‘Siasa bila dini ni uendawazimu’

Na Lilian Nyenza

Kanisa halitaacha kutoa mwongozo kwa watu wake hata kwa mambo ya kisiasa ukiwamo uchaguzi kwa kuwa, siasa bila dini ni sawa na uendawazimu.

Aidha, imedaiwa kuwa tabia ya kuwalaghai vijana kuwa ni taifa la kesho, ndiyo inayowadumaza kiakili na kuwafanya watumiwe na wanasiasa kufanya fujo, badala ya kujitokeza kuongoza kwa kufuata taratibu za nchi.

Mkurugenzi wa chama cha kifamilia cha  Undugu Association Tanzania, Padri Baptiste Mapunda, alitoa kauli hiyo katika sherehe za kuuaga mwaka 2004 na kuukaribisha mwaka mpya wa 2005, zilizofanyika katika ukumbi wa Parokia ya  Mt. Yosefu, Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam.

 

Mkurugenzi huyo wa UNDUGU ASSOCIATION TANZANIA alisema kuwa, Tanzania imeanza kuonesha dalili mbaya za machafuko kutokana na baadhi ya watu wakiwamo wanasiasa kuweka mbele ubinafsi.

“Tukikaa kimya huku mambo yanaharibika katika jamii; eti tuwaachie wanasiasa wafanye watakavyo, tutakuwa hatutendi wajibu wetu na hivyo, Kanisa halitaacha kusema ukweli kwa maslahi ya umma hata kama unamkera mtu. Hii ni kwa kuwa tunajua wazi kuwa siasa bila dini, ni uendawazimu ambao mtu hajui akifanyacho kwa kuwa akili yake haijatimia kiroho.” alisema.

Aliitaka jamiii ya Kitanzania ijifunze thamani ya amani na siasa safi kutokana na hali ya amani na usalama katika nchi jirani za Rwanda na Burundi ambayo ni hatari na inasikitisha.

Alisema vita na mauaji yanayoendelea katika nchi hizo, yanasababishwa na uroho wa madaraka wa watu wachache ambao hawajali utu wa wengine.

Aliongeza kuwa, “Siku zote tunapaswa kukumbuka kuwa, amani na mapendo ambayo Mungu ametujalia, tunapaswa kuyaenzi sisi sote kwa kuwa siasa bila dini, ni sawa na uendawazimu.”

Padri Mapunda aliiasa jamii kuendelea kumuomba Mungu ili azidi kuwajalia amani,upendo na utulivu uliopo sasa, kuwa uwepo hata baada ya Uchaguzi  Mkuu kupita.

Amewataka Waamini kuwaombea viongozi wanyanyasaji kama Herode, wabadilike na hivyo, kuongoza nchi kwa haki na akawasihi Watanzania kuyashinda maovu kwa kutenda yaliyo mema.

Hata hivyo, Padri Mapunda amewatahadharisha vijana kujiepusha kutumiwa na baadhi ya viongozi wa siasa, kwa nia ya kufanya fujo katika uchaguzi.

“Vijana mara nyingi wamekuwa wepesi wa kurubuniwa na vijizawadi vidogo vidogo, ili wafanye kile wanachokitaka wanasiasa wabinafsi. Sasa mimi nasema mkae chini na mlitafakari hilo kwa makini. Mtakao angamia ni ninyi na si wao,” alitahadharisha.

Alisema vijana ni Taifa la leo na Taifa bila vijana limekufa, hivyo aliwasihi kuwaheshimu wazazi na walezi ili wapate kuishi maisha marefu na yenye heri duniani, kama walivyojaliwa kuuona mwaka huu mpya.

Naye Mwenyekiti wa Umoja huo, Bw. Benjamini Komba alisema, lengo la Shirika la Undugu, ni kuiunganisha jamii, ikiwa ni pamoja na kuimarisha Ukristo katika kupata hamasa katika kazi ya umisionari, ili ijengeke roho ya umisionari  wa kweli nchini Tanzania.

Bw. Komba alisema kuwa, Shirika limekuwa na mchango mkubwa kwa jamii, kwa kuwa ni chombo cha kuelimisha jamii na kuendeleza mawasiliano na wamisionari wa Afrika ambao wapo ndani na nje ya nchi kwa lengo la kusukuma mbele kurudumu la Injili katika Taifa hili.

