.
Hapo,
ndipo kinyongo chote cha ndugu huishia kwa kumnyanyasa ikiwa ni pamoja na
kumsingizia kuwa, umalaya wake ndio umesababisha kifo cha mumewe.
Wengi
yakiwamo baadhi ya makabila ya Tanzania, wanaamini kuwa, kifo cha mwanaume
daima lazima kina mkono wa mwanamke ama kwa ushirikina, au njama yoyote. Wazo
hili ni hatari kiroho na kimwili hasa katika kipindi hiki ambacho watu wanamjua
zaidi Mungu katika ulimwengu wa sayansi na teknolojia.
Si
jambo geni kusikia ndugu wa mwanaume (marehemu) akiwamo mama au baba, wakiongoza
jahazi la kudai mali zote za familia ya marehemu bila kujali mkewe na watoto
wataishi vipi endapo watanyang’anywa haki zao.
Mfano
mzuri ni pale mjane huyo anaposema kuwa, kuyokana na matatizo baina yake na mama
mkwe yaliyoanza tangu kipindi Gerald anamchumbia, kutokana na mama huyokutaka
kijana wake aoe mwanamke mwingine, ilifikia hatua hata akakataa kufika nyumbani
kwao.
Anasema
kitendo cha Gerald kumuoa yeye na kuhama, kulilimuuma sana maana aliona kama ameondolewa
chanzo chake cha pesa.
Anasimulia
kuwa, Mama yake Gerald alizidi kuchukizwa baada ya kugundua anapata pesa nyingi
kuliko mwanae kwani nalikuwa mwanamke naliyesoma na mwenye elimu ya juu na hata
wakati wa mahafari yake, alimwalika lakini, akakataa . ”… Gerald alijaribu
kusuluhisha ugomvi huu wakati wa uhai wake lakini hakufanikiwa,” anasema.
Mjane
wa Kiafrika pia katika jamii nyingi, anatakiwa aishi maisha fulani maalumu kwa
kipindi kinachopangwa na familia ya marehemu. Mjane anatakiwa avae nguo nyeusi
na kitambaa kwa muda wa kati ya miezi mitatu .
Mjane
hulazimikakuzivaa kila wakati na hata unapopanda gari hutakiwi kukaa mbele
kwani inaaminika kuwa, ni nuksi.
Anasema,
“Familia ya Gerald iliniamulia kukaa eda kwa miezi tisa kitu kilichokuwa si
kawaida. Ilibidi nimwombe shangazi yangu akawaeleze kuwa mimi sitakaa kwa miezi
hiyo. Nilimtumia shangazi kwani ndiye aliyekuwa akijadiliana nao badala yangu.
Wakati
nikiwa eda, sikuendelea vema na maisha yangu na hata ilipofika siku ya kumaliza
msiba, hawakuniruhusu kumwalika rafiki yangu yeyote katika sherehe, kitu
ambacho kilikuwa muhimu katika maisha ya familia yangu, lakini mila na desturi
ndizo zilizokuwa zikipewa kipaumbele zaidi.
Sikuwa
najali kuomboleza msiba wa mume wangu, nilikuwa bado namuomboleza lakini
kilichokuwa kinanisikitisha, ni jinsi hii jamii inavyonitenga na kunibagua kama
mtu wa taifa jingine.”
Wakati
wajane wa kike wanateswa na masaibu mengi ikiwa ni pamoja na kufukuzwa
nyumbani, kunyimwa huduma zote muhimu na pengine kupigwa na ndugu wa marehemu,
hali ni tofauti kwa mjane wa kiume (mwanaume anayefiwa mkewe). Yeye huishi
anavyotaka baada ya mazishi na hata katika kipindi cha msiba.
Mwanaume
hana mavazi maalumu katika kipindi cha maombolezo. Hali hii, inaonesha kuwa,
bado waafrika wengi wakiwamo baadhi ya wanajamii wa Kitanzania, wamepitwa na
wakati kwani wanaendekeza na kuendeleza ubaguzi. Hawalazimishwi kuvaa mavazi
meusi; hawakatwi nywele! Kwanini ubaguzi uwepo?
Kwa
kweli mila hizi zinahitaji marekebisho ya hali ya juu kulingana na maisha ya
sasa kwani zinawakandamiza wanawake.
Kwa
mjane wa kiume, anaruhusiwa kuoa wakati wowote lakini kwa mjane wa kike,
ajaribu kuishi na mume baada ya kifo cha mumewe aone mateso atakayovuna toka
kwa ndugu wa mume; usawa na haki katika ndoa viko wapi?
haieleweki
ni kwanini mjane mwanamke anakuwa kichwa cha kupata uangalizi huu wa ajabu, na
kwa nini maisha yao yanafanywa kuwa magumu baada ya kufiwa waume.
Wajane
wa Kiafrika wanatakiwa kuamka na kutetea haki zao. Lazima waeleze kila mmoja
kwamba, matarajio wanayoyapata kama wajane ni kutokutendewa haki na ni uonevu
mkubwa.
