Tunautakia
heri mkutano wa viongozi wa dini na siasa
KATIKA ukurasa wa kwanza wa toleo hili, kuna habari juu ya
uamuzi wa viongozi wa kidini wa kuwakutanisha viongozi wa kisiasa nchini Juni
22, mwaka huu lengo kuu likiwa kujadili suala zima la amani katika taifa letu.
Viongozi
hao wa kidini, wanataka kukaa pamoja na wenzao wa kisiasa ili kuangalia kwa
pamoja ni hatua zipi madhubuti zinazostahili kuchukuliwa, hasa wakati wa
kusimamia na kuendesha zoezi zito na nyeti la Uchaguzi Mkuu unaotazamiwa
kufanyika mwakani, kwa amani, haki na utulivu.
Tungependa
bila kukawia, kuwapongeza kwa dhati kabisa viongozi hao wa kiroho kwa uamuzi
wao wa busara waliouchukua. Viongozi hao, bila kujali tofauti za kiimani,
wamechukua uamuzi sahihi na kwa wakati unaostahili.
Tunasema
hivyo, kwa kuzingatia kwamba katika vipindi vyote viwili vya Uchaguzi Mkuu, ule
wa mwaka 1995 na mwaka 2000, taifa lilishuhudia vitendo vya uvunjaji mkubwa wa
amani na malalamiko makubwa yasiyokwisha, juu ya ukiukwaji wa kanuni za
uchaguzi.
Vyama
vya upinzani, vimesikika mara zote mbili vikilalamika kuibiwa kura na Chama
Tawala, CCM.
Ingawa
sio vizuri kukumbusha machungu yaliyowahi kulikumba Taifa hili, lakini hakuna
Mtanzania asiyejua yaliyotokea Januari 27, 2001, huko Visiwani.
Tunasema
hakuna asiyejua kwani Watanzania takriban 30, waliuawa katika vurugu kubwa za
kisiasa zilizotokea kutokana na kupinga kile kilichoitwa “wizi wa kura”
uliodaiwa kufanywa na Chama Cha Mapinduzi, (CCM).
Baadhi
ya walionusurika katika vurugu hizo, walilazimika kukimbilia nchi jirani, na
hivyo, kwa mara ya kwanza katika historia ya Taifa hili, Tanzania ikawa na
rekodi ya kuwa na wakimbizi nje ya nchi.
Kwa
mtazamo wetu, pamoja na juhudi za makusudi zilizofanywa na baadhi ya viongozi
wa nchi hii na hatimaye kuanzishwa kwa Tume ya muafaka, bado hali ya amani na
maelewano ya kweli haijapatikana baina ya CUF na CCM.
Tunasema
hivyo kwani kila chama kimekuwa kikitoa matamshi mazito yanayoelekeza kwenye
uvunjaji wa amani.
Baadhi
ya viongozi wamesikika, tena bila aibu wakitishia kumwaga damu, ikiwa mpinzani
wao ataiba kura! Yapo madai kwamba, chama kimoja kimeamua kutoa mafunzo ya
kijeshi kwa vijana wake ili wawe tayari kulinda kura zake katika Uchaguzi Mkuu
wa mwakani.
Sisi
tunasema, kwa mtu yeyote mwenye akili ya kawaida, anaweza kutabiri
kitakachotokea iwapo kila kimoja kitaweka “makomandoo” wake 20 katika kila
kituo cha kupigia kura.
Tujiulize
katika mazingira kama hayo, hali itakuwaje ?
Taifa
limeshuhudia kwa namna ya mshangao mkubwa, vitendo vya uharibifu wa mali za
mashirika ya kidini, watu binafsi, na za Serikali kwa sababu ambazo kamwe
haziwezi kuwa za kidini, bali siasa zilizojificha katika mgongo wa dini.
Baadhi
ya watu wanawatisha wenzao na kuwaamuru kuhama toka sehemu moja ya nchi kwenda
sehemu nyingine kwa madai ya kutokuwa wazawa wa eneo hilo. Hii ni hatari sana
na huenda, mkutano huo ukawa wa manufaa makubwa kwa Watanzania.
Sisi
tunasema, ni kweli na dhahiri kuwa licha ya juhudi za kutafuta na kuimarisha
muafaka, bado uadui kati ya CCM na vyama vya upinzani unaongezeka kila siku.
Viongozi
wa kisiasa wanatoleana maneno ya kashfa na kejeli katika mikutano ya hadhara
ama hata katika vyombo vya habari.
Ungetegemea
kuwa uhasama huu ungeishia hapo tu, lakini siyo hivyo. Ndani ya vyama vyenyewe
mambo sio shwari. Viongozi kwa viongozi wanagombana na wanafukuzana bila
mpangilio.
Madai
ya ukiukaji wa katiba za vyama husika ni makubwa. Ndani ya vyama hivyo,
malalamiko ya udikteta dhidi ya viongozi waandamizi wa vyama hivyo, ni mengi.
Ukabila ambao zamani haukusikika, sasa sio jambo la siri tena.
Tunasema,
nenda, CCM, TLP, CHADEMA, CUF, UDP na vyama karibu vyote vya siasa, hakuna hata
kimoja kilichopona katika shutuma za vitendo vya rushwa, udini, ukabila, ukanda
na udikteta! Hii ni aibu na ishara mbaya ya huko tuendako.
