Darasa la Saba wamemaliza; sasa kifuate ni nini ?
JUMATANO
iliyopita wanafunzi takribani nusu milioni wa shule za msingi nchini, walifanya
mitihani
Hii ilikuwa kipimo cha
mwisho cha nini kilichopandwa na kila mmoja katika shamba
Tunapenda kutumia nafasi
hii kuwapongeza kwa kuvumilia na hatimaye kuikamilisha safari hiyo ndefu
iliyowapitisha katika milima na mabonde mbalimbali.
Tunasema tunawapongeza
kwani ni ujasiri mkubwa waliotumia kukamilisha safari hiyo licha ya vikwazo
mbalimbali ambavyo kwa namna moja ama nyingine, wamekumbana navyo.
Bado tunasema
tunawapongeza kwa kuwa ni wazi kuwa takribani asilimia 28 ya wanafunzi wenzao,
hawakumaliza safari hiyo.
Wengine walilazimika
kukatiza masomo yao kwa uzembe wa makusudi, wengine kwa kukatishwa tamaa na
jambo hili ama lile na wengine, kwa shinikizo la jamii wanamoishi ikiwa ni
pamoja na wazazi kuwanyima mahitaji ya shule na kuozwa kabla ya kukamilisha
masomo
Ni wazi kuwa wengine
hawakuhitimu masomo
Sisi tunawapongeza
wazazi na Taifa kwa jumla ambao walikubali kubeba na kutimiza jukumu sahihi la kuhakikisha kuwa vijana hao
wanapata haki yao ya elimu, na malezi ya msingi kwa maisha
Tunajua wazazi na walezi
wamejinyima mengi na wengine walilala njaa huku wengine wakitembea hata nusu
uchi ili mradi tu, wahakikishe watoto wao wanapata hazina hiyo ya elimu ambayo
ni msingi na ufunguo bora katika maisha.
Serikali ilijua hilo na
ndiyo maana pia ilijitahidi kutoa kipaumbele katika kupambana na maadui wale
wakubwa wa Taifa ambao ni umaskini, ujinga na maradhi.
Katika kuimarisha vita
dhidi ya ujinga hasa katika ngazi ya elimu ya msingi, ikaondoa vikwazo vyote
vya michango kwa shule hizo na kuboresha mazingiza ya wanafunzi kujifunza vema.
Hii ilikuwa pamoja na
kuongeza idadi ya walimu katika shule na kuchochea ongezeko la vyumba vya
madarasa ili kutoa uwiano bora wa mwalimu na wanafunzi katika darasa.
Pamoja na pongezi hizo,
bado tunawakumbusha wazazi, Taifa na jamii kwa jumla, usemi kuwa : Kulea
mimba si kazi, kazi ni kulea mwana na pia, Kumvua numbi si kazi, kazi ni
magawioni.
Tunasema hivyo kwa kuwa
sasa vijana hao wametoka katika ulimwengu wa shule ya msingi, wameingia katika
ulimwengu mpya ambao shetani anataka agawane na jamii adilifu ya kimungu ili
nae apate fungu lake.
Hiki ni kipindi hatari
Ni kipindi chenye vishawishi vingi vya hatari. Ni kipindi
ambacho shetani anawaalika na kuwavuta vijana kumfuata kwa kujitumbukiza katika
vitendo vya uhuni, ukiwamo ufuska, uvutaji bangi na ulevi wa ama pombe, au dawa
za kulevya.
Ni kipindi ambacho vijana wanapenda kupata maisha mazuri
bila kujua wala kufuata hatua muhimu za kuyafikia.
Pia, ni kipindi ambacho sasa, vijana wengi wanakuwa
katika hatari ya kujifunza kuuza mayai, karanga na sigara mitaani na
vilabuni ; ni kipindi ambacho shetani anawapa semina vijana juu ya kuwa
majambazi na matapeli huku akiwaalika wengine kuwa vibaka na wachomozi
wanaojificha katika upigaji debe kwa
kisingizio cha ugumu wa maisha na ukosefu wa ajira.