Umoja huo haujishughulishi na mambo ya siasa na hauna ubaguzi wa dini, rangi, imani wala itikadi. 

Katika sherehe hizo, Wanaundugu na watu wengine walialikwa na kuhudhuria pamoja na familia zao.

 

 

WARIOBA: Spika, Jaji Mkuu waondolewe

l  Asema Wanawake watatu wamenyimwa Uwaziri Mkuu

l  Tume ya Uchaguzi yamtia hofu

 

Na Mwandishi Wetu

 

WAZIRI Mkuu wa zamani wa Tanzania, Jaji Joseph Warioba amelishauri Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuwaondoa Spika wa Bunge hilo pamoja na Jaji Mkuu wa Tanzania kushika moja ya nafasi nyeti ya nchi.

Nafasi ambayo Jaji Warioba alishauri isishikwe na viongozi hao ni ile ya kukaimu nafasi ya urais, pindi Rais ama Makamu wake wanapokuwa nje ya nchi kikazi ama wawapo katika mazingira yanayoweza kuwafanya washindwe kutimiza majukumu yao, ikiwemo ugonjwa ama hata kifo.

Akihojiwa na gazeti moja la kila wiki hapa nchini hivi karibuni, Jaji Warioba alisema haikuwa sahihi kuwafanya Spika wa Bunge na Jaji Mkuu kukaimu nafasi hiyo na kumwengua mtu muhimu kama Waziri Mkuu na kwamba, anaunga mkono Mabadiliko ya 14 ya Katiba yanayopendekeza kuwaondoa watu hao kushika nafasi hiyo.

Alisema kutokana na mazingira ya sasa, sio jambo la busara kumpa nafasi mtu kama Jaji Mkuu kushika nafasi za kiutawala. Hakufafanua.

Aidha, alisema ingawa baadhi ya nchi Spika huwa wa pili ama wa tatu kwa itifaki ya uongozi, kwa mfumo wa Tanzania ni vema Waziri Mkuu akashika nafasi ya tatu baada ya Makamu wa Rais.

“Makamu wa Rais na Waziri Mkuu ni wasaidizi wa Rais wa moja kwa moja na wanaweza kutekeleza shughuli za Rais vizuri zaidi na kwa urahisi,” alisema mwanasiasa huyo mkongwe nchini katika mahojiano hayo.

Pamoja na kukubaliana na Marekebisho ya 14 ya Katiba hususan Ibara ya 37, Jaji Warioba alipingana na Kifungu cha 51 (2) ambacho kinataka Waziri Mkuu atokane na Wabunge wa kuchaguliwa kutoka majimbo ya uchaguzi, akidai kwamba kimesababisha mawaziri wanawake watatu katika Serikali ya Rais Mkapa ambao uwezo wao wa kushika nafasi ya Uwaziri Mkuu umeonekana bayana kutoteuliwa.

“Katiba imewanyima sifa ya kufikia nafasi ya Waziri Mkuu kwa kuwa wamechaguliwa kwa utaratibu maalum,” alisema na kuongeza kuwa, hawa ni wale ambao ubunge wao hautokani na kuchaguliwa majimboni.

“Kwa hiyo, napendekeza kuwa sharti la sasa kuhusu uteuzi wa Waziri Mkuu liondolewe, na mbunge yeyote awe na nafasi ya kushika nafasi hiyo,” alisema Jaji Warioba.

Kwa upande mwingine, Jaji Warioba ameonesha hofu ya waziwazi kuhusiana na kuundwa kwa kile kitakachoitwa “Tume Huru ya Uchaguzi” itakayowajumuisha wajumbe watano kutoka vyama vya siasa na akasema, kufanya hivyo ni kuvunja misingi ya demokrasia na uhuru wa kweli wa Tume hiyo.

“Mabadiliko ya Ibara ya 74 yanaleta wasiwasi. Ibara Mpya ya 74 (16) inaonesha kuwa Tume ya Uchaguzi itakuwa na wajumbe wanasiasa ambao watawakilisha vyama vya siasa. Badiliko hili linavunja msingi wa kuwa na Tume huru. Hii ni taasisi ya umma na inatakiwa iwe huru kabisa bila kuegemea upande wowote,” alisema Jaji Warioba na kuongeza kuwa, ndio maana chini ya Ibara ya 74 (14 na 15), watu wote wanaohusika na uchaguzi ikiwa ni pamoja na wajumbe  wa Tume, wanazuiwa kuwa wanachama wa chama chochote cha siasa.