Mama
huyo Msouth anakaririwa akisema, “Nakumbuka siku ya harusi yetu. Mzee
mmoja aliniasa kwamba, mume anaposema anakwenda kazini au mkutano, hutakiwi kumuuliza ni wapi; anakwenda na nani
au atarudi kwa sababu hata yeye mwenyewe hafahamu.” “Labda kauli hii
ilinipumbaza.”
Umefika
sasa wakati jamii nzima ikaungana
kuzipinga mila zozote zinatowabagua, kuwatenga na kuwanyanyasa wanajamii
wakiwamo wanawake. Watu wote wajue kuwa, kila mtu ameumbwa kwa mfano na mapenzi
ya Mungu na kwamba watu wote, wana haki sawa mbele za Mungu.
Hata hivyo,
juhudi hizo za usawa, zisiwe zinazoelekea kukiuka mpango wa Mungu katika
uumbaji.
Kwanini mitume wengine hawakuandika Injili?
Katika toleo hili,
Mtaalamu wetu wa Biblia, Padri Titus Amigu, anajibu swali la msomaji wetu
anayetaka kujua zaidi mintarafu Injili. Yeye aliuliza akisema, “Nafahamu kwamba
mitume wa Yesu walikuwa 12 lakini, walioandika Injili walikuwa wanne tu.
Kwanini hawakuandika wote? Au hao hawakuwa mitume, bali wandishi wa habari wa
Yesu Kristo?”
JIBU: Ndugu Msomaji, kuandika kitu licha
ya kuwa ni kipaji cha mtu, pia ni hiari ya mtu mwenyewe anayejua kusoma na
kuandika. Kwa mfano, wewe mwenyewe; je, umewahi kuandika kitabu juu ya matukio
katika ukoo wenu? Kama umefanya hivyo, hiyo ni bahati yako lakini kama
hujafanya hivyo, jiulize ni kwanini?
Basi
waliaoamua kuandika habari za Yesu Kristo na kutuambia alivyoishi na kufanya mambo
yake hapa duniani, walikuwa wengi sana. Soma na uhakikishe hilo katika Injli ya
Luka (Lk 11-4). Walikuwamo mitume na wasio mitume yaani, wafuasi
kadhalika. Hao, ni wengi sana walioamua kuandika.
Ndugu
msomaji, wakati ule hakukuwa na mambo ya uandishi wa habari. Hayo ni maendeleo
ya siku hizi tu. Ila kuandika, wale wenye hiari na vipaji walifanya hivyo kwa
habari zile zilizowavutia. Basi kukawa na maandishi mengi sana.
Kwa
bahati mbaya kwa wakati ule, waandishi hawakujitaja waziwazi labda kwa vile
walitaka kuishi kinyenyekevu bila kujigamba kama waandishi. Kuhusu majina ya
waandishi, basi yakawa yanatajwa mengi tu na ilipofika karne ya pili hadi ya
nne na kuendelea, maandishi yote yalikusanywa na kuchaguliwa yale yaliyokuwa
safi sana na yenye kuhimiza upendo na imani; yale yaliyokubalika na kupokelewa
na Wakristo wengi; yale yasiyopingana na mafundisho ya msingi; yale yasiyotilia
chumvi mambo wala mbwembwe.
Hayo
yakachaguliwa na Uongozi wa Kanisa na kwa msaada wa Roho Mtakatifu, yakawekwa
pamoja na ndipo tukapata Biblia.
Hapo,
yakapatikana maandishi safi yasiyo na mbwembwe wala jeuri ndani yake yaliyofika
27. Maandishi hayo ndiyo yaliyotimiza sifa zote zile nzuri.
Ndiyo
hayo maandishi yaliyo katika Agano Jipya; Injili nne za Mathayo, Marko, Luka na
Yohana. Mengine ni Kitabu kimoja cha Historia yaani MATENDO YA MITUME; Barua 14
yaani Barua kwa Warumi; Barua ya Kwanza na ya Pili kwa Wakorintho, Barua kwa
wagalatia, Barua kwa Waefeso, Barua kwa Wafilipi, Barua ya Kwanza na ya Pili
kwa Wathesolanike, Barua ya Kwanza na ya Pili kwa Timotheo, Barua kwa Tito,
Barua kwa Filemoni na Barua kwa Waebrania na mwisho, kitabu kimoja cha kinabii;
ndio UFUNUO WA YOHANA.
Basi,
kimajina, mitume wengi walikuwa wamehusishwa na maandishi lakini, kama ni
wenyewe waliandika, au la, au labda wanafunzi wao waliandika na wakatumia
majina hayo, hakuna anayejua kwa uhakika.
Maandishi
yote yasiyokuwa mazuri hata yale yaliyokuwa na majina ya mitume, yakaachwa
katika mchujo huo.