Ni kipindi cha vijana hawa kuanza safari kuiendeleza
'Nchi ya ahadi' yaani miji yetu mikuu kama
Dar es Salaam, Mwanza, Arusha, Mbeya na kwingineko. Wanaiendelea wakiwa
wamejaa matumaini ya kupata ajira ya kiutu, na kuwa na maisha mazuri, na katika
hali ya mshituko wanajikuta wakijiunga na jeshi la 'Machinga' wanaolazimika
kusaga lami na kupokea makali ya jua lote siku nzima bila kula ili kuuza (tooth
picks) njiti za kusafishia meno pale wale wanaokula wanapokuwa wameshiba.
Sisi tunasema, hiki ni kipindi kigumu, lakini muhimu sana kwa wazazi,
walezi, marafiki, asasi za kibinafsi na za Kiserikali, kuonesha upendo na
kuwajali vijana hawa kwa kuwafanya kuwa raia wema na watumishi bora wa Mungu.
Hatuna maana kuwa sasa jamii ielekeze nguvu zake katika
kuwapa chakula na pesa bure, la hasha ! Tunachosema, sasa vijana hawa
waelekezwe kilicho bora kufanya ili kujipatia riziki halali.
Wahimizwe kushiriki kikamilifu katika vikundi na asasi za
kidini ili kupata mafundisho mbalimbali yanayowajenga kiroho.
Wajengewe moyo wa kupenda kujiunga na kushiriki katika
vikundi vya uzalishaji mali ili wajitegemee kwa manufaa ya familia zao, Kanisa,
Taifa na hata kwa wao wenyewe.
Wazazi na jamii hawana budi kujua kuwa huu ndio wakati
muafaka wa kuwajengea vijana hao maisha bora ya siku za usoni, au kuwabomolea.
Kila mzazi ajue kuwa uzembe wowote utakaofanywa na mzazi
katika kipindi hiki, utakuwa ndio bei ya mauti ya mwanae na kilio kwa Taifa na
hasa wakati huu ambao ulimwengu umegubikwa na janga la UKIMWI na uhalifu wa
kila namna.
Tukumbuke usemi kuwa mtoto hakui kwa mzazi na kwamba,
mchelea mwana kulia, hulia yeye. Hivyo, wazazi hawana mwanya wowote wa kukwepa
majukumu ya kuwalea kimaadili vijana wao waliohitimu masomo na hata vijana hao
waliohitimu, pia ni nafasi yao kujua kuwa wazazi, Taifa linategemea mchango wao
wa hali na mali katika kulijenga.
Wajue pia kuwa macho ya jamii yote yanawatazama kwa
matumaini.
Kila mmoja ajionee aibu kuwa tunda lenye
sumu katika jamii na badala yake, awe tunda tamu lenye harufu na ladha tamu ya
matumaini inayovutia jamii, Taifa, Kanisa na kikubwa zaidi, kwa Mungu.
Umaskini ni nini? Na
maskini ni nani?
Ndugu Mhariri,
BILA shaka Watanzania walio wengi wanalifahamu sana,
licha ya kuliishi neno hili “umasikini”.
Pengine wengi wamewahi kuitwa
“maskini” na hata kutukanwa kwa maneno kama “mjinga wewe maskini tu.” Na mara
nyingine watu huonesha masikitiko yao kwa tukio fulani baya ambalo limempata
mwenzao wakisema, “maskini wa Mungu... !”.
Wanasiasa nao hasa katika
majukwaa yao ya kunadi sera na propaganda za vyama vyao, husikika mara nyingi
wakizungumza juu ya neno hilo umaskini hasa katika nchi zinazoendelea.
Wakristo nao katika ibada
mbalimbali kama Ibada ya Misa Takatifu, husoma Maandiko Matakatifu ya Yesu
Kristo akizungumuzia masuala mbalimbali juu ya “umaskini na maskini”
Nilijikuta katika tafakari
inayoibua maswali mengi mno juu ya maana
na matumizi sahihi ya maneno hayo.