Aliongeza kuwa, kuchagua wajumbe wa Tume kutoka vyama vya siasa kutaleta matatizo makubwa kwa vile vyama vya siasa ni vingi na haitawezekana vyama vyote vikubaliane kumchagua mjumbe mmoja kuingia katika Tume.

Alionya kuwa, nchi zenye Tume ya Uchaguzi iliyoundwa kisiasa zimepata matatizo kwenye uchaguzi kwa sababu ziliendesha shughuli zake kisiasa na kuitolea mfano Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar ambayo mwaka juzi ilionesha dalili hizo wakati wa uchaguzi mdogo uliofanyika visiwani humo.

“Wajumbe wa CUF hawakukubaliana na hoja ya kuwazuia wagombea waliowekewa pingamizi na NCCR-Mageuzi. Ingekuwaje kama waliopingwa wangekuwa ni wagombea wa CCM?” aliuliza mwanasiasa huyo.

Jaji Warioba aliitaka Serikali kulinda uhuru wa Tume kwa kufanya mabadilko na kuteuwa wajumbe wake nje ya vyama vya siasa ili kuifanya iaminike na wananchi na hivyo kuondoa matatizo yanayoweza kutokea wakati wa uchaguzi.

 

Amani ina utata – Kardinali

Charles Misango na Joseph Sabinus

 

ASKOFU Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo, ametahadharisha juu ya utata wa amani uliopo nchini na akasema jamii isipochukua hatua mbadala kuukabili, ikubali kulaumiwa na vizazi vijavyo.

Kardinali Pengo aliyasema hayo katika Ibada ya Misa Takatifu iliyoandaliwa na Wanawake Wakatoliki Tanzania (WAWATA), Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam na kufanyika katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Yosefu jijini Dar es Salaam.

Kardinali Pengo alisema amani inayodaiwa kuwapo nchini ina utata kwa kuwa imeanza kutishiwa kutokana na matukio mbalimbali ya uvunjaji wa amani vikiwemo vitisho vya mauaji hivyo, akaitaka jamii kutobweteka na kuhadaika ili nusuru taifa lisiangamie.

 

Alisema “dawa” ya kuepukana na janga hili la kutoweka amani linaloitishia Tanzania, ni kila raia mwenye sifa kujiandikisha na kupiga kura ili kumchagua kiongozi anayefaa vinginevyo, ipo hatari wasioongozwa na Mungu wakawachagulia watu kiongozi asiyefaa.

“Inatisha sana maana kama katika hatua za kujiandikisha tu, watu wanauana, basi ni wazi tuna kila sababu ya kumuomba zaidi Mungu alinde amani yetu…,” alisema.

Katika kudumisha amani nchini, Kardinali Pengo aliwaambia wana WAWATA akisema, “Tusichoke kuomba kabla na baada ya uchaguzi… Tusihadaike na amani iliyopo na badala yake, tumkimbilie Mungu katika kipindi hiki.”

Alionya dhidi ya tabia ya baadhi ya watu kukwepa na kuzembea kujiandikisha na kupiga kura akisema, “Tusibaki kusali tu kanisani wakati wengine wanakwenda kupiga kura…Hii ni hatari kwani tukifanya hivyo tunawapa nafasi wasiofanya tafakari kama hii ya Neno la Mungu, kuchagua viongozi wasiofaa na sisi tukabaki kulalalmika.”

Baada ya ibada hiyo iliyofanyika Jumamosi iliyopita, WAWATA jimboni Dar es Salaam, waliwatembelea wagonjwa wa saratani katika Hospitali ya Ocean Road na kuwapa misaada ya vitu mbalimbali vyenye thamani ya takriban shilingi 3,500,000/=

Msaada huo ulihusisha, dawa za meno, kanga, maziwa ya kopo, kandambili, miswaki na taulo.

Uongozi wa Hospitali hiyo uliwashukuru WAWATA jimboni kwa moyo wao wa huruma na upendo kwa wagonjwa na wenye shida mbalimbali.