Ni
katika hali kama hii, tunapolazimika kuunga mkono hatua ya viongozi wa kidini
ya kukaa pamoja na viongozi wa siasa kila mwaka, ili kuangalia namna ya
kuinusuru nchi yetu isitumbukie katika janga la kutotawalika.
Tunaomba
kila kiongozi wa siasa atakayealikwa, ashiriki kikamilifu na kwa nia thabiti ya
kujenga, kuimarisha na kudumisha umoja wa kitaifa na kubwa zaidi, ahakikishe
chama chake kinashiriki Uchaguzi Mkuu ujao kikiwa tayari kushinda au kushindwa
kwani asiyekubali si mshindani.
Tunasema,
viongozi hao wenye dhamana kubwa katika jamii, wote waondokane na dhana mbovu
za kwamba, ili uchaguzi uwe huru na haki, lazima vyama vya upinzani vishinde
katika uchaguzi, kinyume na hapo, mlolongo wa kesi mahakamani kupinga matokeo;
ni aibu na uchanga wa kisisasa.
Kwa
upande mwingine tunasema, ni aibu kwa Chama kilichokaa madarakani kujijengea
dhana kwamba kikiondolewa madarakani ni fedheha na kwamba, lazima kitumie mbinu
zozote kuhakikisha kuwa, kinashinda.
Kwa
kawaida, matokeo ya dhana hiyo iliyopitwa na wakati, ni mizengwe ya kila mtindo
kujitokeza wakati wa upigaji na kuhesabu kura.
Tunasema, hekima za viongozi wa dini zituongoze na pia,
Uchaguzi Mkuu uliofanyika Kenya na kukipa chama cha NARC ushindi, uwe mfano
kuwa penye mashindano, lazima mshindi apatikane.
Na
Sr. Karoline Pasel OSB Mtwara
MIAKA kadha katika kipindi cha joto
katika Kusini mwa Florida, kijana mmoja akaamua kwenda kuogelea katika Bwawa la
zamani nyuma ya nyumba yao. Kutokana na haraka ya kwenda kuoga katika maji,
kijana huyo alitoka kwa mlango wa nyuma na kuacha viatu, soksi na shati.
Alijirusha majini, hakutambua kwamba kadiri alivyokuwa
anaogelea kuelekea kati kati ya bwawa na mamba alikuwa anaelekea ukingoni mwa
bwawa hilo. Mama yake akiwa ndani ya nyumba alikuwa anachungulia dirishani na
kumwona mwanaye na mamba wakikaribiana.
Kwa huzuni alikimbilia kwenye maji, akiwa anamgumilia mwanaye kwa sauti sana.
Aliposikia sauti ya mama yake, akatambua na kuona na kuogelea
kuelekea kwa mama yake, lakini alichelewa. Alipomfikia mama yake tu, mamba
alimfikia na kumkamata miguu yake, mama alimkamata mtoto wake kwa mikono,
wakaanza mvutano kama vita kati ya mamba na mama. Mamba alikuwa na nguvu zaidi
ya mama lakini mama hakukubali kumwacha mtoto wake.
Mkulima alikuwa anapita akasikia makelele akakimbilia na
akachukua silaha yake na kumpiga risasi mamba yule.
Baada ya majuma hospitalini, yule kijana alipona. Miguu yake
ilikuwa imejeruhiwa vibaya na mamba huyo. Na mikononi mwake kulikuwa na makovu
(mikwaruzo) ambayo kucha za mama yake zilizama katika juhudi za kukaza mikono
ili kumwokoa mwanae mpendwa.
Mwandishi wa habari ambaye alimuhoji kijana huyo baada ya
kupona alimwomba kama angeweza kumwonyesha makovu (michubuko) yake. Yule kijana
akakunja suruali yake. Na kisha kwa furaha akasema ‘Lakini angalia mikononi
mwangu pia, nina makovu mengine makubwa pia. Nimeyapata hayo kwa sababu mama
yangu hakutaka kuniacha nichukuliwe na mamba.
Mimi na wewe tunaweza kujifananisha na mtoto huyu tuna makovu
pia. Hapana sio kwa ajili ya mamba, lakini makovu kutokana na maumivu
yaliyopita. Baadhi hayaonekani na yametusababisha huzuni kubwa, lakini majeraha
mengine ni kwa sababu Mungu amekataa kutuacha tupotee.
Wakati wa mahangaiko yako yupo akikusaidia.
Mpenzi msomaji tafakari yetu hii ya leo inatufundisha kuwa
Mungu anatupenda wewe na mimi, wewe ni mtoto wa Mungu, anataka kukulinda na
kukuhudumia, lakini wakati mwingine tunajiingiza katika matatizo bila ya kujua
kilichopo mbele.
Bwawa la kuogelea la maisha limejazwa mambo mbalimbali na
tunasahau kwamba adui wetu anatungojea kutuvamia. Hapo ndipo shida inapoanza na
kama una makovu mikononi mwako ya upendo wake Mungu furahi sana. Hakukuacha na
wala hatakuacha.
Mungu amekubariki wewe ili uwe baraka kwa wengine. Hauwezi
kujua kama mtu yupo kwenye maisha yake na yanaelekea wapi. Usihukumu makovu ya
mwengine kwa sababu haujui ameyapataje (vipi) na kwa nini?
Sasa hivi watu wanahitaji kujua kwamba Mungu unawapenda. usiwaache.