SIANG’A: Ni bahati Express kupangwa na Simba
Na Mwandishi
Wetu
ALIYEKUWA Kocha
Mkuu wa Simba, James Sing’a amesema sasa imekuwa bahati kwake, kwa timu yake ya
sasa ya Express kukutana na timu ya Simba
katika kundi moja katika Michuano ya Klabu Bingwa Afrika Mashariki na
Kati inayoanza mjini Kigali Rwanda wiki hii.
Habari zilizopatikana jijini Dar es Salaam,
zilimkariri Siang’a akiupongeza Ukuu wa Mungu ambaye amewezesha timu yake ya
Express kukutana na timu ya Simba ya jijini Dar es Salaam, ambayo aliifundisha
kwa miaka mitatu kabla ya kuhamia Express ya Uganda.
Siang’a aliondoka katika Klabu ya Simba
baada ya kuibuka mgogoro anaodai kuwa, chanzo chake kilikuwa ni Katibu Mkuu wa
Simba Kassim Dewji.
Siang’a na Dewji walifikia uhasama hadi
kutumia vyombo mbalimbali vya habari katika malumbano.
Viongozi hao wawili mahasimu Dewji na
Sing’a wote wamekwishaondoka kwenda Kigali Rwanda na timu zao za Express na
Simba, zinamenyana Jumatano hii.
Siang’a amesema mchezo baina ya timu yake
na Simba, ndio utakaodhihirisha wazi kuwa nani bora katika ulimwengu wa soka.
Simba iliyowahi kutwaa kombe hilo mara
sita, imepangwa Kundi B pamoja na Timu za Express ya Uganda na Jamhuri
ya Zanzibar.
Kikosi cha wachezaji 20 wa Timu ya Simba,
kiliondoka Ijumaa iliyopita kuelekea Kigali kwa basi ili kushiriki michuano
hiyo.
Kwa mujibu wa habari zaidi zilizopatikana
jijini, Simba ilitakiwa kuondoka na makocha wawili, Patrick Phiri na msaidizi
wake, Patrick Chamangwana.
Kabla ya kukwaana na Express Jumatano hii,
Simba inarusha kete yake ya kwanza kwa kumenyana na Jamhuri ya Zanzibar
Jumatatu hii.
Hadi sasa mashabiki wa soka nchini bado
wana shauku ya kujua kama Simba itaendelea kuchomoa makucha yake kama
ilivyofanya Machi 3, 2002 katika Uwanja wa Amani wa Zanzibar, ilipoichapa
Prince Louis ya Burundi kwa bao 1-0 na hivyo, kutwaa kombe la mwaka huo.
Wakati huo huo:
Mgogoro wa madai ya fedha za James Siang’a dhidi ya Simba, umeingia katika sura
mpya baada ya suala hilo kufikishwa katika Shirikisho la Soka Duniani (FIFA).
Siang’a amechukua hatua hiyo baada ya
uongozi wa Simba kukataa madai yake ikisema kuwa, haikuwa imemwajiri Kocha
huyo.
Klabu hiyo imesema kuwa, Mkenya huyo aliajiriwa na
kampuni ya Mohamed Enterprises ambayo ni wafadhili wa timu hiyo
na siyo klabu ya Simba.
SIMBA: Yanga wasirukie wasichokijua
Na Joachim
Mushi
Klabu
ya Simba ya Dar es Salaam, imewashambulia vikali mahasimu wao, Yanga kwa
kuingilia madai ya mchezaji Ramadhan Wasso anayetaka ashirikishwe katika mgawo
wa fedha za CAF, kama walivyopewa wachezaji wengine wa timu hiyo.
Meneja wa
Simba, Innocent Njovu, amesema hatua ya Yanga kuwashinikiza wamlipe mchezaji
Wasso kile alichokiita “madai hewa”
ni
kuingilia mambo ya ndani ya klabu nyingine yasiyowahusu.
Njovu
alisema, Yanga haijui lolote juu ya madai ya Wasso na kamwe haiwapasi
kuzungumzia suala hilo wasilolijiua.