Ndipo tukabakiwa na maandishi yaliyopo katika vitabu hivyo 27 ambavyo vipo katika
Agano Jipya. Kati ya maandishi hayo au vitabu hivyo, vichache vinaunganishwa
hasa na mitume ambao tunaweza kutafuta habari zao kwa uhakika yaani Injili ya
Yohane na Injili ya Mathayo.
Marko na
Luka walikuwa wafuasi tu; sio mitume na tena wafuasi wa Mitume Petro na Paulo
na wala hawakuwa wafuasi wa Yesu moja kwa moja. Barua nyingi zinaunganishwa na
Paulo ambaye alikuwa Mtume, lakini sio kati ya wale mitume 12.
Kwa hiyo
basi, unaona jinsi majina yanavyolegalega kidogo, lakini ujumbe wao ni mzuri
katika vitabu hivi.
Kwa
vyovyote, ni watu waliohusiana na Yesu Kristo kiimani, walioandika vitabu vya
Biblia yetu yaani ,Agano Jipya na siyo waandishi wa habari maana, kwa enzi zile
za kale, hawakuwapo waandishi wa habari.
Vitabu
vingine viliandikwa na vilihusika pia na habari za Yesu Kristo kama vitabu vya
Agano Jipya tulivyo navyo. Vitabu hivyo lakini, kwa kutokidhi haja na uadilifu
uliotakiwa na wale waliochagua vitabu kwa mwangaza wa Roho Mtakatifu,
viliachwa.
Vitabu
hivyo vina mbwembwe na maelezo mengi yasiyojenga lolote; vina habari nyingi
zilizotiliwa chumvi na kadhalika.
Mfano ni
kama vile vitabu vya Injili ya Filipo, Injili ya Petro, Injili ya Ukweli,
Injili ya Ukamilifu, Injili ya Mikoa Minne ya Mbinguni, Injili ya Mitume Kumi
na Mbili, Injili ya Wafusi Sabini, Injili ya Mathias, Injili ya Yuda, Injili ya
Bathlomeo, Injili ya Maria na Injili ya Koritus.
Mifano
mingine ni Injili ya Basilibesi, Injili ya Mwanzo wa Yakobo, Injili ya Nikodemo, Matendo ya Paulo, Matendo ya
Petro, Matendo ya Thomas, Barua kwa Leokardia, Barua Kati ya Seneka na Paulo,
Barua ya Kughushi kwa Tito, Ufunuo wa Paulo, Ufunuo wa Thomas na
kadhalika. Hivyo vyote, havikukidhi
sifa za Injili, basi vikaachwa.
Hivyo, ni
wazi wengi waliandika kiasi hata haijulikana ni nani alikuwa mwandishi mtume
kwelikweli.
Hata
hivyo, kama nilivyosema, hawa walioandika hata kama hawakuwa ni mitume moja kwa
moja, walikuwa wafuasi wa Kristo kwa maana
hii kwamba, walimsikiliza na kumpenda kwa namna moja ama nyingine.
Hawa hawakuwa waandishi wa habari maana enzi zile
waandishi wa habari hawakuwapo kwa vile magazeti, televisheni na redio,
hazikuwapo. Ni vyombo hivyo vinavyohitaji waandishi wa habari. Haya mambo ya
kuwa na waandishi wa habari ni yetu siku hizi. Hayakuwa yao katika enzi zao zile.
‘Tunataka Mwaka Mpya, Mtazamo Mpya’
Na Pd. Baptist Mapunda (M.Afr)
Tunaposherekea sikukuu ya kuanza mwaka, tena mwaka mpya wa 2005,
lazima tukumbuke kitu kimoja kwamba, hii ni siku ya kuombea Amani Duniani kadiri
ya utamaduni wa Kanisa Katoliki duniani.
Kwa mantiki hii, ni vema kurejea ujumbe wa Baba Mtakatifu Yohane Paulo wa Pili katika siku hii.
Ujumbe
wenyewe ni huu unasema kwamba, “Msishindwe
na uovu, bali ushindeni uovu kwa kutenda wema.” Maneno hayo ya Baba Mtakatifu ameyatoa
katika Barua ya Mtakatifu Paulo kwa Warumi (Rum 12:21). Baba mtakatifu anaendelea kusema kwamba,
“Huwezi kuushinda uovu kwa kutumia uovu.”
Watanzania
tunapoanza mwaka mpya na kuiombea dunia amani ikiwemo Tanzania, tukumbuke kuwa,
“Amani inapatikana tu, iwapo tutadumu katika kutenda wema.” Hii ni changamoto
kubwa kwa Watanzania hasa tunapoelekea kwenye Uchaguzi Mkuu wa Mwaka huu.
Nikiwa
katika likizo ya Krismasi nyumbani Mbinga, Ruvuma, nilisoma magazeti kadhaa
yalikuwa yamesheheni jumbe mbalimbali za Sikukuu ya Kuzaliwa Bwana Wetu Yesu
Kristo.
