SHEREHE ZA KUZALIWA MKOMBOZI YESU KRISTO (KRISMAS/NOELI-2004)
WAZO kuu la
Krismas 2004 ni “Haki na Amani Inayothamini Uhai wa Mwanadamu.” Ndugu zangu
waamini, leo tunaadhimisha sherehe za kuzaliwa kwake Yesu Kristo, Mwana wa
Mungu. Kanisa linatuongoza pangoni Bethlehemu kutuonesha Neno wa Mungu
aliyetwaa mwili (Umwilisho) katika Bikira Maria.
Katika hali ya unyonge, Mungu
anakaa nasi- “Immanueli” ili atuondoe katika mauti ya dhambi. “Watu wale
waliokwenda katika giza wameona nuru kuu; wale waliokaa katika nchi ya uvuli wa
mauti, nuru imewaangazia” (Isaya 9:2).
Aya hii ya Nabii Isaya
inahitimisha matumaini ya wengi wanaotembea katika giza la dhambi. “Mimi ni
njia ya ukweli na uhai. Hakuna awezaye kwenda kwa Baba ila kwa kupitia kwangu” (Yoh
14: 6).
Kwetu sisi tuliotembea wiki
nne za Majilio tukitafakari umaana na umuhimu wa siku ya leo, bila shaka tuna
kila sababu za kuimba kwamba tumefika. Lakini, furaha hii imesongwa na wasiwasi
mkubwa, kwani hali ilivyo nchini mwetu na ulimwenguni kwa jumla, si ya furaha
tunayotazamia sote kwani watu wengi usiku wa leo wanaomboleza kwa sababu ya
kukosa haki na amani iliyo zawadi ya Sikukuu ya Krismas.
Krismas ni Haki na Amani
iliyothamini Uhai
Sababu kuu ya “Umwilisho” ni upeo wa upendo wa Mungu kutaka
kutembea nasi kwa hali zote isipokuwa dhambi. Ni Mungu aliyetuumba kwa mfano
wake amependa kuturudishia Amani na Uhai uliopotea kwa sababu ya dhambi. Hivyo,
uwepo wa Mungu kwa binadamu, ni hakikisho la uwepo wa Haki na Amani iliyo tunda
la uhai wetu.
Leo katika mji wa Bethlehemu
amezaliwa mtoto. Kitendo cha kuzaliwa katika familia zetu kila wakati ni zawadi
na furaha kwa familia nzima.
Uhai ni zawadi inayotoka kwa
Mungu kwani Mungu tunayemwabudu yu hai. Hivyo, zawadi ya uhai- Mungu kuzaliwa
kati yetu.
Je, ndugu zangu, ni kwa namna
gani sisi tunaenzi na kuutunza uhai? Kitendo cha vyombo vya dola kusajili vituo
vya kuharibu na kuondoa uhai kwa kisingizio cha “uzazi wa majira”
ni kinyume cha sherehe za leo.
Nchini mwetu kuna utitiri wa
vituo vya uzazi wa majira na shughuli kubwa za vituo hivi ni
kuharibu uhai. Sera ni kwamba, kadiri wanavyoweza kutoa dawa nyingi za kuharibu
au kusitisha mimba, ndivyo wanavyo jipongeza na kuzawadiwa na wale waliowatuma.
Enyi viongozi wetu, si kila
linalofaa pale China, America na Ulaya linafaa pia Tanzania. Kitendo cha
Serikali zetu kufumbia macho vituo hivi ni kutowajibika na kufanya Katiba ya
nchi inayolinda uhai wa raia kuwa kejeli! Jueni ya kwamba, mamlaka yoyote ina
uwezo wa kugeuza mabaya kuwa mazuri, lakini hamna ruhusa ya kufanya mazuri kuwa
mabaya!
Mazingira ya mahali
alipozaliwa Mkombozi wa Ulimwenguni tunayemwadhimisha, yanaonesha wazi kabisa hali ilivyokuwa wakati wake.
Alizaliwa horini, mkiwa, masikini aliyekataliwa na wote wenye nyumba za
kupanga.
Kristo alizaliwa katika ulimwengu wa chuki na maovu mengi, haki
ilikuwa ni bidhaa ya kununua. Utaifa na kabila la wazazi wake umemfanya
Mkombozi wa ulimwengu kuzaliwa katika pango na kitanda chake kuwa hori la
ng’ombe!
Ndugu zangu, hali ikoje
ulimwenguni na hususani Tanzania yetu? Mara nyingi kipimo cha haki za raia
kimekuwa si uraia wake na ubinadamu wake ila chama chake cha siasa, dini yake,
kabila lake, uwezo wake wa uchumi na mahali alipotokea au anapoishi.
Kitendo cha wana usalama
kuingilia Mahakama ni ashirio wazo la kutokuwa na utawala wa sheria. Mfano
mzuri ni wa waamini Wakristo huko Kiuyu Pemba walionyimwa na vyombo vya usalama
na utawala kusali katika Kanisa lao baada ya Mahakama ya Mwanzo kuamua vingine?
Je, huu ndio utawala bora wa
sheria? Ni zaidi ya miezi 10 sasa tangu ajali ya gari la Skuli ya Tomondo
kugongwa; hakuna kesi kwani aliyesababisha ajali hii ni mzito kiuchumi! Mnyonge
akimbilie wapi? Na hali kama hii itaendelea mpaka lini? Kiini cha sherehe ya
leo ni tangazo kwamba ,maovu hayana nguvu tena ulimwenguni! Tutafanya nini ili
haya yawe kweli?
Haki na Amani ya Kweli ni
katika Kuwajibika
Changamoto za sherehe ya leo,
ni kwa namna gani tunamwishi Immanuel- Mungu pamoja nasi?
Kamwe hatuwezi kusema Mungu
yupo pamoja nasi kama hatutashughulikia masuala nyeti ya HAKI za wote na hasa
wanyonge. Mboni ya utawala wa sheria ni HAKI kwa wote na uwajibikaji wa vyombo
vilivyopewa jukumu la kutekeleza haya. Kutowajibika kwa vyombo vya dola athari
zake ni kubwa na za hatari.
Matukio yaliyotokea wakati wa
chaguzi za mitaa huko Tanzania bara na mengine yaliyotokea huko Kusini Pemba,
wakati wa uandikishaji wa daftari la wapiga kura, ni matunda ya
kutowajibika kwa waliokabidhiwa jukumu
hilo.
Kitendo cha kuweka raia
katika vituo vya kupigia kura kwa muda mrefu kwa sababu za uzembe au ubinafsi
ni kinyume cha utawala wa sheria na demokrasia, na hivyo, Kanisa linalaani kwa
hali zote umwagaji damu uliotokea huko Pemba na Dar es Salaam na linaagiza
wahusika wawajibishwe kisheria.
Propaganda za kuwagawanya
Watanzania kwa nadharia za Uzanzibari na Uzanzibara na vitendo
vya kutishia raia juu haki ya kujiandikisha kupiga kura ni kinyume cha Katiba
ya Muungano na hivyo, wahusika wawajibishwe.
Enyi viongozi na wana siasa
mnaochochea fikra za Uzanzibari na Uzanzibara, jifunzeni kwa majirani zetu.
Ujumbe wa Kristo ni iweni wapenda amani wa nchi yenu kuliko wa madaraka kwa
njia ya upanga.
Ndugu zangu, wengi wa jamaa
zetu wapo magerezani miezi na miaka wakisubiri haki. Vijana wetu wengi
wanatumika kama vitega uchumi vya wachache wenye uchu wa mali na madaraka.
Wengi wa wanajamii
wameathirika kwa dawa za kulevya si kwa hiari yao, ila kwa shinikizo la
umaskini.
Asipofanya hivyo ataishije?
Wengi wa jamaa zetu ni waathirika wa UKIMWI kwa sababu ya kutojua, kutowajibika
na kwa sababu ya anasa bila wajibu. Haya yote ni kwa sababu ya kutowajibika na
hivyo kupotea kwa AMANI. Mungu Immanueli anayetembea nasi anatualika sote
tuwajibike ili tupate yale mema aliyopenda tuyaishi.
Umaana wa Mungu Pamoja Nasi-
Immanuel:
Kila binadamu aliyeubwa kwa
mfano na sura ya Mungu ana uwezo wa kutambua kwamba Mungu ni muumba wa vyote na
mbele yake binadamu wote ni sawa. Mungu huyu aliye chanzo cha kila mmoja wetu
hatutakii maovu ila mazuri, na ndiyo maana anakuja kwetu kwa hali ya ubinadamu
wetu.
Si kweli kwamba Mungu ameumba
matabaka ya watu. Matabaka ya watu ni mavuno ya mwanadamu kushindwa kutumia
uhuru aliomzawadia Mungu.
Sababu za vita ya kwanza na
ya pili ya ulimwengu, ni wanadamu wa nchi za viwanda kutaka kutawala ulimwengu
kwa nguvu ya vita ya silaha. Nia ya kutawala ulimwengu na hasa ulimwengu wa
nchi maskini bado ipo pale pale lakini, kwa muundo na falsafa nyingine.
