Askofu
aichachamalia Serikali
l Wawekezaji wanawanyanyapaa
raia
l Dola inakejeli
Katiba;Utawala wa sheria ‘umekufa’
Na Josephine Nsolo
UVUNJAJI wa Sheria unaofanywa na
baadhi ya watu dhidi ya raia wengine, ni kinyume na madai ya Serikali kuwa
Tanzania inafuata misingi ya utawala
bora na sheria; amesema ASkofu Agustino Shao wa Kanisa Katoliki Jimbo la
Zanzibar. Aidha, Mhashamu Shao, ameijia
juu Serikali akidai vurugu katika chaguzi, unyanyasaji wa wawekezaji dhidi ya
raia na uharibifu wa mimba ni matunda inayovuna Tanzania kwa kutowajibika
viongozi wake.
Kwa mujibu wa taarifa iliyolifikia
KIONGOZI, Mhashamu Shao aliyasema hayo katika maadhimisho ya Sikukuu ya
Krismasi yaliyofanyika kitaifa Jimboni Zanzibar.
Alisema katika kipindi hiki sherehe hizo zimesongwa na
wasiwasi kwani furaha iliyopo nchini na duniani kote ni tofauti na
iliyotarajiwa kwa kuwa imesongwa na hofu ya vurugu na ukosefu wa amani.
Askofu Shao alisema kwa kuwa uhai ni zawadi kutoka kwa Mungu,
kila mmoja anawajibika kuulinda, kuuheshimu na kuuenzi ,“….Je, ni kwa namna
gani tunauenzi na kuutunza Uhai ? Kitendo cha vyombo vya dola kusajili vituo
vya kuharibu na kuondoa uhai kwa kisingizio cha UZAZI WA MAJIRA ,ni kinyume cha
sherehe za leo,” alisema.
Akaongeza, “Nchini mwetu leo kuna utitiri wa vituo vya uzazi
wa majira na shughuli kubwa za vituo hivi ni kuharibu Uhai. Sera ni kwamba,
kadiri wanavyoweza kutoa dawa nyingi za kuharibu mimba au kusitisha mimba,
ndivyo wanavyojipongeza na kuzawadiwa na wale walio watuma”.
Kiongozi huyo wa Kanisa Katoliki alisema kuwa, kitendo cha
Serikali kufumbia macho vitendo hivi ni kutowajibika na kufanya Katiba ya Nchi
inayolinda uhai wa raia, kuwa kejeli.
“Enyi viongozi wetu, si kila linalofaa pale China, Amerika au
Ulaya, linafaa pia Tanzania… Jueni kwamba, mamlaka yoyote ina uwezo wa kugeuza
mabaya kuwa mazuri, lakini hamna ruhusa yakuyafanya mazuri kuwa mabaya,”
alisisitiza ubaya wa vitendo hivyo vya ukatili dhidi ya Uhai.
Aidha, Askofu Shao alisema inasikitisha kuona hivi sasa
kipimo cha haki za raia si uraia wa mtu na ubinadamu wake, bali chama cha
siasa, dini, kabila na uwezo wake kiuchumi hali aliyosema, ni hatari.
“Hata kitendo cha wana usalama kuingilia mahakama ni ashirio
wazi la kutokuwa na utawala wa sheria,” alisema na kuongeza kuwa, mfano mzuri
ni waamini Wakristo wa Kiuyo Pemba walionyimwa na vyombo vya dola, haki ya
kusali katika kanisa lao baada ya Mahakama ya Mwanzo kuamua kinyume.
“Je, huo ndio utawala bora wa sheria? Ni zaidi ya miezi kumi
sasa tangu ajali ya gari la skuli ya Tomondo kugongwa, hakuna kesi kwani aliye
sababisha ajali hiyo ni mzito kiuchumi. Mnyonge akimbilie wapi? Na hali kama
hii itaendelea hata lini?” Alihoji na kusisitiza kuwa, ni wajihu wa kila
Mtanzania kulinda haki za wote wakiwamo wanyonge.
Akaongeza, “Mboni ya utawala wa sheria ni HAKI kwa wote na
uwajibikaji wa vyombo vilivyopewa jukumu la kutekeleza hayo. Kutowajibika kwa
vyombo dola athari zake ni kubwa na za hatari.”