Ujumbe
mmoja ulionifurahisha, ni ule wa
Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo aliposema, “Watu wenye uchu wa madaraka na
uroho wa mali hawawezi hata siku moja, kudumisha amani, mshikamano wa kitaifa,
upendo na undugu kati ya Watanzania.” Nami daima nimeamini hivyo, kwani uongozi
bora unahitaji sadaka kubwa.
Kwa
muda mrefu nchi yetu imejulikana kama nchi yenye amani na mshikamano wa
kitaifa. Lakini, matukio ya hivi
karibuni haoneshi kuwa, tunaendeleza tunu hiyo, bali sasa nchi inaonekana wazi
kuelekea kubaya.
NIONAVYO MIMI, amani
ya kweli inaambatana na Ukweli maana ni kwa ukweli, tutawekwa huru. Ukisoma
magazeti na kusikiliza mazungmzo ya watu nchi nzima, unapata picha kwamba uhuru
unakosekana katika sehemu nyingi.
Uhuru
unakosekana kwa vyombo vya habari katika sehemu za nchi yetu, wandishi wa
habari wanawoga mkubwa kuripoti matukio maovu kwa hatari ya kufuatwa na vyombo
vya dola. Kuna kukosekana kwa uhuru wa watu kueleza yale wanayoyaona,
wanayoyaishi, na kadhalika.
Hali
hii haiashirii kudumu kwa amani inayoanzia mioyoni mwetu, na kama mioyo yetu
inakuwa na woga na malalamiko kila wakati, basi hii ni shida kubwa katika
jamii; kwani amani itakuwa ya maneno tu, huku wengine wakiwa kama mshumaa
unaongua ili kuangazie wengine.
Kamati ya Haki na Amani imetoa bango
lisemalo, “HOFU NI SUMU.” Hivyo, tunapoanza mwaka mpya, tuuanze kwa
kubadili mitazamo ili tujitafiti ni kwa nini watu wengi wasomi na wasiosoma,
wote tumegubikwa na hofu na hivyo, kutosema ukweli.
Kwa
mang’amuzi yangu, moja ya sababu ni kukosa kufahamu haki za msingi katika
jamii. Nikiwa Mbinga katika likizo hiyo, nilijifunza mengi toka kwa Wana
Mbinga, jinsi hofu ilivyotanda katika maisha ya watu. Hii inanipa picha kwamba,
maendeleo huko hakika ni ndoto ya mchana maana, bado watu hawataki kubadili
mtazamo.
Jitihada
kubwa zinatakiwa ili kuwakwamua watu kutoka katika wimbi la hofu. Mtu akieleza
ukweli juu ya jamii, siasa, uongozi na umasikini, anaonekana kuwa adui wa chama
fulani au Serikali. Ni kwa nini? Hapa, elimu ya uraia inahitajika sana katika
jamii ili kusaidia kuendeleza amani.
NIONAVYO MIMI, Tunapoanza
Mwaka Mpya, Watanzania tuwe na mtazamo mpya wa Kuupenda Ukweli na kupenda
kusikiliza maoni ya wengine hasa kwa viongozi wetu.
Sio
siri, siku hizi katika nchi yetu inaonekana kama vile kusema ukweli ni
kutenda dhambi. Rais Benjamin Mkapa aliyebakiwa na miezi kumi akiwa
ofisini, alipochukua madaraka ya nchi hii alitangaza sera, sera aya “Uwazi
na Ukweli.” Je, inakumbukwa? Inaheshimiwa na kutekelezwa?
Naamini
sera hii ni nzuri, lakini je, Watanzania tunaifuata? Mwaka huu 2005 uwe mwaka
wa uwazi na ukweli na hasa katika kupendekeza, kukampeni na kuchagua viongozi
mbali mbali wa taifa akiwemo Rais wa nchi atakayefuata nyayo za Rais Mkapa huko
Ikulu
Hata
hivyo inaanza kutia moyo kuona kuwa, kadri siku zinavyopita, watu wanazidi
kupata uelewa juu ya maisha yao, siasa, uongozi, maendeleo, halikadhalika, imani yao. Maendeleo ya kisayansi na
teknolojia, nayo yanawasaidia watu kuuelewa ulimwengu na kujifunza namna
wenzetu katika nchi nyingine, wanavyoendesha demokrasia ya vyama vingi bila
uoga, chuki wala uadui toka pande zote za watawala na wataliwa.
Mawasiliano
ya mtandao nayo yanapanua uelewa wa kiakili pamoja na kwamba
wakati mwingine, mtandao huo unaleta mambo yaliyo kinyume na utamaduni wetu.
Kiongozi wa Tanzania ya leo asijidanganye kuwa watu wamelala la hasha! Watu
wanaelewa mambo mengi sana, ila tu hawana nguvu na nafasi ya kusema ukweli huo
bila kutiwa matatani.
Kusema
ukweli kunadai sadaka, tunajua yaliyompata Yesu Kristo, alikufa kwa sababu ya
kusema na kutetea ukweli. Nchi yetu kama nilivyosema awali, inahitaji manabii.