Hivyo, lengo la makala haya
siyo tu kuelimisha jamii bali pia
kutafuta majibu kutoka kwa wasomaji na waandishi juu ya maswali
umaskini ni nini? Na maskini ni nani?
Tafakari juu ya maswali hayo
ilinirudisha nyuma mwaka mmoja tokea sasa. ninakumbuka
nilipokuwa mkoani Kagera nikifanya utafiti juu ya ‘chanzo na madhara ya
uharibifu wa mazingira mkoani humo’. Matokeo ya utafiti huo yalionesha
kuwa umasikini ni chanzo kimojawapo kati
ya vyanzo vingine vingi vya uhalibifu wa mazingira. Ilinibidi kutembelea wilaya
na vijiji mbalimbali ili nijionee uhalisi wa mambo.
Nikiwa katika kijiji cha Ruanda kilichopo tarafa ya Kamachumu,
Wilaya ya Muleba, nilibahatika kuzungumza na baadhi ya wanakijiji juu ya maana
ya umaskini.
Wao waliufafanua umaskini
kwamba ni hali ya chini kimaisha ambapo mtu anakuwa hana uwezo wa kuwa na
nyumba iliyoezekwa kwa bati, hana uwezo wa kumiliki baiskeli aina ya Phonex,
hana kuku angalau watatu, hana shamba la migomba, hana uwezo wa kupata
angalau mikungu mitatu ya ndizi kutoka kwenye shamba lake kwa wakati mmoja na
pia, mtu huyo hawezi kumudu kula ndizi kila mlo.
Maelezo ya wanakijiji hao
yalinifurahisha sana kwani yalinipa changamoto ya kuanza kujitathimini ili
nifahamu niko upande upi kati ya walio maskini na wasio kuwa maskini.
Mwisho, nikajikuta ninaangukia
kwenye kundi la wale watu ambao hawana uwezo wa kumudu gharama za kula ndizi
kwa kila mlo, pili hawana kuku hata mmoja na tatu hawana nyumba ya bati hivyo
basi mimi ni maskini.
Baada ya tathimini hiyo fupi
niliingiwa na hofu kubwa kwa kutoamini maelezo yao kwani yalipingana kabisa na
fikra nilizokuwa nazo awali juu ya maana ya umaskini na maskini ni nani.
Ili kuhakikisha ukweli wa
maelezo hayo, niliamua kutembelea Wilaya ya Karagwe. Wilaya hii ipo mpakani
kabisa mwa Tanzania na nchi jirani za Rwanda, Burundi na Uganda.
Nikiwa kule, nilibahatika
kukutana na jamii ya wafugaji ambao wana mifugo yao ndani na kandokando ya
Msitu wa Kimisi.
Wafugaji hao walieleza kuwa
umasikini ni hali fulani ya taabu na
dhiki na wakafafanua kwamba, maskini ni yule mtu ambaye hana uwezo wa kumiliki
anglau ng’ombe mia tatu, na hawezi kukamua ebyanzi (chombo rasmi mfano wa chupa ya chai
kinachotumiwa kukamlia maziwa) hamsini kwa wakati mmoja.
Nilipo muuliza mmoja kati yao
swali kuhusu uwezo wa kuwa na nyumba ya bati na uwezo pia wa kula ndizi kwa
kila mlo, alinishangaa na kunidharau kwani aliniambia kuwa nyumba za bati
hupiga kelele sana wakati wa mvua na hasa wakati wa usiku ambapo huwa ni wakati
wa kupumzika na kulala pono.
“Mvua zikinyesha huwezi kustahimili
makelele ya bati unalazimika kuamka,” alieleza.
Kuhusu uwezo wa kumudu gharama
za kula ndizi kwa kila mlo, alinidharau pia, akasema ndizi ni chakula cha
watoto ambacho mtu maskini asiye na maziwa, nyama na mihogo hushindia.