Mintarafu matukio ya vifo yaliyotokea katika zoezi la
Uchaguzi wa Serikali za Mitaa Tanzania Bara na uandikishaji wa wapiga kura
katika Daftari la Kudumu huko Kusini Pemba, ni matunda ya kutowajibika kwa
waliokabidhiwa jukumu hilo.
“Kitendo cha kuwaweka raia katika vituo vya kupiga kura kwa
muda kwa sababu za uzembe au ubinafsi, ni kinyume cha utawala wa sheria na
demokrasia hivyo, Kanisa lina laani kwa hali zote, umwagaji damu uliotokea huko
Pemba na Dar es Salaam na linaagiza wahusika wawajibishwe kisheria,” alisema.
Alionya dhidi ya propaganda za kuwagawanya Watanzania kwa
nadharia za Uzanzibari na Uzanzibara na kusema
kuwa, vitendo vya kutishia raia juu ya haki ya kujiandikisha kupiga kura ni
kinyume cha Katiba ya Muungano hivyo, wahusika wawajibishwe.
Aidha, Kiongozi huyo wa kiroho alitahadhalisha kuwa hadi sasa
bado nia ya mataifa
makubwa kuzitawala nchi masikini inatekelezwa kwa kasi chini
ya mwavuli wa UTANDAWAZI na
UBINAFSISHAJI unaolenga kumiliki njia kuu za uchumi wa nchi.
“Je, nani asiyejua nguvu ya utawala ni uchumi wenye nguvu?…Si
kweli kwamba wawekezaji nchini hawafahamu umuhimu wa haki ya kila kuishi kwa
jasho lake. Lakini, ni nani anayewahalalishia kwamba mwekezaji ana mahitaji
zaidi ya mwenyeji anayemwezesha?” alisema.
Akaongeza, “Mishahara, marupurupu na faida wanayopata
wawekezaji ikilinganishwa na wasomi na wahudumu Watanzania, ni kielelezo wazi
cha ukoloni mambo leo na muundo endelevu wa matabaka ya watu…..Ili ulimwengu
utambue kuwa Mungu tunayemsherehekea leo ni wa wote, vyombo husika vidhibiti
unyanyapaa wa raia wanaofanyiwa na wawekezaji,” alisema.
Vyama ‘vyaishitaki’ Serikali kwa viongozi wa dini
l ‘Mashabiki wanaviponza vyama; hawaongozeki
kama wanachama’
Na Joachim Mushi
VYAMA vya siasa “vimeishitaki”
Serikali kwa viongozi wa dini, vikidai kuwa, ndiyo inayosababisha vurugu za
kisiasa zinazotokea wakati wa chaguzi kwa kuwa inafanya mambo kinyume na
makubaliano.
Katika Mkutano wa Juhudi za
Kuimarisha Amani Nchini, kwa mkoa wa Dar es Salaam (Wilaya ya Ilala/Kinondoni)
ulioandaliwa na kufanyika katika Hoteli ya Travertine jijini Dar es Salaam
mwanzoni mwa juma, viongozi hao wa vyama vya siasa walisema, Serikali ni chanzo
cha uvunjaji wa amani kwa kukiuka taratibu mbalimbali ikiwa ni pamoja na
kutumia dola kwa manufaa ya chama kimoja cha siasa (CCM).
Juhudi za Viongozi wa Dini Kuimarisha Amani nchini ni mpango
unaoendeshwa kwa pamoja na viongozi wa
dini kutoka Baraza Kuu la Waislam Tanzania (BAKWATA), Jumuiya ya Kikristo
Tanzani (CCT) na Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC).
Juhudi hizi zilizoanza mwaka 2003, zinayo ofisi ya kitaifa na
ofisi mbili za mikoa ya dar es
Salaam na Pwani.
Katibu wa chama cha Tanzania Labour Party (TLP),
Bw. Hubert Joseph, aliwaambia viongozi hao wa dini kuwa, kuzembea na kushindwa
kutekeleza baadhi ya maazimio baina yake na vyama vya siasa, Serikali
imesababisha machafuko ya amani pamoja na migogoro iliyojitokeza hasa katika
Uchaguzi mdogo wa Serikali za Mitaa uliofanyika hivi karibuni kwakushindwa
kutekeleza na kutetea, sheria, kanuni na taratibu za nchi kwa vitendo hususan
katika chaguzi.