Kadri tunavyouelekea Uchaguzi Mkuu, manabii hao wanazidi kuhitajika kwa nguvu
zaidi.
Watanzania
tuna misamiati mingi sana ya kutufundisha mathalani, “Tenda wema uende zako,
usingoje shukrani.” Hivyo, sote tutambue ukweli kuwa, “uongozi” ni
utumishi siyo “utawala.” Hii ni kuanzia makanisani, serikalini, katika
chama, taasisi na jamii kwa jumla.
Si
mara chanche tunawasikia watu wanalalamikia uongozi kuwa ni wa kiutawala zaidi
kuliko kiutumishi. Kwa mtindo huo, nidhahiri kuwa amani itatoweka tu; kwa vile
hakuna masikilizano wala heshima kwa wale wanaoongozwa maana wanaburuzwa kama
bakuri linaloelea baharini.
Sasa,
Watanzania tubaki kuwa watu wa kuburuzwa tu!? Hapana! Sasa tuanze Mwaka Mpya na
mtazamo unaotekezeleka kuwa, watu wenye uchu wa madaraka na uroho wa mali
hawatufai na hatuwataki.
Kwa
msingi huo, tusiwe vinyonga unababilika rangi ghafla baada ya kuona shilingi
2000, au T-Shirt yenye picha ya mgombea hata kama hafai kukuondoa
katika ugumu wa maisha unaokukwaza. Hivi tunapodanganywa kwa bei rahisi namna
hii, anayeumia ni nani?
Ni
wazi kuwa, uongozi ni dhamana anayopewa mtu au kikundi kwa manufaa ya jamii
nzima hivyo, watanzania tuuige mfano bora wa wajumbe wa Shirikisho la Soka
Tanzania (TFF) kwa kuamua kufanya mabadiliko ya dhati na kweli, wakatekeleza
nia yao.
Watanzania
tukubali kuwa, watoa rushwa hawatufai, wala rushwa, hawatufai na hata wanaotoa
amri za kijeshi bila kutaka maoni ya wengine, pia hatufai.
Kwa
mtazamo wangu, Mwaka Mpya uanze kwa kuipa PCB meno ya kumng’ata mwizi bila
kujali mwizi ana umbo la tembo, simba au chui eti huyo asionwe, lakini sungura
na dagaa kwa mwili mdogo na upole wao, wanaswe kwa mitego ya shilingi 10,000/=
Katika
Barua hiyo ya Mtakatifu Paulo katika ujumbe wa Baba Mtakarifu, tunamwona
akikazia kwamba, “Usilipe uovu kwa uovu” (Rum 12:17). Hivyo basi, tuushinde uovu kwa kutenda wema.
Yesu
Kristo anasema, “Achaneni na utamaduni wa “jino kwa jino.” Upendo ndiyo
njia ya Kristo hivyo, tuwapendeni hata adui zetu. Kwa kulijua hilo ni gumu
katika maisha yetu anasema, hiyo ni “Amri” wala siyo “ombi.”
NIONAVYO MIMI, Tunapoanza
Mwaka Mpya wa 2005 wa Uchaguzi Mkuu, viongozi wa siasa waache visasi kati yao, na maneno ya kuchochea
chuki kwa wananchi. Tukumbuke kuwa, amani iliyopo ni zawadi toka kwa Mungu; ni
mpango wake Mungu kama alivyotuasa Kardinali
Pengo katika mahubiri yake ya
Noeli.
Katika
mwaka huu tuliouanza, wapiga kura tuwachuje watakaogombea katika nafasi
mbalimbali za uongozi na tukitambua kuwa, huyu ni mtu wa kisasi, basi
tumtupilie mbali kwani atakuwa kichocheo na chanzo cha kutoweka kwa amani yetu
ambayo ni zawadi ya Mungu.
Mtazamo
wetu uwe wa kuchagua watu wanaoendeleza nchi yetu kwa masilahi ya wote, ya siyo ya kikundi fulani tu, au mtu
binafsi. Watu wenye uchu wa madaraka na mali, chuki na uchochezi ni wa kuepukwa
kama ukoma, ebola na magonjwa mengine hatari.
NIONAVYO MIMI, Kila
chama cha siasa kipendekeze watu wanaokubalika
na jamii na siyo vyama vyao. Tusipendekeze watu kutokana na hisia HUYU
NI MWENZETU, bali tutazame amani, umoja, mshikamno na maendeleo ya Taifa.
Kila
Mtanzania aombe kuongozwa na Roho Mtakatifu katika kutekeleza wajibu huu.
Tujiulize; HUYU MWENZETU NI NANI na KWA MANUFAA YA NANI?
Mwaka
huu uwe wa kutazama maslahi ya wote hasa maskini huko vijijini ambao wapo hoi
kabisa. Asiyeamini niyasemayo, aende kijijini aishi huko kwa wiki mbili tu,
kasha arudi aniambie alichobaini huko.