“Sisi kama
Simba hatudaiwi pesa zozote na Wasso ama hata Kocha Siang’a kama inavyosikika
huko mitaani na kwenye magazeti. Na ndio maana Wasso hasemi anadai shilingi
ngapi na ni za mshahara upi ama posho gani ambazo alikuwa hajalipwa,” alisema
Meneja huyo.
“Wasso sio
mchezaji wa Simba kwa sasa. Sisi tumewapa motisha wachezaji wa Simba, sasa
kelele zinatoka wapi tena? “ aliuliza Meneja Njovu kwa mshangao.
Akizungumzia
suala la madai ya Kocha Siang’a ya kudhulumiwa pesa zake na klabu hiyo, Njovu
alisema Simba, haidaiwi chochote na kocha huyo kwa sababu haikuwa na mkataba
nae.
Alifafanua
kuwa, Siang’a alikuwa na mkataba baina yake na mfadhili mkuu wa klabu hiyo,
Mohamed Enterprises, na wala klabu haikuhusika na masuala yoyote yahusuyo pesa
na kocha huyo raia wa Kenya.
“Kama kuna
fedha anadai, aende kwa yule aliyewekeana nae mkataba. Huyo ndiye alikuwa
mwajiri wake na angeweza kumpangia kufanya jambo lolote, kama alivyompangia
kuja kuifundisha Simba” alisema meneja huyo.
Hivi karibuni, Kocha Siang’a alikaririwa na
baadhi ya vyombo vya habari akidai kudhulumiwa fedha zake na klabu ya Simba,
baada ya kumalizika kwa mkataba wa kuifundisha kabla ya kuondoka kwenda kufanya
kazi hiyo nje ya nchi.
Yanga Asili
yaiunga mkono FAT
Machumu Manyama na
Libert Lukaya
KUNDI la Yanga Asili, limekiunga mkono Chama Cha Soka chini
(FAT ), kwa hatua yake ya kuvitaka vilabu viwe na vitega uchumi badala ya
kutegemea mapato ya mlangoni.
Akizungumza
na KIONGOZI hivi karibuni jijini Dar es Salaam, Mwenyekiti wa kundi hilo,
Yusufu Mzimba alisema kuwa, umefika wakati kwa vilabu vinavyoshiriki ligi
mbalimbali hapa nchini, kuwa na vitega uchumi vyao na siyo kutegemea fedha za
mlangoni ambazo hazikidhi mahitaji kwa mwaka.
Mzimba
alisema kuwa, iwapo mbinu hiyo mpya ya kubuni na kuanzisha vitega uchumi
itafanikiwa basi, itakuwa njia nzuri ya kuleta maendeleo ndani ya vilabu na
taifa kwa ujumla na tabia ya vilabu kuwa tegemezi itakwisha.
Akifafanua
zaidi Mzimba alisema mpango huo wa FAT, unapaswa kuungwa mkono kwa nguvu zote
na wadau wa sekta hiyo, hususan wapenda michezo, ili waendane na mabadiliko ya
wakati na kuepusha tabia ya vilabu kuwa ombaomba.
Kundi
hilo ambalo limekuwa likilumbana na kundi jingine la “Yanga kampuni” limesema kuwa, vilabu vingi hapa nchini
vinakabiliwa na uhaba wa fedha kutokana na kutokuwa na vyanzo vya mapato vya
kuaminika na visivyo tegemezi.
Hivi
karibuni Chama Cha Soka nchini, FAT kilivitaka vilabu vinavyo shiriki Ligi Kuu
Bara, kuanzisha mpango mpya wa kujiletea
mapato kutoka katika vitega uchumi vingine badala ya kutegemea mapato ya
mlangoni tu.
Kauli hiyo ya FAT, ilikuja kufuatia vilabu vinavyoshiriki ligi kuu bara, kutaka kugawana mapato ya mlangoni, badala ya timu mwenyeji kuchukua mapato yote kama ilivyoamriwa na chama hicho cha soka.