“Vyama vya siasa tunapokaa na Serikali na kutoa mapendekezo
juu ya kipi kifanyike ili kulinda amani nchini, Serikali imekuwa ikikubali kwa
mdomo tu, lakini haitekelezi, sasa kama hali hii itaendelea hivi, amani ya nchi
yetu ni wazi itakuwa rehani,” alibainisha Joseph.
Naye Katibu wa NCCR-Mageuzi Wilaya ya
Kinondoni, Rajabu Kazimoto alikilalamikia Chama Tawala (CCM) kwa madai kuwa,
kinaenea uzushi kuwa vyama vya upinzani vinatishia kuvunjika kwa amani nchini.
Alisema dola ni chombo cha umma, hivyo haipaswi kukisaidia
chama chochote kupiga kampeni au kukijengea mazingira ya kukiwezesha kushinda
katika u wowote ukiwamo Uchaguzi Mkuu wa Wabunge na Rais, unaotarajiwa
kufanyika Oktoba Mwaka huu.
Kwa upande wa Chama Tawala CCM, Naibu Katibu Msaidizi Wilaya
ya Kinondoni Bw. Mwendwa Ikuu alisema lugha zinazotumiwa na baadhi ya wanasiasa
hususan wa upinzani wawapo majukwaani, ndizo zinazosababisha migogoro baina ya
vyama, na hatimaye kuzusha balaa na machafuko.
Ikuu alisema viongozi wa vyama vya siasa nchini hawana budi
kuwa makini na lugha zao wanapokuwa wanapozungumza na wananchi katika mikutano
mbalimbali ikiwamo ya hadhara.
“Lugha za matusi, kashfa na vitisho katika majukwaa ya siasa
baina ya chama na chama, serikali na chama kama hazitoepukika, basi tutaendelea
kuwa na migogoro na hata pengine kuvunjika kwa amani ya Tanzania pasipo
kutegemea,” alisisitiza .
Katika Mkutano huo, Mwenyekiti wa Taasisi ya kuimarisha Amani
Tanzania Wilaya ya Kinondoni, Alhaji Suleimani Mwenda, aliwataka Viongozi wa
Vyama vya Siasa nchini, kutanguliza utaifa mbele ili kulinda amani nchini.
Alhaji Suleimani alisema, vyama vya siasa havina budi kufuata
na kulinda taratibu na sheria za nchi kwa kuwa na wanachama sahihi na si
washabiki wa chama.
Alisema kwa kiasi kikubwa, taratibu na maelekezo katika vyama
vya siasa huvurugwa na kukiukwa na mashabiki na kwamba, ndio wanaosababisha
vurugu na upotevu wa amani katika jamii hasa nyakati za kampeni na mikutano ya
kisiasa.
“Chama kinapokuwa na washabiki wengi zaidi ya wanachama,
msimamo wake huwa hafifu kutokana na washabiki kutokubali kutii amri za chama
na viongozi wao. Mashabiki wapo katika chama ili kuchochea vurugu na kamwe
huwezi kuwaongoza,” alisema Alihaji Mwenda.
Aidha, aliwataka viongozi wa vyama vya siasa kuwaelimisha
wanachama umuhimu wa kuheshimu uanachama wao alioulinganisha na namna mtu
anavyoabudu na kuitii dini yake.
Parokia yazitunuku kanda
zilizoshinda uchangiaji
Na Josephine Nsolo
KANISA
Katoliki Parokia ya Kimara, Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, limewatunukia
baadhi ya waamini wake hati maalum za shukrani kutokana na michango yao ya
ujenzi wa Kanisa.
Hati hizo zilitolewa kwa waamini
hao Jumapili iliyopita na Paroko wa Parokia hiyo, Padri Fransis John, zilienda
kwa waamni wa Kanda nne, kati ya nane zilizochanga kiwango kikubwa cha fedha
kwa mwezi Desemba.