Mwaka
2004 ulikuwa wa matukio mengi sana, ambapo maovu yalizidi, mathalani; ubakaji,
uvutaji bangi, ubadhirifu wa mali ya
umma, wizi wa fedha katika mabenki, malumbano ya kisiasa, ugaidi, na kadhalika. Haya sasa, tuyaache yaende; sisi tuanze
upya, ya kale yamepita, tusonge mbele kwa matumaini na Imani, kwamba Yote
tutayashinda pamoja na Mwokozi Wetu Yesu Kristo.
NAWATAKIENI HERI YA MWAKA MPYA NA BARAKA TELE
Mtu binafsi, Vyama vinaruhusiwa
kumiliki Majeshi ya Ulinzi?
Na Dotto Shashi
HIVI karibuni kulitokea mjadala mkubwa wa umma uliosabishwa na
tamko la Kiongozi mmoja wa Chama cha Siasa nchini, ambaye alieleza nia ya chama
chake kutaka kuanzisha kikundi cha ulinzi kwa ajili ya kulinda mali za chama
hicho.
Kauli
ya kiongozi huyo iliifanya Serikali iingilie kati suala hilo na mpaka ikafikia hatua ya kutoa ufafanuzi wa kisheria
dhidi ya tamko la kiongozi huyo.
Japokuwa
kiongozi huyo alieleza moja kwa moja majukumu ya kikundi hicho cha ulinzi kuwa,
ni kulinda mali za chama hicho. Kwa mtazamo halisi na wa kimsingi, kikundi
hicho hakitofautiani kimaana na jeshi lililopo hivi sasa nchi la ulinzi kama
inavyoainishiwa katika katiba yetu.
Katika
mada ya toleo hili, tutaangalia katiba inaeleza nini juu ya Majeshi ya Ulinzi
nchini, yaani “The Armed Forces.” Ikiwa ni pamoja na mambo mengine
kuhusiana na majeshi hayo.
Sura
ya Tisa ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano ya Tanzania, 1977, kama ilivyofanyiwa
marekebisho mbalimbali, inaeleza kuhusu Majeshi ya Ulinzi.
Kifungu
cha 147 Ibara ndogo ya Kwanza (1) cha Katiba kinaeleza kuhusu
katazo kwa mtu au kikundi cha watu au serikali, kuanzisha au kuwa na Jeshi la
Ulinzi la aina yeyote ile nchini Tanzania, isipokuwa serikali pekee.
Katika
ibara ndogo ya Pili (2) yaani “Sub Article (2),” inaeleza kuwa,
Serikali ya Jamhuri ya Muungano inaweza kwa mujibu wa sheria, kuanzisha au
kumiliki majeshi ya aina yeyote Tanzania, kwa makusudi ya ulinzi na usalama wa
nchi (kwa maana ya mipaka) pamoja na watu wa Tanzania.
Kimsingi
hapa tunaona kuwa, ni serikali pekee yenye uwezo wa kuanzisha na kumiliki
jeshi, hivyo kwa mtu binafsi kama tulivyoona hapo mwanzo, sheria inamkataza,
vivyo hivyo kwa chama cha siasa.
Tukiendelea
kutazama zaidi sifa za majeshi ya ulinzi na usalama, tunaona kuwa, Ibara ndogo
ya tatu, katika kifungu hicho cha 147 cha Katiba, inaeleza kukatazwa kwa askari
yeyote wa jeshi la ulinzi na usalama kujiunga katika chama chochote cha siasa,
isipokuwa katiba inampa haki ya kupiga kura askari huyo, kama ilivyoainishwa
katika kifungu cha Tano (5) cha Katiba.
Labda
mpaka hapo mtu anaweza kuwa anajiuliza swali kuwa je, askari wa majeshi ya
ulinzi na usalama ambaye amekatazwa na katiba yetu kujiunga na chama cha siasa
ni yupi?
Swali
hili linajibiwa na ibara ndogo ya nne (4) ya kifungu cha 147 cha katiba. Kwa
mujibu wa ibara hiyo, askari wa majeshi ya ulinzi na usalama, maana yake ni
askari aliye katika ajira ya ama Jeshi la Ulinzi, yaani “Defence Forces,”
Jeshi la Polisi (Police Force), Magereza, yaani (Prisons Service)
au Jeshi la Kujenga Taifa, Yaani “The
National Service” aliyekatika ajira hiyo ama kwa masharti ya
muda au masharti ya kudumu yaani “Temporary or Permanent terms.”
Sasa
tuangalie mamlaka ya Amiri Jeshi Mkuu, yaani, “Powers of Commander in –
chief.”
Katika
kifungu cha 148 Ibara ndogo ya kwanza kinaelezea mamlaka ya Amiri Jeshi
Mkuu, ambaye ni Rais wa Jamhuri ya Muungano.
