Atuhumiwa kuvunja banda na kuiba mayai DAR ES SALAAM: MKAZI mmoja wa Temeke,Rashidi Manitu(24) hivi karibuni alifikishwa katika Mahakama ya Mwanzo Temeke kujibu shtaka la kuvunja banda la kuku na kuiba mayai. Iidaiwa na Msoma mashtaka wa mahakama hiyo,Konstebo wa pilisi Moshi Lugama mbele ya hakimu Idd Mbonde kuwa mshtakiwa alivunja banda na kuiba mayai tray 10 zenye thamani ya shilingi 17,500 mali ya Lelona Adamson. Konstebo Moshi aliendelea kudai kuwa mshtakiwa alitenda kosa hilo Oktoba 24 mwaka huu saa 3.00 usiku katika eneo la Temeke Kitombondo na amekana kuhusika na shtaka hilo. Watuhumiwa kuiba sh.8000 DAR ES SALAAM: SADICK Juma (28) na Mwidini Jumanne (26)wote wakazi wa Manzese Mpakani wamepelekwa rumande baada ya kukosa mtu wa kuwatolea dhamana katika shitaka la wizi wa radio yenye thamani ya shilingi 8,000 mali ya Renetus Anthony. Akisoma hati ya shtaka linalowakabili washtakiwa hao ,mosoma mashtaka wa mahakama hiyo Konstebo wa polisi Thobias Anselemo mbele ya hakimu Marry Matoi alidai wa washtakiwa wote kwa pamoja waliiba radio ndogo yenye thamani ya shilingi 8,000 na walitenda kosa hilo Novemba mosi mwaka huu saa 2.00 usiku katika eneo la Magomeni Mikumi. Akana kutishia kumuua mpagaji wake DAR ES SALAAM:KISA Mussa (30) mkazi wa Ubungo Kibo hivi karibuni alifikishwa kwenye mahakama ya Mwanzo Manzese kujibu shitaka la kutishia kumuua kwa maneno ambapo alimtishia mpangaji wake Salome Stephen. Mbele ya hakimu Kwege Mketo ,msoma mashtaka wa mahakama hiyo,Konstebo Leonard Izuya alidai kuwa mshtakiwa alimtishia mpangaji wake kuwa atamuuwa wakati wowote na alitenda kosa hilo Oktoba 9 mwaka huu saa 3.00 usiku katika eneo la ubungo Kibo.Mshtakiwa alikana kuhusika na shtaka hilo na yupo nje kwa dhamana. Atuhumiwa kumpiga mwanamke kwa kichwa DAR ES SALAAM:FADHILI Hassan (17)mkazi wa Magomeni Kagera hivi karibuni alifikishwa katika Mahakama ya Mwanzo Magomeni kujibu shtaka la shambulio ambapo alimshambulia Reheme Bakari kwa kumpiga kichwa usoni. Msoma mashtaka Konstebo Thobias Anselemo alidai mbele ya hakimu Marry Matoi kuwa mshtakiwa alifanya kosa hilo Novemba Mosi mwaka huu saa 11.00 jioni katika eneo la Magomeni Kagera na amekana kuhusika na shtaka hilo.