Kwa mujibu wa paroko huyo,
kanda iliyoshika nafasi ya kwanza katika uchangiaji huo unaofanywa kila wiki
kwa njia ya kuzishindanisha ni Kanda ya Stop- Over iliyochanga shilingi
6,750,000/- ikifuatiwa na Kanda ya Kanisani iliyotoa shilingi 592,000 huku
Kanda ya Jeshini ikichukua nafasi ya tatu kwa kutoa shilingi 572,000. Kanda iliyoshika
nafasi ya nne na kujipatia hati hiyo ni Tanesco iliyotoa shilingi 540,000/-.
Kanda nyingine zilizoshiriki
ingawa hazikupewa hati ni Korogwe A, Korogwe B, Bonyokwa na Kigango cha
King’ongo.
Padri Francis alisema kuwa,
Uongozi umetoa hati hizo kama ishara ya shukrani kwa waamini hao na kuwatia
moyo katika kazi ya ujenzi wa kanisa hilo linalojengwa kwa nguvu za waamini.
“Tumefarijika na moyo wa
waamini wetu kwa kubuni mbinu kamambe za uhamasishaji wa kila wiki uliotusaidia
kukusanya wastani wa shilingi 800,000/= kila wiki, tofauti na shilingi 70,000
hadi 100,000/= zilizokuwa zikikusanywa hapo awali,” alisema.
Paroko alisema Uongozi wa
Kanisa hilo uliwashirikisha waamini waliogawanywa katika kanda nane, kuchangia
angalao shilingi 1,000/= kila wiki ili
kusukuma zaidi upatikanaji wa fedha za ujenzi.
“… Wapo waamini ambao wamejitoa
kikamilifu na huchangia hadi shilingi 70,000/= kila wiki na wengine ingawa
uwezo wao mdogo, lakini wanajitolea kwa kile kidogo walichonacho,” alisema.
Hata hivyo, alisema baadhi ya
waamini bado ni wagumu na kutoa michango yao. “Lakini hatuwezi kukata tamaa,
tutaendelea kuwahamasisha,” alisema.
‘Yesu Kristo sio Nabii Issa bin Mariamu’
Na Mwandishi Wetu
WAKRISTO wametakiwa kuielewa vizuri
imani yao pamoja na imani za dini nyingine zinazoonekana au kusemekana kuwa na
uhusiano na Ukristo.
Wito huo uliotolewa na Paroko Msaidizi wa Parokia ya Kristo
Mfalme Tabata, Padri Gabriel alipokuwa akihubiri katika misa ya tatu katika
sikukuu ya Noeli (Krismasi).
Wito huo wa Padri Gabriel umekuja kutokana na mchanganyiko
kuhusu kufanana au kutofautiana kati ya Bwana Yesu Kristo katika Biblia na
Nabii Issa bin Mariamu katika Kurani.
Katika mahubiri hayo yaliyogeuka kuwa darasa na kuvuta
usikivu na umakini wa waamini, kiongozi huyo wa dini alisema kuwa Bwana Yesu
Kristo na Nabii Issa ni wawili tofauti kabisa kutokana na vigezo kadhaa.
“Tulipoambiwa kwamba Yesu Kristo ndiye Nabii Issa sisi
tukakubali tu. Hapo tulikuwa tumepotoka. Unakuta Mkristo anaambiwa kwamba nyie
mnasherekea Issa ambaye sio Mungu anakasirika na kutaka kupigana, kumbe sio
kweli ni ukosefu wa elimu tu,” alisema.
Alivitaja vigezo hivyo kuwa ni ukoo, utume, mahali na namna
walivyozaliwa, maana ya majina yao pamoja na ukoo wa Mariamu ambavyo kila
kimoja kinaonekana kuwa tofauti kabisa.
Juu ya kigezo cha ukoo, Padri Gabriel alisema kuwa wakati
Biblia Takatifu inaonesha kuwa Yesu alizaliwa kutokana na ukoo wa Mfalme Daudi
ambaye alitokana na mmoja wa watoto kumi na wawili wa Israel (Yakobo) aliyeitwa
Yuda, Kurani kwa upande wake inaonesha kuwa Nabii Issa bin Mariamu alitokana na
ukoo wa Haruni ndugu yake Musa.
“Utume wao sasa, wakati Bwana Yesu Kristo alikuja kutafuta na
kuokoa kilichopotea (kuokoa watu na dhambi zao), Issa bin Marimu alikuja
kufundisha watu namna ya kumwabudu Mungu na kuamini torati na baadaye,
akateremshiwa Kurani; yaani alikuja kuwafundisha watu dini,” alisisitiza.