Ibara
hiyo ndogo inaeleza kama ifuatavyo:-
“Bila
kuathiri sheria nyingine yoyote iliyotungwa na Bunge, miongoni mwa mamlaka ya
Rais kama Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi, ni pamoja na kuamrisha majeshi
ya ulinzi. Kujiingiza au kufanya shughuli za Operesheni za kijeshi zihusianazo
na ulinzi wa Jamhuri ya Muungano, kufanya shughuli za uokoaji (Rescue)
kwa ajili ya kuokoa maisha na mali nyakati za hatari na au masuala mengine
yoyote endapo Amiri Jeshi Mkuu ataona inafaa na lazima.
Kwa
mujibu wa kifungu hicho, shughuli/operesheni hizo Amiri Jeshi Mkuu, anaweza
kuamrisha zifanyike ndani au nje ya Tanzania, mfano ushiriki wa jeshi la
wananchi la Tanzania katika kulinda amani nchini Liberia, miaka michache
iliyopita, kushiriki Kongo baada ya Mabutu kuondolewa Msumbiji wakati wa vita
vya ukombozi n.k.
Katiba
pia imeeleza mamlaka mengine ya Amiri Jeshi Mkuu ambaye ndiye Rais katika Ibara
ndogo ya Pili (2) ya kifungu cha 148 kuwa ni pamoja na:-
(a) Mamlaka
ya kuwateua makamanda wa juu katika majeshi ya ulinzi ya Jamhuri ya Muungano.
(b) Kuajiri au kuachisha watu kutoka majeshi ya
ulinzi.
(c) Mamlaka ya kuteua makamanda wa vikosi
mbalimbali vya majeshi ya ulinzi na kusimamisha mamlaka ya askari yeyote katika
majeshi ya Ulinzi na kuhusiana na utumishi wa askari katika jeshi.
Ibara
ndogo ya tatu (3) ya kifungu cha 148, inaeleza kuwa chochote kitakacho fanywa
na askari katika majeshi ya ulinzi, kinyume na amri zilizotolewa na Amiri Jeshi
Mkuu kama zilivyoainishwa katika Ibara ndogo ya kwanza (1) na Ibara ndogo ya
Pili (2) ya kifungu cha 148 cha Katiba kitakuwa ni batili.
Tumeona
kwa kifupi sheria inavyoelekeza kuhusu majeshi na jinsi ya uanzishwaji wake kwa
mujibu wa katiba.
Ki
msingi, katiba ya Jamhuri ya Muungano ya Tanzania, inaelekeza kwa ujumla juu ya
majeshi ya ulinzi na usalama nchini, lakini kwa sheria maalumu zihusianazo na
miundo na utendaji wa majeshi hayo.
Mfano
kuna sheria inayohusu jeshi la ulinzi la wananchi wa Tanzania, yaani “Tanzania
Peoples Defence Act.” Sheria ya Jeshi la Polisi yaani, “The
Police Force Ordinance” na au Jeshi la Magereza, yaani “The
Prisons Services Ordinance.”
Tukirejea
katika suala zima la uwezo wa kuanzisha Jeshi, kwa mtu binafsi, kikundi cha
watu au shirika kama tulivyoona katika utangulizi wa mada ya toleo hili,
tunaona kuwa ni vigumu kisheria kufanya hivyo.
Jambo
hili ni tofauti kabisa na suala la uanzishwaji wa makampuni ya ulinzi, yaani “Security
Companies,” kwani makampuni ya ulinzi husajiliwa na Wizara ya Mambo ya
Ndani na wala si majeshi katika maana nzima ya majeshi ya ulinzi na usalama.
SHERIA ZA
KANISA
Wanaokwenda vitani wanaweza kupewa Sakramenti ya Mpako?
Na Pd. David Mubirigi
Katika
Toleo lililopita tuliishia katika kipengele kilichokuwa kikizungumzia kanuni ya
1003, namna Mhudumu wa Sakramenti anavyoweza kuhudumia. Sasa endelea na mada
hii kama anavyoifafanua Mwandishi.
Baadhi yao au wote wanaweza kushiriki katika kupaka mafuta
iwapo idadi ya wagonjwa ni kubwa.
Sala
inayosomwa na kiongoza-Ibada tu ni, “Kwa mpako huu mtakatifu na kwa pendo
lake kuu, Bwana akujaze/awajaze na nguvu ya Roho Mtakatifu”. Baada ya jibu
la “Amina”, anaendelea kusema: “Akuondoe/awaondoe katika enzi ya dhambi,
akuweke/awaweke huru.
Kwa
wema wake akupe/awape nafuu katika mateso yako/yenu na kukujalia/kuwajalia
neema”. Jibu ni: “Amina”.
Kuhusu
utayari wa kuadhimisha sakramenti hii, kila Padri ameruhusiwa kusafiri na
mafuta matakatifu.
Lengo
ni kumwezesha kuadhimisha sakramenti hii wakati wowote wa ulazima (SC
Rit, Decr., ‘Pientissima mater ecclesia’, Mar. 4,1965;AAS 57(1965),409;DOL
3314; SCC, general directory, ‘Peregrinans in terra’, Apr. 30,1969:AAS 61
(1969),3605; DOL 2616).