Nia hii inatekelezwa kwa kasi
mno chini ya mwavuli wa “utandawazi” na “ubinafsishaji” unaolenga
kumiliki njia zote za uchumi wa nchi masikini! Je, ni nani asiyejua nguvu ya
utawala ni uchumi wenye nguvu? Mungu anayetembea nasi ni Mungu wa haki kwa
wote.
Aidha, si kweli kwamba
wawekezaji nchini hawafahamu umuhimu wa haki ya kila mtu kuishi kwa jasho lake,
lakini ni nani anayewahalalishia kwamba mwekezaji ana mahitaji zaidi ya
mwenyeji anayemwezesha kuzalisha ?
Mishahara, marupurupu na
faida wanayopata wawekezaji ikilinganishwa na wasomi na wahudumu Watanzania, ni
kielelezo wazi cha ukoloni mambo leo na muundo endelevu wa matabaka ya watu!
Ili ulimwengu utambue Mungu
tunaye msheherekea leo kuwa ni Mungu wa
wote, vyombo husika vidhibiti unyanyapaa wa raia wanaofanyiwa na wawekezaji.
Ndugu zangu, shangwe ya usiku
huu na kipindi chote cha Krismas ni kwamba; Mungu anazungumza nasi kwa mara ya
mwisho kwa njia ya mwiliisho-Mungu kuwa mwanadamu ni ukweli ambao hauwezi
kuondolea kwani ni yeye mwenyewe amependa iwe hivyo.
Ni Mungu amejishusha ili
aweze kutuinua kwa hali zote. Hiki ni kielelezo wazi kwamba anatupenda na yupo
nasi. Yeye ni uhai wetu, muda wetu na anasafiri nasi katika yote.
Ni Mungu anayesema kwa maneno
ya Nabii Isaya; “Kwa ajili ya Unguja na Pemba sitanyamaza, na kwa ajili
ya Tanzania sitatulia, hata haki yangu itakapotokea kama mwangaza, na wokovu
wangu kama taa iwakayo.”
Tumwombe atembee nasi kipindi
chote cha matayarisho ya Uchaguzi Mkuu wa 2005. Tumwombe hekima yake na tuweni
wavumilivu na wenye subira katika kusikiliza sauti yake.
Mungu Immanuel abariki watu
wa Tanzania, Mungu Immanuel abariki Afrika na Mungu Immanuel abariki jamii yote
aliyopenda kuigawia upendo wake.
Nawatakieni
nyote kila Baraka na Amani ya Mungu Immanuel.
Familia takatifu chimbuko la utakatifu
l Ndoa
ni kazi ngumu, lakini muhimu
l
Kwanini wengine hawaoi au kuolewa ?
Na
Furaha Nakulele
KWA kawaida,
neno familia linaposikika, mara moja mtu hukumbuka BABA, MAMA na WATOTO. Yesu,
Maria na Yosefu ni mfano bora wa Familia Takatifu ambayo kubwa zaidi,
inaheshimu tunu ya UHAI.
Ni kwa mantiki hiyo,
tunapozungumzia juu ya KRISMAS na kuisherehekea, tunazingatia kuwa, Maria na
Yosefu walizingatia na kuuheshimu uumbaji wa Mungu hasa juu ya uhai, ndiyo
maana kamwe, hawakufanya jaribio lolote la kumuuua Yesu, baada ya kuzaliwa, au
hata KABLA YA KUZALIWA ; kwa njia ya utoaji mimba (ABORTION).
Ni kwa mamtiki hiyo,
tunaposherehekea Krismas ya mwaka huu, wote hatuna budi kutambua, kuwa chanzo
cha sherehe hizi ni wito wa ndoa ambao ndio asili ya miito yote na hivyo,
kwamba ndoa inatarajiwa kuwa inayoleta FAMILIA TAKATIFU duniani, isiyo na
magomvi, mauaji, masengenyo, UTOAJI MIMBA na vitu vingine vyovyote
visivyoendana na mapenzi ya Mungu.
Ni kwa msingi huo, tuanze
toleo hili kwa kuangalia NDOA hasa kwa mujibu wa Kanisa Katoliki.
Kwanza ijulikane kuwa, kuna
aina tatu za ndoa ambazo ni Ndoa yaKimila, Ndoa ya Kiserikali na Ndoa Takatifu
ya Kikristo.
NDOA
YA KIKRISTO
Kwa maneno mengine, Ndoa ni
agano linalowekwa kati ya mwanaume na mwanamke wabatizwa mbele ya Mungu ili
wawe mke na mume.
Kwa mujibu wa Maandiko
Matakatifu, agano hili linawafanya wabatizwa wawe mwili mmoja wakishiriki haki
zote za ki-ndoa pamoja na mafao ya kijamii yatokanayo na hali ya ndoa.
Ndoa humpa uwezo na mamlaka
mwanamke na mwanamme kuishi pamoja wakishirikiana na kujengana na kutekeleza
upendo wa ki-Mungu (Mwa. 2: 20b - 24).
Ndoa ina malengo makuu mawili
yaani, kuwafanya wanandoa kushirikishana upendo unaowawezesha kuishi katika
umoja, pamoja na kuendeleza tendo la uumbaji, yaani kuleta uhai mapya, yaani
kuzaa watoto kama alivyozaliwa MTOTO YESU.
1Yoh. 1: 8-16, Mwa. 1: 22.
Mwasisi wa ndoa ni Mungu
mwenyewe Mungu akishawaumba, mwanamme na mwanamke hupendana kati yao; huwa sura
ya mapendo kamili na daima ambamo Mungu ampenda mtu.
Kwamba mwanamme na mwanamke
waliumbwa mmoja kwa ajili ya mwingine, maandiko yanathibisha (Mwa. 2:18, Mwa. 2:24, Mt 19:6)
Mwanzoni mwa maisha yake,
Yesu alifanya ishara yake ya kwanza kwa ombi la mama yake wakati wa arusi ya
Kana (Yoh.2 : 1-11)
Hapo kanisa laona maana kubwa
ya uwepo wa Yesu katika arusi ya Kana. Linaona uwepo uthibitisho wa uzuri wa
ndoa na tangazo kwamba:- ndoa itakuwa ishara halisi ya uwepo wa Kristo.
Ruhusa iliyotolewa na Musa ya
kumwacha mke ilikuwa ni kibali kilichosababishwa na ugumu wa moyo, (Mt. 19: 8).
Kwa hakika yake umoja wa ndoa ya mume na mke hauvunjiki kwani Mungu mwenyewe
aliunganisha. (Mt. 19:6). Kutengana kunakoeleweka ni kwa kufa mmoja.
Vitabu vya Ruthu na Thobiti
vyatoa ushuhuda wa kusisimua wa maana ya ndoa iliyoinuliwa ya uaminifu na ya
upole.
Yesu mwenyewe anatambua hilo.
Ndio maana yeye mwenyewe anatoa nguvu ya neema kwa ajili ya kuishi ndoa kama
mtazamo mpya wa ufalme wa Mungu. Kwa kumfuata Kristo, kwa kujikania wenyewe, na
kwa kuchukua kila mmoja msalaba wake, watu wa ndoa wataweza kupokea maana ya
asili ya ndoa na kuishi kwa msaada wa Kristo (Mt. 19:11)
Kama ndoa ina yote hayo
mazuri kwa nini baadhi hawaoi na
hawaolewi, mfano Mapadre na Watawa?
Shirika la Kutetea Uhai
(PRO-LIFE), Tanzania linasema, “Kristo ni kiini cha maisha yote ya Kikristo.
Kifungo cha uhusiano naye, huchukua nafasi ya kwanza kabla ya vifungo vingine
vyote, vya kifamilia au vya kijamii. (LK. 14 : 26, Mk. 10 : 28 - 31), Kristo
mwenyewe amewaalika mapadri, watawa kumtafuta/kumfuata katika mtindo huu wa
maisha ambamo yeye anabaki mfano.’
Linaongeza, ‘Sakramenti ya
ndoa na ubikira (useja) kwa ajili ya ufalme wa Mungu yatoka kwa Bwana mwenyewe.
Ni yeye anayeyapa maana yao kulingana na neema inayotakiwa, kuyaishi kulingana
na matakwa yake na maana ya kikristo ya ndoa, haya mawili hayatengani na
yanaimarishana.’
Ieleweke wazi kuwa, watendaji
wakuu wa agano la ndoa ni mwanamme na mwanamke waliobatizwa, walio huru kufanya mapatano ya ndoa na wanaonesha
kwa hiari ukubaliano wao.
Kama hivyo ndivyo, labda mtu
anaweza kujiuliza kuwa, kuwa huru maana yake nini ? Ni kutokuwa chini ya
shuruti na kutokuwa na kizuizi kutokana na sheria ya maumbile au Kanisa. (CIC,
Can 1057 #1) NB. Kama uhuru
unakosekana, ndoa ni batili.
