TFF mpya
ituunganishe - WADAU
Na Machumu Manyama
UONGOZI
mpya wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) chini ya Rais Leodgar Tenga,
umepongezwa kwa kuchaguliwa kwake lakini umetakiwa kwanza, kuunganisha vyama
vikuu vinavyosimamia mchezo huo ili kufanikisha azima iliyokusudiwa na
Shirikisho hilo.
Wadau mbalimbali wa soka
waliyasema hayo, baada ya kufanyika Uchaguzi Mkuu wa kutafuta viongozi wa
Shirikisho hilo katika Hotel ya Golden Tulip jijini Dar es Salaam hivi karibuni
walipozungumza na KIONGOZI kwa nyakati tofauti.
Walisema iwapo uongozi huo mpya
utayafanya yale waliokuwa wakijinadi wakati wa kuomba nafasi za uongozi, basi
huenda soka la Tanzania likafanikiwa na kuepusha ile aibu iliyodumu kwa
takribani miaka 10 nchi ikiwa msindikizaji katika mashindano ya kimataifa.
Mwenyekiti wa Kundi la Yanga
Asili Bw. Yusuf Mzimba alisema, kutokana na uongozi uliopita kuwa mbali na
wadau mbalimbali wa soka pamoja na
Baraza la Michezo la Taifa (BMT) na Umoja wa Vilabu Nchini (UTAFOC),
Uongozi huu mpya unapaswa kuwa karibu na vyama hivyo hasa kwa kushirikiana katika
kutoa maamuzi ya pamoja ili kuendeleza soka.
Alisema kuwa, katika uongozi
uliopita kulionekana kuwepo kwa uhusiano mbovu na vyama hivyo, hali iliyofanya
mawasiliano ya pamoja kuwa magumu huku kila mmoja akitoa maamuzi yake binafsi.
“Ni wakati sasa kwa uongozi
mpya kuweka uhusiano mzuri ili kuwepo kwa mawasiliano ya kutosha kutoka pande
hizo ambazo ndizo wasimamizi wakubwa wa soka letu,” alisema.
Naye mpenda michezo
aliyejitambulisha kwa jina la John Richard alisema hivi sasa jukumu kubwa alilonalo Bw. Tenga na viongozi
wenzake ni kuhakikisha matatizo yaliyokuwepo hapo awali ambayo yalikuwa kikwazo
katika maendeleo ya soka yanaondolewa
ili watimize matakwa ya Watanzania kuendelea kisoka tunapoanza mwaka huu mpya.
Aliongeza kusema kuwa,
viongozi hao wanapaswa kuepuka kupindisha kwa kanuni na sheria za soka
zilizosababisha migongano ndani ya shirikisho hilo awali.
Alisema ni wakati sasa kwa TFF
mpya, kusimamia kikamilifu sheria na taratibu za soka kwa kuwa ndio muhimili na
mwongozo wa maendeleo ya soka karibu katika kila nchi duniani.
Wadau hao walisema hawana wasiwasi na viongozi waliorithi madaraka hivi sasa, kwa kuwa wanawajua kuwa ni wakereketwa na watu wenye uchungu na mpira wa Tanzania, hivyo wamewatakia kila la kheri viongozi hao.
ASHANTI
yatahadharisha Ligi Kuu
Na Machumu Manyama
BAADA ya kufanikiwa
kupanda daraja msimu huu na kushiriki Ligi Kuu ya VODACOM Tanzania Bara
2005, timu ya soka ya Ashanti ya Ilala, imepania kufanya kweli katika ligi hiyo
inayotarajiwa kuanza baadae mwaka huu.
Katibu
Mkuu wa timu hiyo, Arafati Bakari ameliambia KIONGOZI, hivi karibuni jijini Dar
es Salaam kuwa, mwendo waliotoka nao katika Ligi Daraja la Kwanza, wanatarajia
kuuendeleza hata katika Ligi Kuu.
Alisema,
Watanzania wasubiri kuona soka la kisasa kutoka kwa timu yake inayoundwa na
wachezaji wasio na majina makubwa kama ilivyozoeleka kwa timu nyingi zinazo
shiriki Ligi Kuu.
Katika
kuimarisha kikosi chao, hawatarajii
kuwasajili wachezaji wakongwe na walio na majina makubwa katika medani ya soka
nchini badala yake, watasajili wachezaji chipukizi ili waoneshe uwezo wao.
“Lengo
letu ni kuinua vipaji vya chipukizi, kwa hiyo tutawapa nafasi zaidi, ili nao
wauoneshe umma wa Watanzania uwezo wao,
watoto wenye vipaji tunao (Ashanti),” alitamba Bakari.
Aliongeza
kuwa, katika kujidhatiti na ligi hiyo kubwa nchini, wanatarajia kuanza mazoezi
yao hivi karibuni, huku wakiwa na kikosi cha wachezaji 25.