Kwa upande wa namna walivyozaliwa, Biblia inasema kuwa Bwana
Yesu Kristo alizaliwa katika mji wa Bethlehem nchini Israel, wakati wa usiku na
katika zizi la ng’ombe; huku Kurani ikisema kuwa, Issa bin Mariamu alizaliwa
chini ya mti wa mtende wakati wa mchana nchi na mahali alipozaliwa
havijulikani.
Kuhusu maana ya majina yao, Padri Gabriel alisema kuwa jina
Yesu linatokana na neno la Kiebrani ‘Yehosua’ lenye maana ya mwokozi au
mkombozi; wakati Issa ni neno la Kiarabu lenye maana ya wekundu uliochanganyika
na weupe yaani zeruzeru au albino.
Alisema katika Biblia zilizoandikwa kwa Kiarabu jina Yesu
linajulikana kama ‘Yasu’ na sio Issa kama Waislamu wanavyodai na kama Wakristo
walivyoaminishwa kwa muda mrefu.
Alisema katika Kurani, jina Yasu lipo lakini huwa hawasemi
kama lipo bali wanasisitiza Issa tu, ambaye whana uhusiano wowote na imani ya
Kikristo.
“Ndugu zangu ni muhimu kuyaelewa mambo haya vizuri ili
tuheshimu imani na dini za wenzetu ili nao waheshimu imani zetu. Wao wana haki
ya kuheshimu imani yao na sisi pita tunapaswa kuwaheshimu,” alisema.
Wito huo wa Padri Gabriel ulikuja siku chache baada ya
kuripotiwa habari kwamba baadhi ya waamini wa dini za Kiislamu na Kikristo
walishambuliana na kupigana baada ya kudaiwa kukashifiana huko Tabata Kimanga
na kuvunja hali ya amani.
Wanasiasa wanageuza siasa
biashara - Mbunge
Na Mwandishi Wetu
MBUNGE wa Bunge la Afrika Mashariki, Dk. George Nangare,
amesema miongoni mwa matatizo yanayoikabili Tanzania, ni baadhi ya wanasiasa
kuigeuza siasa kuwa biashara huku wengine, wakiwamo wa Chama Tawala, kudhani
bado wako katika mfumo wa chama kimoja cha siasa.
Dk.
Nangare aliyasema hayo hivi karibuni wakati akizungumza na waandishi wa
habari, Ilala Dar es Salaam juu ya hali
ya kisiasa wakati huu ambao Tanzania inaelekea katika Uchaguzi Mkuu wa Rais na
Wabunge, Oktoba 2005 .
Alisema
kutokana na baadh ya wanasiasa kubweteka mawazo yao katika mfumo wa siasa wa
chama kimoja ambao Tanzania iliupa mgongo mwaka 1992, ipo haja kwa jamii kupewa
elimu zaidi ya uraia kuanzia ndani ya vyama vya siasa na katika sehe mu
mbalimbali.
“Hata
hizi vurugu zinazotokea katika chaguzi; tatizo ni kwamba kuna watu hata ndani
ya CCM ambao bado mawazo yao yanaamini one party system mpaka
sasa… Na wanasiasa wengine wanageuza siasa kuwa biashara badala ya utumishi wa
umma,” alisema katika mazungumzo hayo baada ya mahafari ya hivi karibuni chuoni
DSJ.
Hata
hivyo alisema kuwa, vurugu zinazojitokeza katika masuala ya kisiasa hususan
wakati wa uchaguzi, zinatokana na uchanga wa kidemokrasia uliopo miongoni mwa
jamii hivyo, akashauri Watanzania kubadilika na kukomaa kisiasa ili kwenda na
wakati.
“Demokrasia
ni changa sehemu nyingi duniani na hii ndiyo maana hakuna uchaguzi kamili
duniani, lakini kwetu Watanzania lazima tujitahidi kuonesha ukomavu wetu.
Inapotokea kutoelewana, watu wazungumze na kupata suluhisho kwa amani,” alisema
Dk. Nagare.