FAMILIA
Familia hujengwa na Baba,
Mama na Mtoto au Watoto. Kwa kawaida, familia takatifu ni fam,ilia ambao wadau
wake wote, wanapendana, wanaheshimiana, wanasameheana, wanasali pamoja na
wanashiriki shida na raha mpaka mwisho lakini, kikubwa zaidi, yote hayo
wanayafanya ili kutimiza mapenzi ya Mungu.
Wazazi wana jukumu kubwa la
kuwajenga mazingira mazuri ya familia yaani, malazi, mavazi, chakula,
elimu na mahitajin mengine.
PRO- LIFE, Tanzania inasema,
‘Familia kama hifadhi takatifu ya uhai, itambue kuwa zawadi kubwa sana na yenye
thamani kubwa sana katika ndoa ni watoto. (LG &1, Zab. 128:3). Hii ndiyo
maana ulimwengu sasa umepewa zawadi ya UKOMBOZI ; yaani KUZALIWA KWA YESU KRISTO.
Kristo alipenda kuzaliwa na kukua katika Familia
Takatifu ya Yosefu na Maria. Kanisa si kitu kingine ni “Familia ya Mungu “ ,”ni
kanisa la nyumbani.”
Familia ni muhimu sana, kiasi
kwamba nafasi yake katika kujenga utamaduni wa uhai haiwezi kuchukuliwa na kitu
kingine.
Jukumu la malezi si la mtu
mmoja ni la wote, ni la jamii nzima.
Kama kanisa la nyumbani,
familia imeitwa kutangaza Injili ya Uhai.
Familia
isali ili kumtukuza na kumshukuru Mungu kwa zawadi ya uhai.
Haki za familia zizingatiwe.
NDOA
NA FAMILIA:
“Mungu akaumba mtu kwa mfano wake, kwa mfano wa Mungu
alimuumba, mwanaume na mwanamke aliwaumba, Mungu akawabarikia, Mungu akawaambia
zaeni mkaongezeke…” (Mwa 1: 26-27).
“Sasa huyu ni mfupa katika mifupa yangu, na nyama katika nyama
yangu. Kwa hiyo mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye ataambatana na
mkewe, nao watakuwa mwili mmoja” (Mwa 2: 23-24)
Msingi wa familia unatokana na katika Maandiko
Matakatifu yanayoibua dhana zifuatazo, mwanaume na mwanamke wanaounganika na
kuunda familia, wameumbwa kwa mfano wa Mungu
Binadamu ni kiumbe
kilichobarikiwa na Mungu, uzao ambao ndio tunda la mwunganiko wa mume na mke
umebarikiwa
Watoto, yaani uzao ni baraka
itokayo kwa Mungu, ni baraka inayoendeleza tendo la uumbaji ambalo binadamu
anashiriki pamoja na Mungu
“Kutozaa kwa makusudi, au
kuzuia kuzaa bila sababu yoyote ni kuzuia tendo la uumbaji ambalo binadamu
amepewa na kubarikiwa na Mungu na kama lingefanyika katika familia ya Maria na
Yosefu, ulimwengu huu usingepata Mkombozi na badala yake, ungeamia,” linasema
Shirika hilo la kutetea uhai, tawi la Tanzania kupitia Mwenyekiti wake, Bw.
Emil Hagam.
Linasema, Mke na mume huunda
muunganiko usioweza kugawanyika; kila mmoja ni mali ya mwezake, na kwa ajili ya
mwenzake. Hawa, huunda familia ya pekee nje ya wazazi wao wakishiriki agano
lisiloweza kuvunjwa
Sasa, katika dunia hii yenye
mkanganyiko wa mawazo, dhana ya familia inaweza kuelezwa kwa namna mbalimbali
kutegemeana na mwelekeo wa taaluma na lengo la mfasiri.
Mwanamume na mwanamke
walioungana katika ndoa, pamoja na watoto wao ndio wanaounda familia. Familia
kama taasisi ipo hata kabla mamlaka za kijamii hazijaitambua na ambazo zina
wajibu wa kuitambua. Hii ndiyo tafsiri ambayo kwayo tafsiri nyingine zozote
zihusizo familia zitarejea.
Kwa kuumba mwanamume na
mwanamke, Mungu alikusudia kuunda familia ya binadamu na kuitengenezea
mazingira maridhawa ya makubaliano. Wanafamilia ni wale wanaokaa na
kushirikiana kijamii pamoja, lakini kila mmoja akiwa na hadhi yake.
Silika
ya familia ya Kikristo
Agano
la ndoa:
Wakati wote familia
imetambulika kama msingi na namna ya kueleza tabia ya kijamii ya binadamu.
Familia kwa hiyo ni muunganiko wa watu ambao namna yao ya kuishi na kukaa
pamoja ni kwa njia ya “Komunioni”- - muunganiko wa watu.
Ndoa ni agano ambalo kwalo
mwanaume na wanamke kila mmoja hujitoa kwa mwenzake na kila mmoja anamkubali
mwenzake kama mwenzi na mshirika wake wa maisha.
Mwuungano wa hiari wa
mwanamume na mwanamke.
Ni binadamu tu mwenye uwezo
wa kuamua kwa hiari juu ya kuunganika pamoja kwa msingi wa uchaguzi wa hiari.
Katika ndoa mwanamume na mwanamke wanaungana kiasi cha kuwa mwili mmoja (Mwa.
2:24). Japo ni binadamu wawili walio tofauti wanao uwezo wa kuishi pamoja
katika ukweli na upendo.
Uzao
wa binadamu:
Muunganiko unaotokana na ndoa
huleta furaha na faraja ya uzao wa binadamu wapya. Kwa hiyo, kwa tendo hilo
wazazi hushiriki na Mungu Muumbaji katika kuumba na kuzalisha kiumbe kipya.
Mungu anashiriki katika ubaba wa mzazi wa kiume na umama wa mzazi wa kike katika
kuleta uhai mpya.
Sifa za familia kwa kadiri ya
barua ya Papa Yohane Paulo II: “Families
of the World”.
Familia halisi ni taasisi ya
msingi ya jamii, inayojengwa katika uhalisi wa binadamu, na yenye kujikita
katika muunganiko wa hiari wa mwanamme na mwanamke katika agano la maisha ya
ndoa kwa ajili ya Kushibisha hamu za moyo wa binadamu za kutoa na kupokea
upendo, Kuwapokea na kuwalea watoto katika maendeleo yao ya mwili na akili na Kushirikiana makazi ambayo huunda msingi
wa maisha ya kijamii, kielimu, kiuchumi na kiroho.
Mengine ni Kujenga uhusiano
na kupasisha kizazi kipya pamoja na Kutoa huduma kwa wahitaji mbalimbali.
Familia
kama Fumbo la Kanisa
Familia ya
Kikristo inajifunua wazi na kutambulika kama jumuiya na wanakanisa, na kwa
msingi huu familia ni kanisa la (mwanzo) nyumbani. Hii ni jumuiya ya imani,
matumaini na mapendo.
Familia hii ni muunganiko wa
watu, ishara na mfano wa muunganiko wa Baba na Mwana katika Roho Mtakatifu.
Katika uzazi wa watoto na kuwaelimisha tunarejeshwa kutambua uumbaji wa Mungu
Baba.
Kwa hiyo, familia inaalikwa
kuishi maisha ya sala na ya sadaka ya Kristo. Sala za kila siku zinaimarisha
upendo na hivyo kuwezesha kazi ya uinjilishaji na umisionari kufanyika.
Familia imepewa jukumu la
kutoa huduma ya kujenga ufalme wa Mungu kama mshiriki katika maisha na
umisionari wa kanisa. Katika familia matendo ya kikanisa ya uinjilishaji,
ufundishaji na uelimishaji hufanyika.
Matendo hayo hufanyika
mithili ya mama kanisa anavyowezesha kizazi kuendelea kufundisha na kujenga
familia ya kikristu. Familia hutekeleza utume wake wa kikanisa ndani na nje ya
kanisa.
Katika familia wanandoa
wanaishi kisakramenti, na hivyo ndoa inayojenga msingi wa familia inaonekana
kama sakramenti ya kutakatifuza na kama tendo la ibada au kuabudu.
Wajibu
wa familia
Familia kama taasisi iliyo
wazi na ya msingi ina wajibu mbalimbali miongoni kwa watu wanaoiunda.
Mwandishi wa Barua kwa
Waefeso anatujulisha wajibu wa kila mmoja wa watu wanaounda familia, mume, mke
na watoto.
Mwandishi anatukumbusha kuwa
wajibu wa msingi ni ule wa uhusiano. “Kila mmoja amstahi wenzake kwa sababu ya
kumcha Kristo”. (Efe. 5: 21). Huu ndio wajibu wa msingi kwani unatutambulisha
na kutushirikisha maisha yetu na Kristo.