Tanzania iko katika vuguvugu la kuelekea katika UchaguziMkuu wa Rais, Wabunge , Madiwani na Wawakilishi, unatarajiwa kufanyika Oktoba mwaka huu.

Kumekuwapo na matukio kadhaa yanayotishia amani ya nchi katika vituo kadhaa vya kuandikisha wapiga kura hususan katika baaadhi ya maeneo ya Tanzania Visiwani.

Hali hiyo pamoja na Uchaguzi wa Serikali za Mitaa na Vijiji uliofanyika Novemba mwaka jana, umesababisha vifo vya watu takriban watatu jambo ambalo limeleta hofu kubwa kwa Watanzania wengi.

 

Serikali inaangamiza upinzani - Prof.

l   ‘Ruzuku ingekuwa chanzo cha migogoro, CCM ingekufa’

 

Na Mwandishi Wetu

 

KITENDO cha Serikali kutoa ruzuku kwa vyama vya siasa vyenye wawakilishi bungeni pekee, kimeelezewa kuwa ni mpango wa kuangamiza mfumo wa vyama vingi nchini.

Mwanzilishi wa Chama cha siasa cha Demokrasia MAKINI, Profesa Leonard Shayo alisema jijini Dar es Salaam kuwa, utoaji wa ruzuku kwa ubaguzi unafanya sera ya siasa ya vyama vingi nchini kuwa ya kinafiki na inayotishia kuviangamiza vyama vichanga.

Shayo ambaye ni Profesa wa Idara ya Hisabati na Komputa ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaamu, alisema ni jambo la kushangaza kuona ‘Baba anamzaa mtoto lakini unapofika wakati wa chakula anamuweka pembeni.’

“Serikali ndiye baba wa vyama vyote na ilikubali mfumo wa vyama vingi, sasa inakuwaje ishindwe kutoa ruzuku kwa vyama vyote vyenye usajili wa kudumu?” alihoji.

Alisema uamuzi wa kutoa ruzuku kwa uwiano wa jumla ya wabunge, unaonesha dhahiri kuwa unafanywa na serikali kwa nia ya kukipendelea chama kilichoshika madaraka kwa kuwa kina wabunge wengi.

Profesa Shayo alisema anashangaa kuona hata baadhi ya vyama vya upinzani eti navyo vikakubaliana na suala hilo, bila kuangalia athari zake huko mbeleni.

 “Ni mbinu tu ilitumika kuvibana vyama vingi na kitendo cha vyama vingine kukubali kucheza mchezo wa siasa bila kuwa na uwanja wa siasa kinaashiria uwezekano mkubwa wa kuwepo viongozi wa vyama waliopandikizwa kuviendesha, ”alisema Profesa Shayo.

Alisema vyama vya kweli vya siasa, ni lazima viendeshwe na nguvu za wananchi katika utaratibu wa kulipwa ruzuku na kwamba, michango kwa vyama, inaweza kutolewa ama na wanachama wa chama husika au vyama vya siasa vyenyewe.

Alisema kukosekana kwa ruzuku kumepunguza jukumu la vyama vya siasa katika kuwaelimisha wananchi na kutangaza sera, jambo ambalo si tu lingewapa mwanga wa kutambua ni kipi chama kizuri, bali pia wangeweza kutambua waanzilishi wababaishaji na wale wasio wababaishaji.

Hata hivyo, amekanusha madai kwamba suala la migogoro ndani ya vyama linasababishwa na ruzuku inayotolewa na serikali.

Aidha, Profesa Shayo amewaasa wananchi kuwa makini na vyama vyenye migogoro na kubainisha kuwa, wanapaswa kuangalia na kuichambua migogoro hiyo ili kujua kuwa, inasababishwa na nini kabla hawajatoa maamuzi.

Alisema huenda kuna njama zinazofanywa na baadhi ya watu, katika kuzua migogoro wakiwa na nia ya kuvidhoofisha vyama vya upinzani.

“Migogoro hii ichunguzwe kwa makini, inawezekana kabisa kwa kiongozi wa chama cha siasa akawa kibaraka aliyepandikizwa kwa lengo la kudhoofisha chama chake na upinzani kwa jumla, kwa maslahi ya aliyempandikiza,” alitahadharisha.