Chimbuko
la mwongozo huu ni hati ‘Pientissima Mater Ecclesia’ ya mwaka
1965 iliyotolewa na Idara ya Kiti cha Kitume kuhusu Ibada.
Lakini,
mwongozo huu umepoteza uzito wake kutokana na ruhusa iliyotolewa na Kanuni
ya 999 inayomruhusu padri yeyote kubariki mafuta ya mpako wakati wa
adhimisho la Sakramenti ya Mpako wa Wagonjwa. Ruhusa imetolewa wakati wa
ulazima, kama vile, hatari ya kifo.
WAPOKEAJI WA SAKRAMENTI: Kan. 1004-1007.
Sehemu
hii ya sheria ya kanisa inazo kanuni 4. Kanuni ya 1004 inahusu adhimisho
halali na marudio ya sakramenti. Kanuni ya 1005-1006 zinahusu kesi za mashaka
na dhana katika adhimisho la sakramenti. Mwisho, kanuni ya 1007
inawataja wale wanaozuiliwa kupokea sakramenti hii.
Adhimisho halali:
kan. 1004
Kuhusu
uhalali wa adhimisho la sakramenti, Sheria ya Kanisa imetaja masharti 5 ambayo
ni pamoja na ubatizo, umri wa mang’amuzi, nia ya mpokeaji (kan. 1006), ugonjwa
mbaya au uzee na hali ya kiroho. Kutokana na uwazi wa baadhi ya masharti hayo,
nitajaribu kueleza baadhi tu ya masharti, kama vile, umri wa mang’amuzi na
ugonjwa au uzee.
Kwa
kuwa lengo la kwanza la adhimisho la sakramenti hii ni kuondoa dhambi na
kukamilisha kitubio, kuongeza neema au kurudisha neema iliyopotea kwa sababu
dhambi, mpokeaji hana budi kuwa na uwezo wa kutenda dhambi.
Kwa
hiyo sakramenti hii, haitolewi kwa watoto wachanga au watu waliozaliwa punguani
(kan.99) kwa sababu hawana uwezo wa kutenda dhambi.
Hawajapoteza
neema ya Mungu waliyoipata wakati wa ubatizo (DZ,3536).
Badala
yake, sakramenti hii inatolewa kwa muumini aliyefikia umri wa mang’amuzi au
zaidi. Hata mtu mzima aliyebatizwa wakati wa hatari ya kifo na ameelezwa maana
na umuhimu wa sakramenti hii katika maisha ya waamini, anaweza kupewa sakramenti
hii.
Iwapo
kuna mashaka kama muumini amekwishafikia umri wa mang’amuzi apewe sakramenti
hii kwa masharti, “sub conditione” (kan. 1005).
Sharti
la pili ni ugonjwa mbaya au mkubwa au uzee. Ndiyo maana Mtume Yakobo anasema,
“Mtu wa kwenu amekuwa hawezi? na awaite Wazee wa Kanisa; nao wamwombee, na
kumpaka mafuta kwa jina la Bwana”, (Yak. 5:14). Hayo, pia, ndiyo
mafundisho na desturi ya kanisa (Dz,1698).
Kwa
bahati mbaya, kanuni hii haielezi kuhusu hali ya ugonjwa au uzee ambapo muamini
anapaswa kupokea sakramenti hii. Inataja tu kuwa muumini apewe sakramenti hii
pale ambapo hali yake inaanza kuwa hatarini kwa sababu ya ugonjwa au uzee, “….ob
infirmitatem vel senium in periculo incipit versari”.
Kwa
hiyo, kanuni hii inatoa nafasi kwa waamini (kan.1001) kutumia busara na hekima
zao katika kuamua kuwa afya ya muumini fulani imeanza kuwa hatarini.
Aidha,
kanuni haitaji aina ya ugonjwa, ndiyo maana, hata magonjwa ya akili
yanahusishwa. Siku hizi magonjwa ya akili yameanza kuwa tatizo na tishio kubwa
kwa wanadamu. Kwa hiyo, waumini wenye magonjwa mabaya au makubwa ya akili
wanahitaji kuimarishwa na Sakramenti ya Mpako wa Wagonjwa (Pastoral Care,
27, n. 53). Mgonjwa anaweza kupakwa kabla ya kufanyiwa upasuaji
hospitalini iwapo upasuaji unasababiswa na ugonjwa (Rituale Romanum,
Ordo, 10). Lakini, siyo maaskari wanaokwenda vitani au watu wakunyongwa
kwa sababu hali hizo hazisababishwi na magonjwa au uzee. Maaskari walio vitani
wanaweza kupakwa iwapo wamepata majeraha mabaya. Kuhusu uzee, muumini mzee anaweza kupakwa iwapo ameanza kuwa
dhaifu ingawa uzee siyo ugonjwa (Rituale Romanum, Ordo unctionis
infirmorum eorumqe pastoralis curae, vaticanis, 1972, n. 11).