Baada ya kueleza wajibu huo
wa msingi, mwandishi wa barua hiyo anafafanua wajibu wa mume, mke na watoto.
Kimsingi wajibu zote zinaegemea tunu za upendo, utii na heshima.
Familia zinazojengeka katika
misingi hiyo ndizo zinazodumu na kuwa imara. Wanafamilia katika familia za
namna hiyo hukubaliana, huchukuana, hujengana, kila mmoja kwa manufaa ya
mwenzake na kwa manufaa ya pamoja.
Wajibu wa familia
kwa jamii unaelezwa vizuri kwa kutambua uhusiano asilia uliopo kati ya familia
ambayo sehemu, na ndiyo inayouunda jamii kwa upande mmoja, na jamii ambayo
hundwa na mkusanyiko wa familia moja moja kwa upande mwingine. Kwa hiyo bila
familia hakuna jamii. Kwa upande mwingine familia inahitaji jamii kwa ajili ya
ustawi wake.
Raia anaweza kumfungulia rais kesi ya madai
Na Dotto Shashi
SHERIA inaruhusu mtu yeyote ambaye ana
madai dhidi ya Rais wa nchi kufungua kesi ya madai hayo, ili aweze kupatiwa
haki yake.
Ni
wazi kuwa mtu anaweza kujiuliza je, inawezekana vipi kwa raia kumfungulia kesi
ya madai Rais wake?
Jibu
la swali hili limewekwa wazi katika Katiba
ya Jamhuri ya Muungano ya Tanzania ya mwaka 1977 kama ilivyofanyiwa
marekebisho mbalimbali.
Kifungu
cha 46 Ibara Ndogo ya Pili (2)
ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano ya Tanzania, kinaeleza kuhusu ufunguaji wa
kesi ya madai dhidi ya Rais kwa jambo lolote alilofanya katika uwezo wake kama
raia wa kawaida yaani, “Institution of Civil Case in respect as an
ordinary citizen.”
Katiba kinaelekeza suala zima la ruhusa ya
kumshitaki Rais kwa kosa la madai, yaani “a civil wrong,” .
Katika
sheria juu ya shughuli au mambo ya Rais, yaani, “Presidential Affairs
Act, CAP9.” Taratibu zimewekwa kuhusu suala zima la kufungua kesi ya
madai dhidi ya Rais wa nchi.
Mahakama
ambayo inaruhusu kupokea mashitaka hayo ya madai, katika, Kifungu cha Tano
(5) cha sheria hiyo kinaeleza kuwa hakuna kesi yoyote ya madai
inayofunguliwa dhidi ya Rais itaruhusiwa katika mahakama yoyote isipokuwa
mahakama kuu pekee yaani, “No Civil Proceedings which may be instituted
against the President shall be instituted in any court other than the High
Court.”
Hivyo
endapo una madai dhidi ya Rais wako, basi mahakama inayotakiwa kufungua madai
hayo ni Mahakama Kuu pekee.
Kifungu
cha Sita (6), Kifungu Kidogo cha kwanza (1) cha sheria ya shughuli
au mambo yanayomhusu Rais (Presidential Affairs Act), kinasema,
mtu yeyote ambaye anakusudia kufungua kesi ya madai dhidi ya Rais ni lazima
atoe notisi ya siku Thelathini (30) kwanza kabla ya kufungua kesi hiyo.
Hii
ni kwa mujibu wa Kifungu cha 46 Ibara ya (2) cha Katiba ya Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania.
Katika
Kifungu Kidogo cha Kwanza (1) (9) cha Kifungu cha Sita (6),inaelezwa
kuwa, notisi ya mashitaka ya madai dhidi ya Rais ni lazima iambatane na Hati ya
madai. Yaani “Plaint”
(b)
Notisi na hati hiyo ya madai itatumwa kwa Katibu Mkuu Kiongozi au kwa Katibu wa
Kudumu au binafsi wa Rais au Notisi na Hati hiyo itatumwa kwa Rejesta
iliyolipiwa kabla, kwa Katibu Mkuu Kiongozi Ikulu kupitia njia ya posta.
Kifungu
Kidogo cha Pili (2) kinaeleza kuwa, endapo mahakama itaridhika kuwa kesi
dhidi ya Rais imefunguliwa na kwamba mdai, yaani “Plaintiff” ana
haki dhidi ya Rais, Mahakama hiyo haitatoa hukumu au agizo dhidi ya Rais
isipokuwa kwa kuarifu kwa njia ya maelezo ya kisheria kuwa kuna madai dhidi ya
Rais yaliyothabiti, yaani “By way of declaratory order.”
Lengo
la utaratibu huu ni kumfahamisha Rais, ili aweze kukidhi matakwa hayo na wala
si kumwamrisha, kama inavyokuwa kwa watu wengine wanapofunguliwa kesi za madai.
Kwa
upande wa amri ya kukamatwa (arrest), Kifungu cha Nane (8), Kifungu
Kidogo cha Kwanza (1) kinaeleza kuwa, Rais ana kinga dhidi ya kukamatwa yaani, “The
President shall be immune from arrest.”
Kifungu
Kidogo cha Pili kinasema hakuna amri yoyote itakayo tolewa kwa Rais na mahakama
yoyote au mtu au mamlaka yenye uwezo wa kutoa amri ya;-
(a).
Kumtaka Rais au kumlazimisha kufika mahakamani iwe kwa uwezo wake kama Rais au
hata katika uwezo wa kawaida.
(b).
Kumtaka au kumlazimisha Rais kumleta mtu au kutoa kitu chochote mahakamani.
Kifungu
Kidogo cha Tatu (3) kinasema
endapo upande katika kesi unaomba ruhusa ya kuitwa mahakamani kwa Rais
kama shahidi katika kesi hiyo au kumtaka Rais amlete mtu au kitu chochote
mahakamani hapo, mahakama itatakiwa kumfahamisha Rais juu ya maombi hayo,
lakini mahakama hiyo haitatoa amri nyingine au kutoa wito juu ya maombi hayo.
Kifungu
cha Tisa (9) kifungu kidogo cha kwanza kinasema kuwa, hati ya kuitwa
shaurini (Summous) ni marufuku kupelekwa Ikulu, au nyumba za
kupumzikia wageni au katika viwanja vya Ikulu au katika makazi mengine yoyote
maalumu ya Rais, isipokuwa mpaka yatolewe maelekezo kutoka kwa Katibu Mkuu
Kiongozi juu ya utekelezaji wa utaratibu huo wa ki-mahakama.
Katika
kifungu cha Saba (7) Kifungu Kidogo cha Kwanza (1) kuhusu
utaratibu wa kisheria dhidi ya Rais anaposhitakiwa, sheria inasema taratibu nyingine zote zielekezwe kwa Mwanasheria
Mkuu yaani, “The Attorney General,” isipokuwa kwa zile zilizoelekezwa katika Kifungu cha 46 cha
Katiba Ibara ya Pili (2) kama tulivyoona hapo awali.
Sakramenti
ya Mpako wa Wagonjwa(2)
Wanaokwenda vitani wanaweza kupewa Sakramenti ya
Mpako?
KATIKA toleo lililopita,
tuliishia katika kipengele kinachoelekeza namna ya kumpaka mafuta mgonjwa
wakati wa kutoa Sakramenti ya Mpako wa Wagonjwa. Katika toleo hili, tutaanza
kuangalia wajibu kwa wagonjwa na kisha, tutaona kama askari wanaokwenda vitani
au watu wanaokwenda kunyongwa wanaruhusiwa kupewa SAKRAMENTI
YA MPAKO WA WAGONJWA. Endelea.
Wajibu kwa wagonjwa: kan. 1001
Wenye
wajibu wa kuhakikisha kuwa wagonjwa wanapata Sakramenti ya Mpako wa Wagonjwa
katika muda unaofaa ‘tempore opportuno’ ni wale walio karibu na
wagonjwa. Hao, ni pamoja na jamaa, marafiki, madaktari na wauguzi.
Wengine ni wachungaji wa kiroho
kutokana na kazi yao ‘ex officio’. Wengine ni wagonjwa wenyewe
ingawa kanuni hii haiwataji.
Lakini, ni wazi kwamba iwapo
wenye wajibu huo wamepuuzia, wagonjwa wenyewe hawana budi kujishughulikia kwa
kuomba sakramenti hiyo (RAnointing 13: DOL 3333).
Kanuni hii inashauri kuwa,
wagonjwa wapokee Sakramenti ya Mpako wa Wagonjwa katika ‘muda unaofaa’, yaani,
‘tempore opportuno’.
Je, maana yake ni nini? Mtaguso
II wa Vatikano unasema kuwa, mara tu muumini atakapoanza kuwa hatarini kwa
sababu ya ugonjwa au uzee, ni muda unaofaa kupokea Sakramenti ya Mpako wa
Wagonjwa (SC 73).