Sasa nikazidi kuchanganyikiwa
zaidi kwani maelezo yao yalitofautiana kabisa na kugongana na yangu na hata
kushindwa kuoanisha maelezo ya wilaya ya kwanza na hii niliyopo sasa.
Nilipoivinjali maktaba ya Mkoa
huo wa Kagera, kamusi na maandishi ya waandishi mbalimbali yalitafsiri
umasikini kama hali ya ufukara, udhaifu, unyonge, uhoehae, hali ya kuwa na
dhiki, upungufu, ukosefu na uhitaji.
Nao wataalam wa uchumi na
maendeleo wao wanasema kwamba umasikini ni hali ile ambapo mtu anakuwa hana
uwezo wa kupata mahitaji yake ya msingi kama malazi, chakula na mavazi.
Tafakari yangu juu ya “umasikini ni nini?” “Na masikini ni
nani?” haishii tu katika kusimulia yaliyotokea wakati nilipokuwa ninafanya
utafiti mwaka mmoja uliopita, bali hata
leo hii ambapo mikutano mingi ya kitaifa na kimataifa inafanyika ili kutafuta
mbinu na mikakati ya pamoja ya kuuondoa umasikini duniani.
Ukienda kanisani utasikia
maneno haya yaani umaskini na maskini, yakitamkwa ama katika Injili au katika
mahubiri.
Ebu tujiulize tena “umasikini
ni nini?” “Na masikini ni nani?”
Wakati mikakati na mbinu ya
kuondoa umaskini inaendelea Yesu Kristo katika Maandiko Matakatifu kupitia
waandishi Luka, Mathayo, Marko na Yohana, anaonekana kuipenda na kuifurahia
hali ya umasikini akionesha sababu kwamba hali ya umasikini itamfanya binadamu
kuufikia na kuupata ufalme wa mbinguni.
Mfano katika Injili ya Luka,
inaeleza “Heri ninyi mlio maskini kwa sababu ufalme wa Mungu ni wenu”. (Lk 6:
20).
Katika Injili hiyo hiyo ya
Luka tunaelezwa habari za Lazaro, mtu aliye kuwa maskini, alivyoupata ufalme wa
Mungu (Lk 16:19-31)
Maneno hayo ya Yesu Kristo
yananitia raha na matumaini katika roho yangu.
Wengi wetu tunaitwa maskini na
nchi yetu imetengwa kwenye kundi la nchi zilizo maskini.
‘Heri ninyi mlio maskini kwa
sababu ufalme wa Mungu ni wenu.”Huenda Watanzania wakafarijika sana na matamshi
haya.
Lakini; kwa maana hiyo
mikakati na mbinu za kuondoa umaskini
kwa mtazamo huu huenda ukatuingiza mahala pengine na sio kwenye njia ya
kutuelekeza katika ufalme wa Mungu?
Na je,
tuufurahie na kuuenzi umaskini kwa sababu Yesu Kristo ameubariki? Au tufanye
kila tuwezalo ili tuondoe huu umasikini wetu wakati huo tukijua kabisa kwamba
kufanya hivyo kutapelekea sisi kuikosa nafasi
ya kuingia katika ufalme Mungu? Maana imeandikwa heri maskini?
Je, kuna sababu ya kuhangaika
na mambo ya mbinguni wakati ya hapa duniani yanatushinda?
Hivi ni kweli kwamba umaskini
aliouongelewa Yesu Kristo hauna tofauti na unaongelewa sasa? Je, matajiri wao
hawana nafasi ya kuingia katika ufalme wa Mungu?
Pamoja na maelezo na fafanuzi zote hizo, bado
ninauliza na nina hamu ya kujua “umaskini ni nini?” “Na maskini ni nani?”
Ninakaribisha maoni au majibu
kupitia Gazeti hili
Edward
Mujungi,
S.L.P. 2133,
DAR ES
SALAAM.