Aidha,
katika mazungumzo hayo Dk. Nangare alisisitiza kuwa, jukumu la kuzisaidia
taasisi mbalimbali nchini ni la umma mzima, lakini lazimaSerikali iongoze hali
hiyo.
Alikuwa
akijibu swali lililotaka maoni yake kuhusu taasisi mbalimbali kuichangia Timu
ya Soka ya Serengeti Boys ili ishiriki michuano ya kimataifa.
Alisema
kwa mantiki hiyo, si kwamba kila kitu Serikali ifanye peke yake, bali
Watanzania wajue wana haki, hiari na wajibu kuziunga mkono taasisi
zinazowawakilisha kitaifa na kimataifa.
Dk.
Nangare alisema, “Mwendo huu ni mzuri, lakini Serikali iweke mipango mizuri ili
isiwe kwamba kila taasisi inajiamria kufanya inavyotaka bila kontroo.”
Alisema,
Serikali kupitia wizara zake, itenge bajeti kwa vikundi vyote muhimu ili
kuepuka tabia ya wawakilishi wa nchi kupitisha bakuri kuomba misaada eti kwa
kuwa Serikali haikutenga bajeti.”
Papa ampa Umonsinyori Padri Mutabazi
BABA Mtakatifu Yohane Paulo wa Pili, amempa Padri Emmanuel
Mutabazi wa Jimbo Katoliki la Rulenge, heshima ya Umonsinyori.
Kwa
mujibu wa taarifa toka kwa Askofu wa Jimbo hilo Mhashamu Severine NiweMugizi,
Baba Mtakatifu alimpa Padri Mutabazi heshima hiyo Mwezi Novemba, mwaka jana
nchini Italia.
Mhashamu
NiweMugizi amesema, hadi anapata heshima hiyo, Padri Mutabazi (kwa sasa ni
Monsinyori), alikuwa Mhadhiri katika Chuo Kikuu cha Kanisa Katoliki Nchi za
Mashariki mwa Afrika (CUEA) kilichopo Nairobi, Kenya.
Akielezea
historia yake, Askofu NiweMugizi alisema, Monsinyori huyo mpya alizaliwa Julai
15, 1944 huko Runazi- Biharamulo. Baba yake ni Bw. Buswage na Mama ni Bibi
Kabengo.
Monsinyori
Mutabazi alibatizwa Desemba 24, 1944. Alipata Daraja ya Ushemasi Desemba 12,
1969 na Upadrisho Septemba 13, 1970.
Alipata
masomo ya Theolojia katika Seminari Kuu ya Kipapala tangu mwaka 1967 hadi 1970,
kisha akaenda katika Chuo cha Urbaniano
Roma kwa masomo ya Theolojia tangu mwaka 1971 hadi 1972. Pia, alipata
masomo ya Biblia huko Roma tangu 1972 hadi 1975.
Mwaka
1970, aliteuliwa kuwa Paroko Msaidizi wa Parokia ya Nyaishozi na mwaka 1971,
akatumikia wadhifa huo parokiani Ntungamo. Januari 1976 hadi Agosti mwaka
huohuo, alikuwa Paroko Msaidizi katika Parokia ya Rulenge na kisha, akaendelea
na wadhifa huo katika Parokia ya Nyakahura tangu mwaka 1976-1977.
Alikuwa
Mwalimu wa Biblia katika Seminari Kuu ya Kipalapala tangu mwaka 1978 na mwaka
1979 hadi 1980, alikuwa akifundisha Biblia katika Seminari Kuu ya Segerea.
Alikuwa
Mkuu wa Seminari (Rekta) ya Kibosho tangu mwaka 1981 hadi 1983 na akaendelea na
wadhifa huo katika Seminari ya Ntungamo tangu mwaka 1984 hadi 1986.
Januari 1987 hadi Septemba 1994 alikuwa
Mwalimu katika Seminari Kuu ya Segerea na tangu 1994 hadi 1997, alifanya kazi
katika Parokia ya Buziku akiwa Paroko, Mkurugenzi wa Utume wa Biblia na Katibu
wa Ekumene.
Septemba 1997 hadi Agosti 1998, alikuwa Mlezi katika Nyumba ya Malezi ya Chabalisa, Msimamizi wa Utume wa Biblia na Katibu wa Ekumene.