Kwa hiyo, ‘muda unaofaa’ ni
pale ambapo hali ya mgonjwa au mzee inaanza kuwa mbaya. Ni juu ya mhudumu wa
wagonjwa au mzee au mgonjwa mwenyewe kwa kutumia busara kuona kwamba, hali
imeanza kuwa mbaya na kumwita mhudumu wa Sakramenti ya Mpako wa Wagonjwa.
Mpako wa watu wengi: kan. 1002
Ingawa mara nyingi mpako
unafanyika kwa mtu mmoja, pengine unaweza kufanyika kwa watu wengi, kama vile:
wakati wa mahujaji, mkusanyiko wa wagonjwa wa jimbo au wa mji au wa parokia au
wa jumuiya fulani au hospitalini (RAnointing 83-85).
Mfano mzuri ni adhimisho la
sakramenti hiyo wakati wa mahujaji ya Lurdi ya mwaka 1969 ambapo Ibada ya namna
hiyo iliruhusiwa (N6 (1970)13-33; CLD 7,687).
Kanuni ya 1002 inaeleza kuhusu
hali ambapo watu wengi wanaweza kupakwa katika Ibada moja. Lakini, askofu wa
jimbo hana budi kusimamia au kutoa mwongozo kuhusu adhimisho ambapo wagonjwa
kutoka maparokiani au hospitalini au sehemu nyingine wanavyoweza kupokea
sakramenti hiyo kwa pamoja (RAnointing 17: DOL 3337).
Huu ni wajibu wa Askofu kwa
jimbo tu kwa sababu ndiye mwenyekiti na
mratibu wa shughuli zote za kiliturjia jimboni (kan. 835).
MHUDUMU WA SAKRAMENTI: Kan. 1003
Ingawa ni kanuni moja tu
inayoeleza kuhusu mhudumu wa sakramenti hii, kanuni hii inatoa mwongozo muhimu
kwa wahudumu wa Kanisa. Kadiri ya kanuni hii, ni padrI tu anayeweza kuadhimisha
sakramenti kihalali.
Ikisisitiza utaratibu huu,
kanuni inasema:”……Unctionem Infirmorum valide administrat……..Solus
sacerdos”. Neno “sacerdos” linamaanisha askofu au padrI.
Utaratibu wa kuwa na padrI kama
mhudumu wa sakramenti hii umekuwa msimamo wa Kanisa kwa muda mrefu (Conc.
Tridentino, Sess. XIV,25 Nov. 1551, cap. 3 et can. 4:DZ 1697 et 1719).
Kanisa linafuata mwongozo wa
Mtume Yakobo aliyesema, “Mtu wa kwenu amekuwa hawezi? Na awaite wazee wa
Kanisa; nao wamwombee, na kumpaka mafuta kwa jina la Bwana,” (Yak 5:14).
Mtaguso wa Trenti ulitishia kumtenga mtu yeyote atakayefundisha kinyume na
mafundisho hayo.
Mapadri au maaskofu wenye haki
na wajibu wa kuadhimisha sakramenti hii ni wale wenye ofisi za kichungaji
katika jumuiya za waamini, kama vile, askofu katika jimbo lake, paroko na
paroko msaidizi katika parokia yao na chapleni katika jumuiya ya waamini aliyokabidhiwa.
Chapleni anakabidhiwa hospitali
au jumuiya ya watawa au jeshi au wakimbizi au mabaharia au shule. Mapadri
wengine ni pamoja na gombera wa seminari (Kan. 262) na mkubwa wa shirika
la kiklero la watawa.
Kwa hiyo, haki na wajibu huo
hauwahusu mapadri na maaskofu wasiokuwa na ofisi za kichungaji katika jumuiya
za waamini.
Lakini, padri yeyote au askofu
anaweza kuhudumia mgonjwa kwa sababu kubwa na kwa idhini iliyodhaniwa, yaani ‘de
consensu…… praesumpto’, kutoka kwa mhudumu halali. Sababu kubwa ni,
kama vile, hatari ya kifo.
Anaombwa, kuwa baada ya
kuadhimisha sakramenti hiyo, kutoa taarifa kwa mhudumu halali au wa kawaida,
yaani mhudumu mwenye haki na wajibu ‘ex officio’.
Adhimisho la pamoja
linaruhusiwa, yaani, mapadri wawili au zaidi kushiriki katika ibada moja.
Mmoja kati yao anaweza kusoma
sala na kupaka mafuta wakati wengine wakishiriki sehemu nyingine, kama vile,
ibada ya utangulizi, masomo, sala ya maombi na kuweka mikono juu ya mgonjwa (Ordo,
19; RAnointing 17-19; DOL 3337-3339).
Washiriki wote hawawezi
kushiriki katika kupaka mafuta kwa sababu sehemu za kupaka mafuta zimepunguzwa
sana (kan. 1000). Baadhi yao au wote wanaweza kushiriki katika kupaka
mafuta iwapo idadi ya wagonjwa ni kubwa.
Sala inayosomwa na
kuiongoza-ibada tu ni: “Kwa mpako huu mtakatifu na kwa pendo lake kuu, Bwana
akujaze/awajaze na nguvu ya Roho Mtakatifu”.
Baada ya jibu la “Amina”,
anaendelea kusema: “Akuondoe/awaondoe katika enzi ya dhambi, akuweke/awaweke
huru.
Kwa wema wake akupe/awape nafuu
katika mateso yako/yenu na kukujalia/kuwajalia neema”. Jibu ni: “Amina”.
Kuhusu utayari wa kuadhimisha
sakramenti hii, kila padri ameruhusiwa kusafiri na mafuta matakatifu. Lengo ni
kumwezesha kuadhimisha sakramenti hii wakati wowote wa ulazima (SC Rit,
Decr., ‘Pientissima mater ecclesia’, Mar. 4,1965;AAS 57(1965),409;DOL 3314;
SCC, general directory, ‘Peregrinans in terra’, Apr. 30,1969:AAS 61
(1969),3605; DOL 2616).
Chimbuko la mwongozo huu ni
hati ‘Pientissima Mater Ecclesia’ ya mwaka 1965 iliyotolewa na
Idara ya Kiti cha Kitume kuhusu Ibada.
Lakini, mwongozo huu umepoteza
uzito wake kutokana na ruhusa iliyotolewa na kanuni ya 999 inayomruhusu padri
yeyote kubariki mafuta ya mpako wakati wa adhimisho la Sakramenti ya Mpako wa
Wagonjwa. Ruhusa imetolewa wakati wa ulazima, kama vile, hatari ya kifo.
WAPOKEAJI WA SAKRAMENTI: Kan.
1004-1007.
Sehemu hii ya sheria ya kanisa
inazo kanuni 4. Kanuni ya 1004 inahusu adhimisho halali na marudio ya
sakramenti. Kanuni ya 1005-1006 zinahusu kesi za mashaka na dhana katika
adhimisho la sakramenti. Mwisho, kanuni ya 1007 inawataja wale wanaozuiliwa
kupokea sakramenti hii.
Adhimisho halali: Kan. 1004
Kuhusu uhalali wa adhimisho la
sakramenti, Sheria ya Kanisa imetaja masharti 5: ubatizo, umri wa mang’amuzi,
nia ya mpokeaji (kan. 1006), ugonjwa mbaya au uzee na hali ya kiroho.
Kutokana na uwazi wa baadhi ya
masharti hayo, nitajaribu kueleza baadhi tu ya masharti, kama vile, umri wa
mang’amuzi na ugonjwa au uzee.
Kwa kuwa lengo la kwanza la
adhimisho la sakramenti hii ni kuondoa dhambi na kukamilisha kitubio, kuongeza
neema au kurudisha neema iliyopotea kwa sababu dhambi, mpokeaji hana budi kuwa
na uwezo wa kutenda dhambi.
Kwa hiyo sakramenti hii
haitolewi kwa watoto wachanga au watu waliozaliwa punguani (kan.99) kwa sababu
hawana uwezo wa kutenda dhambi.
Hawajapoteza neema ya Mungu
walioipata wakati wa ubatizo (DZ,3536). Badala yake sakramenti hii
inatolewa kwa muumini aliyefikia umri wa mang’amuzi au zaidi.
Hata mtu mzima aliyebatizwa
wakati wa hatari ya kifo na ameelezwa maana na umuhimu wa sakramenti hii katika
maisha ya waumini, anaweza kupewa sakramenti hii.
Iwapo kuna mashaka kama muumini
amekwishafikia umri wa mang’amuzi apewe sakramenti hii kwa masharti, ‘sub
conditione’ (Kan. 1005).
Sharti la pili ni ugonjwa mbaya
au mkubwa au uzee. Ndiyo maana Mtume Yakobo anasema, “Mtu wa kwenu amekuwa
hawezi? Na awaite wazee wa kanisa; nao wamwombee, na kumpaka mafuta kwa jina la
Bwana”, (Yak. 5:14). Hayo, pia, ndiyo mafundisho na desturi ya kanisa (Dz,1698).
Kwa bahati mbaya, kanuni hii
haielezi kuhusu hali ya ugonjwa au uzee ambapo muumini anapaswa kupokea
sakramenti hii.