Akaongeza kuwa, “Kama kugombania ruzuku kungekuwa ndiko chanzo cha migogoro, basi migogoro mingi ingejitokeza ndani ya Chama Tawala ambacho ndicho chenye ruzuku kubwa pamoja na raslimali nyingi.”

Amemshauri Rais Mkapa kuwa, pamoja na kufanikisha mambo mbalimbali ya kimaendeleo katika nchi hii, pia hana budi kulisimamia na kuliangalia upya suala hilo.

Alisema hali hiyo itasaidia kila chama cha siasa chenye usajili wa kudumu kipate ruzuku ambayo katika kipindi hiki kinachoelekea katika Uchaguzi Mkuu ili kitajikimu katika kampeni.

“Ni ndoto kutegemea chama kichanga kama cha Demokrasia MAKINI kueneza sera zake kwa wananchi kwa kutegemea nguvu za wanachama peke yake,” alisema Prof.Shayo.

Aliongeza kuwa, “Watanzania wengi ni maskini kiasi kwamba wanashindwa hata kulipia kadi zao za uanachama, sembuse kuchangia gharama za kuendesha chama!” 

 

Makamu wa Mama Mkuu afariki 

l Alizimia kwa miezi mitatu

Na Getruda Kaninka, Sumbawanga

MAKAMU wa Mama Mkuu wa Shirika la Masista wa Maria Mtakatifu Malkia wa Afrika, Sista Martha Ngua, amefariki  hivi karibuni, baada ya kuugua kwa muda mrefu.

Sista Ngua alifariki kutokana na ugonjwa wa shinikizo la damu, lililomsababishia kupooza na kisha kupoteza fahamu kwa muda wa miezi mitatu kabla hajaaga dunia katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Mbeya alikokuwa amelazwa kwa matibabu.

Kwa mujibu wa taarifa za shirika lake zilizolifikia Gazeti hili, Marehemu Sista Ngua alianza kuugua mwanzoni mwa mwezi Julai mwaka jana, alipokuwa katika safari za kikazi katika Konventi ya Jimbo Katoliki la Mbeya.

Akihubiri wakati wa Ibada ya Misa Takatifu ya mazishi ya sista huyo, Askofu wa Jimbo la Mpanda, Mhashamu Paskali Kikoti, alimwelezea Sista Ngua kama mtu aliyejitoa kikamilifu na kwa moyo wote, kufanya kazi za utawa kwa uadilifu, bidii na unyenyekevu mkubwa.

Mhashamu Kikoti alisema, marehemu atakumbukwa pia kwa jinsi alivyokuwa mvumilivu hasa wakati wa magumu na kwa namna alivyojitolea kuwahudumia watu mbalimbali kwa upendo, ukarimu na huruma bila ubaguzi.

Marehemu Sista Martha Ngua alizaliwa Januari 20,1937 katika kijiji cha Matanga, Wilayani Sumbawanga katika Mkoa wa Rukwa, akiwa mtoto wa kwanza kati ya watoto 11 wa mzee Alois Ngua na mama Marselina Nyika.

Baada ya masomo yake ya msingi, alijiunga na Shirika la Masista wa Maria Mt. Malkia wa Afrika, Jimbo la Sumbawanga Desemba 8, 1954, akiwa kama Mpostulanti. Miaka sita baadaye, aliweka nadhiri za kwanza, Novemba 21,1960.

Alipata kozi ya ualimu mwaka 1963, katika Chuo cha Ualimu cha Ndala mkoani Tabora. Mwaka 1974 hadi 1977, alijiunga na shule ya sekondari katika Seminari ya Kaengesa na kuhitimu vizuri.

Oktoba 25, 1970, Marehemu Sista Ngua, alijiweka wakfu kwa nadhiri za daima. Alifanya kazi za kitume katika parokia mbalimbali kabla ya kuchaguliwa kuwa Mama Mkuu wa Shirika tangu mwaka 1989 hadi 1995.

Aidha, alichaguliwa kuwa Makamu wa Mama Mkuu wa Shirika hilo kuanzia mwaka 2001, na kushikilia nafasi hiyo hadi alipofariki Novemba 17, mwaka jana. Mungu aiweke roho ya Marehemu Sista Martha Ngua mahali pema peponi, AMINA