Inataja tu kuwa muumini apewe
sakramenti hii pale ambapo hali yake inaanza kuwa hatarini kwa sababu ya
ugonjwa au uzee, ….ob infirmitatem vel senium in periculo incipit
versari”.
Kwa hiyo, kanuni hii inatoa
nafasi kwa waamini (kan.1001) kutumia busara na hekima zao katika kuamua kuwa
afya ya muumini fulani imeanza kuwa hatarini.
Aidha, kanuni haitaji aina ya
ugonjwa, ndiyo maana, hata magonjwa ya akili yanahusishwa. Siku hizi magonjwa
ya akili yameanza kuwa tatizo na tishio kubwa kwa wanadamu.
Kwa hiyo, waamini wenye
magonjwa mabaya au makubwa ya akili wanahitaji kuimarishwa na Sakramenti ya
Mpako wa Wagonjwa (Pastoral Care, 27, n. 53).
Mgonjwa anaweza kupakwa kabla
ya kufanyiwa upasuaji hospitalini iwapo upasuaji unasababiswa na ugonjwa (Rituale
Romanum, Ordo, 10).
Lakini, siyo maaskari
wanaokwenda vitani au watu wakunyongwa kwa sababu hali hizo hazisababishwi na
magonjwa au uzee. Maaskari walio vitani wanaweza kupakwa iwapo wamepata
majeraha mabaya.
Kuhusu uzee, muumini mzee anaweza kupakwa iwapo ameanza kuwa
dhaifu ingawa uzee siyo ugonjwa (Rituale Romanum, Ordo unctionis
infirmorum eorumqe pastoralis curae, vaticanis, 1972, n. 11).
Itaendelea
Kwanini Injili ya Barnaba
haikuingizwa katika Biblia?
Padri Titus Amigu, Mkuu wa Seminari Kuu ya
Peramiho iliyopo katika Jimbo Kuu Katoliki la Songea, ambaye ni Mtaalamu wetu
wa Biblia, anajibu swali la mmoja wa wasomaji wetu linalosema: Nasikia kwamba
kulikuwa na Injili Barnaba. Je, hiyo ni kweli? Kama ilikuwepo, imekwenda wapi?
Jibu: Injili ya
Barnaba ipo lakini haikuingia katika Biblia, iliachwa tangu mwanzo. Ifahamike
kuwa, sio hiyo tu iliyoachwa, bali kuna Injili nyingine kama 22 juu yake
zilizoachwa. Hazikuingia na hazikupata ruhusa ya kuingia katika Biblia.
Watu wengine wengi pia,
hawana habari na Injili hizo. INJILI ZA APOCRIFA, ziliachwa na Kanisa katika
Karne ya 4 na mpaka sasa zipo na zimechapwa katika vitabu husika.
Maktaba kubwa zote ni sharti
ziwe na vitabu vya Apocrifa. Nami kwa bahati nzuri, ninazo huko niliko. Injili
zingine zilizoachwa na Kanisa ni hizi zifuatazo; Injili ya Batholomeo, Injili
ya Baslibosi, Injili ya Kuzaliwa Bikira Maria, Injili ya Waebioni, Injili ya
Wamisri, Injili ya Eva, Injili ya Gamalika, Injili ya Waebrania, Injili ya
Utoto wa Yesu na Injili ya Kiarabu ya Utoto wa Yesu.
Nyingine ni Injili ya
Kiarmenia ya Utoto wa Yesu, Injili ya Kiapocrifa ya Yohane, Injili ya Malkion,
Injili ya Maria, Injili ya Wanaseni, Injili ya Wanazareni, Injili ya Nekodemo,
Injili ya Petro, Injili ya Filipo, Injili ya Thomasi, Injili ya Mapokeo ya
Matia na Injili ya Ukweli.
Injili zote hizo zipo.
Ilitokeaje tukio hili, hiyondiyo kazi tunayofanya sasa hivi. Kumbuka ndugu
msomaji tukio la Yesu kuzaliwa kama binadamu na Mungu hapa duniani, lilikuwa
tukio kabambe sana. Tukio la ajabu sana. Tukio lililowatingisha wote. Wayahudi
na hata jirani zao Waarabu.
Basi, matokeo yake ikawa watu
wengi sana wakaamua kuandika habari hiyo. Hilo unasoma katika utangulizi wa Injili
ya Luka1:1-4 kwamba, Watu wengi sana wakati ule, waliandika habari za Yesu.
Na yeye Luka pia akaamua kuandika habari za Yesu; hizo hizo. Ila baada ya
kuzifanyia uchunguzi kamili.
Alichunguza huko na huko ili
andike habari kamilifu. Basi ndugu msomaji, kwa vile watu walikuwa wengi
walioamua kuandika, Injili zilikuwa nyingi sana kwa kadiri ya maweza ya
waandishi.
Wengine waliandika habari za
Yesu kwa mbwembwe na madoido na hata kutilia chumvi mambo mengi.
Ndipo wakubwa wa Kanisa letu
katika karne zile za mwanzo, walipoamua kuitengeneza Biblia katika kukusanya
mambo hayo rasmi yanayo muhusu Mungu, wakiongozwa na Roho Mtakatifu,
wakazichukua Injili nne tu, zilizomo kwenye Biblia yetu.
Kwa maana hizo zilikidhi
vigezo vifuatavyo bila shida; Kigezo cha kwanza kilikuwa ni muunganisho wa
maandiko yale, na kigezo cha pili kilikuwa kuwa na asili ya kitume, yaani
kuhusika kwa mitume katika kuziandika.
Kigezo cha tatu kukubalika
kwa maandishi yale na jumuiya za awali za Kikrito; na kigezo cha nne, kuwa na
hadhi ya kuchochea imani na mapendo. Kigezo cha jumla, kilikuwa ni Uongozi wa
Roho Mtakatifu mwenyewe.
Basi Injili zote za mbwembwe
na zile zilizojaa madoido mengi zilizokuwa haziwezi kuchochea imani wala
mapendo ya mtu yeyote, na wala hazikuwa na muunganiko wa mafundisho na wala
hazikukubaliana na jumuiya ya awali za Kikrito, hizo ziliachwa kwa maana
zilikuwa wazi kwamba, hazikuandikwa kwa msaada wa Roho Mtakatifu.
Si Injili tu zilizoachwa kwa
sababu hizo, bali vipo pia vitabu vingi vingine vya Apokrifa kama vile vitabu
vya Matendo ya Andrea, Matendo ya Yohane, Matendo ya Paulo, Matendo ya Thomasi,
Barua ya Lentulusi, Barua kwa Waledesia, Alexandria na Ufunuo wa Petro, Ufunuo
wa Paulo na Ufunuo wa Thomasi na vitabu vingi vingine.
Jambo hili la kuacha vitabu
kama hivyo na kutoviruhusu vitabu kuingia katika Biblia, lisiwe ni kikwazo.
Jambo hilo ni alama ya wazi ya kukomaa na alama ya wazi ya uadilifu wa imani
yetu ya Kikristo.
Hii ni imani makini yenye
lengo la kuwaokoa watu, na sio kuwaongopea na kuwapoteza, au kuwayumbisha.
Basi, vitabu vilivyo kwenye Biblia, ni SAFI na vyenye kuchochea na mapendo kati
ya watu.
Vimewekwa rasmi vimekubalika
na watu, vimetokana na Roho Mtakatifu. Havina mbwembwe, havina madoido, havina
chumvi, neno wala jambo la ziada.
Ninamalizia kwa kuonesha
uhalali wa kitendo hiki cha kuacha vitabu visivyowafaa watu safi kuingia katika
Biblia. Tuikumbuke tukio lile maarufu dhidi ya Idd Amin wa Ugada, tangu 1978,
mwishoni mwishoni kidogo hadi 1979.
Wakati wa vita au miaka ya
mbele kidogo, watu wengi sana waliamua kuandika juu ya vita, wengine waliandika
vitabu, wengine mashairi, wengine insha na hata wengine walifanya katuni na
kadhalika.
Kumbe maandishi yote hayo
yalitofautiana. Wengine walitia mbwembwe, wengine walitilia chumvi, wengine
waliongeza mambo ya kwao na hivyo basi, kutofautiana kukawa ni jambo la kweli.
Basi ikiwa sisi leo tunataka
kuchukua maandishi kwa ajili ya kufuindishia watoto wetu, historia halisi ya
Tanzania na matendo yake, ni lazima jopo la wanahistoria liyachambue maandishi
hayo.
Yaani wachukue vitabu au
maandishi yaliyo makini na si yale yanayotiliwa mbwembwe, madoido na chumvi
nyingi. Watu hao watayaacha yale mashairi yanayo mwita Idd Amin, NDULI, au JOKA
KUKU na PAKA SHUME. Mashairi na vitabu vya namna hiyo, havitavifaa vizazi vya
jamii vijavyo; ni lazima viwekwe kando.
Kufanya jivyo itakuwa ni ishara ya uadilifu wa taifa letu na
ukweli wa wanahistoria. Ndivyo basi ilivyotokea kwa Injili ya Barnaba. Injili hii
ipo na ukitaka unaweza kuiona na kuisoma.
Nenda kwenye maktaba kubwa na uliza vitabu vinavyoitwa
APOKRIFA za Agano Jipya kwa maana vipo pia vitabu vya Agano la Kale ambavyo ni
Apokrifa vilevile kama vile KUPALIZWA KWA MUSA
KITABU CHA ADAM NA EWA.
Ukiona utakubali kuwa kwa kweli, haikupasa kuchukuliwa na kufanywa kama kitabu cha makini maana mambo yake, hayakiri imani, wala hayachochei mapendo. Hata Wakristo wa mwanzo hawa kubali hayo mambo.
Haki za watoto zisihusishwe na siasa; zilindwe
Na Tiganya Vicent, MAELEZO.
PAMOJA
na jitihada za Serikali ya Tanzania, Shirika la Kazi Duniani (ILO) na wadau
wengine, kupambana na utumikishwaji watoto katika kazi za hatari, baadhi ya
wanasiasa wilayani Iramba, wamekuwa wanapotosha wananchi kwa kudai kuwa hizo ni
kampeni za baadhi ya viongozi wa vyama vya siasa, katika kuelekea uchaguzi Mkuu
hapo mwakani.
Hali hii imechangia kwa kiasi
kikubwa kudidimiza maendeleo ya kampeni ya mapambano dhidi ya tatizo hilo
linalowakabili watoto walio chini ya umri wa miaka 18.
Kwa mujibu wa maelezo ya
viongozi wa vikundi vya sanaa vinavyojihusisha na uhamasishaji wa mapambano
dhidi ya utumikishwaji watoto wilayani Iramba, wamekuwa wakikabiliana na
vikwazo kutoka kwa wanasiasa wanaodiriki kuwadanganya wananchi kwa kusema kuwa,
zoezi la kuwaondoa watoto katika utumikishwaji katika kazi hatari ni sehemu ya
kampeni za kisiasa za chama tawala.
Hali hiyo imekuwa ikichangia
kuwakatisha tamaa wasanii wanaojitolea kuelimisha jamii dhidi ya mapambano ya
tatizo hilo ambalo limeenea kwa kiasi kikubwa wilayani humo.
Mratibu wa Programu ya Muda
Maalum wa Kupambana na Ajira mbaya Wilayani Iramba, Bw. Hezron Msule, alisema
kuwa, watu hao ni sawa na wauaji, kwani hawana huruma hata kidogo kwa maelfu ya
watoto wilayani humo ambao wanapata mateso ya kutumikishwa katika ajira za
hatari.
Alisema kuwa, watu hao si wema
kwani wanapenda watoto hao waendelee kuwa watumwa wa wenzao wakati watoto wa
sehemu nyingine wanapatiwa haki za msingi kama elimu na muda wa kuendeleza
vipaji vyao.
Bw. Msule alisema kuwa,
kuendelea kuachia tatizo la utumikishwaji kwa watoto, ni sawa na kuendelea
kukubali madhara yanayotokana na tatizo hilo kama vile kupata maambukizo ya
janga la UKIMWI.
Ni vema wanasiasa hao
wakafahamu kuwa, watoto zaidi ya milioni nne nchini, wanatumikishwa katika kazi
za hatari zikiwamo biashara ya mapenzi, kazi za nyumbani, mashamba na katika
migodi.
Watoto hao wote wako katika
hatari ya kuathirika na kudumaza vipaji vyao kwa kukosa elimu na hivyo,
kurudisha nyuma maendeleo ya Taifa.
Aidha, watoto wengi walioko
katika kazi za hatari, hufanyishwa kazi ambazo hazilingani na umri wao na
kukosa muda wa kupumzika, kucheza, kukosa mapenzi ya wazazi au walezi na mara
nyingine, unyanyaswaji wawapo kazini.
Mara nyingi watoto
wanaotumikishwa, wamekuwa wakipata madhara mbalimbali kama vile kupata mimba
katika umri mdogo ambazo huwasababishia matatizo wakati wa kujifungua, kupatwa
na magonjwa ya zinaa ikiwemo UKIMWI, kutumia dawa za kulevya, kukua katika hali
isiyo ya maadili, kuathirika kisaikolojia na kukosa heshima katika jamii.
Kufuatia hatari hiyo
inayowakabili watoto wanaotumikishwa nchini, Serikali ya Tanzania chini ya
Chama Tawala cha Mapinduzi, iliamua kuridhia mikataba mbalimbali duniani ya
kupambana na ukatili dhidi ya watoto na siyo siasa kama baadhi ya wanasiasa hao
wa Iramba wanavyodai.
Ni vema wanasiasa hao pia
wakaelezwa na kuelewa kuwa, Tanzania ni mwanachama wa Shirika la Kazi Duniani
(ILO) na imeridhia mikataba miwili ya ILO.
Mikataba hiyo ni pamoja na ule
wa Namba138 unaomtaja mtu mtoto kuwa ni yule mwenye umri chini ya miaka 18 na
Mkataba Namba 182, unaofafanua kuwa, mtoto wa umri huo hapaswi kuajiriwa katika
kazi ngumu na hatari.
Kufuatia utafiti uliofanywa na
Serikali ya Tanzania kwa kushirikiana na ILO, Wilaya ya Iramba ni miongoni mwa
wilaya zenye matatizo makubwa ya usafirishaji na utumikishwaji watoto katika
biashara ya mapenzi na kazi za ndani.
Katika kutambua ukubwa wa
tatizo hilo, Serikali ya Tanzania kwa msaada wa Shirika la kazi Duniani imekuwa
ikitumia mikakati mbalimbali kuwaelimisha wanajamii kuunga mkono mapambano
dhidi ya biashara zote zinazohusu utumikishwaji watoto.
Mikakati hiyo ni pamoja na
uundaji wa vikundi vya hamasa ambavyo vina jukumu la kutumia sanaa kuelimisha
jamii madhara ya utumikishwaji watoto na faida za kuwaondoa katika utumwa huo.
Vikundi hivyo vilivyoanzishwa
na Idara ya Habari Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kushirikiana na Chama cha Waandishi
wa Habari Wanawake (TAMWA), vimeshafanya kazi kubwa ya kuhamasisha jamii katika
wilaya 11 ambapo kwa wastani, kila wilaya ina vikundi 14.
Vikundi hivi vimekuwa
vinatumia kazi mbalimbali za sanaa kuelimisha jamii madhara ya mtoto
kufanyishwa kazi ambazo ni nzito ikilinganishwa na umri wake.
Matokeo ya kazi za sanaa
yameanza kuonekana ambapo baadhi ya wazazi wameapa kutowaruhusu watoto wao
kuondoka nyumbani kwao kwenda mijini kufanya kazi wanapomaliza elimu ya msingi.
Siyo hivyo tu, Serikali pia
inatumia waandishi wa habari kuielimisha jamii na kuhabarisha jamii. Kwa hiyo,
kiongozi yeyote anayesimama bila aibu na kusema kuwa vikundi vinatumika katika
jamii kuelimisha juu ya mapambano dhidi ya utumikishwaji huo vipo kwa lengo la
kupiga kampeini, ni hatari na vinastahili kuogopwa kama ukoma.
Kiongozi kama huyo ni wazi
kuwa atakuwa hafai mbele ya jamii ya Watanzania. Kwani tayari anaonesha udhaifu
wake wa kiutendaji na hana utu kwa binadamu wenzake, kwa kuwa anaonesha
kufurahia utumwa wanaofanyiwa watoto hao katika nchi yao na wengine, waendelee
kupata magonjwa mbalimbali kwa tatizo la wajinga wachache.
Mkakati mwingine ambao
Serikali imeshachukua ni pamoja na kutunga sheria inayowabana waajiri wa
watoto, ambao Rais Benjamin William Mkapa hivi karibuni alitia saini sheria
hiyo.
Sheria hiyo imekusudia
kukomesha vitendo vyote vya kuwashurutisha watoto kufanya kazi ngumu na za
hatari kwao. Hatua nyingine, ni pamoja na kuunda kamati za vijiji za kupambana
na tatizo hilo.
Tanzania ni miongoni mwa nchi
tatu duniani, zinazotekeleza programu ya muda maalum ya kuwaondoa watoto katika
utumikishwaji wa kazi za hatari, nchi nyingine ni Nepal na ELSalvador.
Programu hiyo inafadhiliwa na
Serikali ya Marekani kupitia Shirika la Kazi Duniani (ILO) ambapo kwa upande
wake, Serikali ya Tanzania inakusudia kwamba hadi kufikia mwaka 2010, watoto
wote wawe wameondolewa katika utumikishwaji nchini.
Programu hiyo ni moja ya
shughuli za serikali zisizohusika na siasa bali zenye lengo la kuokoa maisha ya
watoto. Hivyo, ni vema wanasiasa wakaacha kuchanganya siasa na shughuli za
maendeleo ya jamii, kwani wanawapotosha wapiga kura wao katika mambo ambayo
yana manufaa sio kwa watoto, bali kwa Watanzania wote.
Watoto hao walioko katika
utumikishwaji ndio hao wanaotarajiwa kuwa wanachama wa siku za baadaye na
viongozi wa vyama hivyo. Hivyo, siyo vizuri kuwaacha waangamie kwa utashi wa
watu wanaojifunza siasa.
Ni vema pia wakasema ukweli
juu ya mazuri yanayoridhiwa na serikali kwa manufaa ya nchi na wanachama wake.
Upinzani sio ubishi wa kupinga kila kitu, bali ni ukosoaji unaolenga kujenga na
sio kubomoa.
Ni ukweli usiofichika kuwa,
vita dhidi ya utumikishwaji watoto ni miongoni mwa juhudi nzuri zinazofanywa na
Serikali ya Awamu ya Tatu. Lakini, ni vema wanasiasa wanaoubeza mpango huo
wakaelewa kuwa watoto hao wanaotumikishwa si wanachama wa CCM.
Vita dhidi ya utumikishwaji
isichanganywe na siasa. Ni vema wanasiasa hao wakaviacha vikundi hivyo vya
sanaa vifanye kazi waliyotumwa na jamii ili watoto waje kufurahia maisha yao
hapo baadaye.
Ni vema viongozi hao wa vyama
vya siasa wilayani Iramba, wakaelewa kuwa ziko wilaya nyingine kama vile Ilala,
Kinondoni, Temeke, Kondoa, Urambo, Arusha, Simanjiro,Arumeru, Mufindi na Iringa
Vijijini, ambapo wananchi wa huko wameshaliona tatizo linalowakabili watoto, ni
la jamii na wala siyo la chama fulani, na hivyo wameungana katika mapambano
hayo.
COLLETA; Shule ya msingi iliyozingatia
elimu kwa wote
l
KAPTENI KOMBA: Marehemu alituusia kuwajali yatima
Na Lilian Nyenza.
MATOKEO ya mtihani wa darasa la saba yaliyotangazwa
Desemba 2004, yameifanya shule binafsi ya msingi ya Kumbukumbu ya Colleta ya
jijini Dar es Salaam, kuingia katika kitabu cha maajabu baada ya wanafunzi wake
wote kufaulu kuingia sekondari isipokuwa mmoja tu.
Shule
hiyo, pamoja na ile ya sekondari ya Bakili Muluzi inayomilikiwa na msanii
maarufu na mwanasiasa wa siku nyingi, Kapteni Mstaafu John Komba, imeshika
nafasi ya sita kwa Wilaya ya Kinondoni na 11 kwa mkoa wa Dar es Salaam katika
matokeo hayo.
Wanafunzi
hao waliofaulu ni wa kwanza tangu kufunguliwa kwa shule hiyo, iliyoko Mbweni,
nje kidogo ya jiji la Dar es Salaam na ni mara ya kwanza pia kuwa na wanafunzi
wa darasa la saba.
Matokeo
hayo ndiyo yamewafanya wazazi na wananchi kujiuliza kuwa, chanzo kikubwa cha
mafanikio ya haraka ya shule hiyo ni nini.
Shule
ya Kumbukumbu ya Colleta inamilikiwa na Kapteni Komba kupitia taasisi ya Educate
Girls ambayo pia inamiliki shule ya awali na Sekondari iliyoanzishwa
rasmi mwaka 1997 na kuzinduliwa rasmi hivi karibuni na Waziri Mkuu wa Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania, Bw. Frederick Sumaye.
Lengo
kuu lilikuwa kuwaelimisha watoto wa kike ambao hapo nyuma, waliwekwa pembezoni
katika usawa wa elimu.
Mkurugenzi
huyo anasema, msukumo wa kuanzisha shule hizo ulitokana na wosia wa Marehemu
Mama Colleta ambaye alikuwa mama mkwe wake ambaye kabla hajafa, aliwaagiza
kuwatunza na kuwasaidia watoto yatima.
“Wakati
wa uhai wake Mama Colleta aliwapenda sana watoto hasa waliokuwa wakiishi katika
mazingira magumu akiwahudumia kwa hali na mali, hali iliyosababisha kutuachia
wosia kwamba, tuendelee kuwatunzwa na kuwapenda watoto yatima,” alisema Kapteni
Komba na kuongeza kuwa, mama huyo alifariki dunia mwaka1995.
Aidha,
Mkurugenzi huyo alisema mbali na wosia wa mama huyo, alipata nguvu baada ya
kupewa wazo la kuanzisha shule hizo na aliyekuwa Rais wa Malawi Dk. Bakili
Muluzi ambaye pia alitoa msaada wa hali na mali katika ujenzi wa shule hizo.
“
Ametoa karibu theluthi mbili ya gharama za ujenzi wa shule hizi,” anasema
Kapteni Komba.
Kutokana
na changamoto hizo, taasisi hiyo ilijiwekea malengo makubwa manne ambayo
yalikuwa ni kuanzisha shule ya chekechea, msingi, sekondari na chuo cha ualimu.
“Matatu kati ya hayo tumeweza kuyatimiza
katika miaka saba ya uhai. Tumefanikiwa kuanzisha shule za chekechea, shule ya
msingi pamoja na sekondari. Mipango ipo njiani ili kuhakikisha tunaanzisha chuo
cha ualimu,” anasema.
Anasema
ujenzi wa shule ya msingi umekamilika na tayari mwaka huu umeanza kutoa zao la
kwanza la darasa la saba, wakati ujenzi wa shule ya sekondari iliyopewa jina la
Bakili Muluzi kwa heshima ya Rais wa zamani wa Malawi, ikiwa imefanikiwa kupata
wanafunzi wa kidato cha pili.
Kwa
sasa, shule hizo zina jumla ya wanafunzi 23 wa chekechea, shule ya msingi
wanafunzi 91na shule ya sekondari
wanafunzi 50,” Kati ya wanafunzi hao, tunao wale ambao ni yatima na
wamefiwa wazazi wao kutokana na ugonjwa wa UKIMWI.
Kwa
mujibu wa Kapteni Komba, idadi ya wanafunzi hao yatima ni 30, kati yao 20
wakiwa wasichana. “ Tunawapatia watoto hawa huduma zote kuanzia ada, chakula,
usafiri pamoja na vifaa vya shule pasipo malipo yoyote,” anasema.
Pamoja
na kujengwa nje kidogo na mji na wanakotoka watoto wengi wanaosoma katika shule
hiyo, uongozi umetafuta usafiri ambao huwachukuwa na kuwarudisha wanafunzi kutoka
nyumbani kila siku za masomo, wakati mipango ikifanywa ili shule hizo ziwe za
bweni.
Ili
kutimiza haja hiyo, ujenzi wa hosteli umeanza ambapo benki ya CRDB imeahidi
kuwapa mkopo ili ifikapo Aprili, 2005 huduma ya kuwalaza wanafunzi shuleni hapo
iweze kuanza.
Uongozi
wa shule hizo una mpango wa kujenga zahanati itakayotoa huduma za afya kwa
wanafunzi, baada ya kuahidiwa na Kanisa Katoliki Jimboni Dar es Salaam msaada
wa wafanyakazi wa afya wakiwemo masista.
Hata
hivyo, Kapteni Komba alisema pamoja na mafanikio hayo, shule inakabiliwa na
matatizo kadhaa yakiwemo kukosekana kwa hali ya usalama ambapo watu wanaohisiwa
kuwa majambazi, wamewahi kuvunja na kuiba vifaa kadhaa vya shule vikiwemo
televisheni tatu na kompyuta tano.
Kutokana
na tatizo hilo, uongozi wa shule hiyo umeiomba Serikali kuwaruhusu kujenga kituo kidogo cha polisi
kwa gharama za shule na iwapatie askari wa kulinda usalama wa eneo hilo kwa
nyakati zote. Aliwaomba wafadhili kuisaidia shule kujenga uzio {ukuta}
kuzunguka shule zao.
Shule
hizo bado zinakabiliwa na uhaba wa chakula, vitabu, viwanja vya michezo na
vifaa vyake na kuomba wafadhili wajitokeze na kuwasaidia kutatua tatizo hilo.
“Tatizo
sugu ni maji ambayo hatuyapati na tunaiomba Serikali iliangalie tatizo hilo,”
alisema.
Katika
uzinduzi huo, Waziri Mkuu Fredrick Sumaye alikubali ombi la kuwa mlezi wa shule
hizo na kuongeza kwamba, yeye kama mkereketwa mkuu wa elimu haoni sababu za
kusita kuwa mlezi.
Bw. Sumaye aliahidi kufuatilia
kwa karibu matatizo ambayo yanakikabili kituo na kuyapatia ufumbuzi wa haraka.