BARAZA LA MAASKOFU KATOLIKI TANZANIA

MAONI YA BARAZA LA MAASKOFU KATOLIKI TANZANIA KUHUSU MASUALA KADHAA YA NCHI YETU

TUYAONAYO NA TUYASIKIAYO

Wakati Taifa linaelekea kwenye uchaguzi Mkuu wa madiwani, wabunge na Rais, wanasiasa wako kwenye hekaheka za kugombea nafasi za uongozi, raia wengi hawajatambua kinachoendelea na wachache wanaotambua wamejawa na wasiwasi.

Sisi Maaskofu kama wachungaji tunaona na kusikia mengi ambayo yanatupatia wasiwasi sana. Kwa mfano. idadi ya vijana na watoto wasioweza kulipa ada na michango ya shule inazidi kuongezeka. Katika familia hasa akinamama na watoto wengi wanakosa huduma za afya.Wakulima wanakosa nyenzo na wanahangaishwa na soko huria. Wanakosa utetezi na ushauri ufaao dhidi ya wanunuzi binafsi. Kadhalika Taifa lina tatizo la vijana wengi kukosa ajira halali. Haya yote yanachangia kuongezeka kwa tabaka la wanyonge katika Taifa letu. Tabaka la matajiri wachache wenye uwezo linazidi kupata nguvu. Wakati huo huo Serikali inajali zaidi uhai wa uchumi wa kifedha kuliko uhai wa maisha ya jamii.

DEMOKRASIA YETU

Tulipoanza mfumo wa vyama vingi vya siasa tulikuwa na tumaini la kupanua demokrasia yetu. Tulitambua kwamba jukumu hilo litachukua muda mrefu. Ni wajibu wa Serikali kuhimiza, kulinda na kuendeleza jitihada hizo. Kutokana na tunayoyaona na kuyasikia tunajiwa na maswali mbalimbali.

Kwa mfano, mabadiliko ya Katiba yanayoendelea kutokana na "White Paper" je, yanatekelezwa kwa manufaa ya Watanzania wote au wenye madaraka tu au kikundi cha watu wa sehemu fulani?

Je, Serikali inalinda haki na fursa za vyama vya upinzani ili kurahisisha juhudi zetu za kujenga demokrasia; kwa mfano kutoa ruhusa na ulinzi katika mikutano ya vyama hivyo?

Je, kuna uwazi na mshikamano ndani ya chama tawala au kuna kuogopana na kutumia mbinu za ujanja ili kuhodhi madaraka? Je, ndani ya chama kuna nafasi ya kutathmini kwa kina na makini sera na mifumo mbalimbali?

Vilevile katika vyama vya upinzani, je, kuna demokrasia ya kweli? Ni kwa misingi gani wanachama wanachagua viongozi wao na kuwagombea wakati wa uchaguzi? Je, vyama hivi vinaleta sera yoyote ya pekee katika Taifa letu au ni kulalamika tu? Inakuwaje basi kwamba Taifa linakosa fursa ya kuchagua sera tofauti au maoni tofauti mintarafu utekelezaji bora zaidi wa sera?

MWALIKO WETU KWA WATANZANIA NA KWA VIONGOZI

Tunawaalika watu wote wenye mapenzi mema kumwomba Mwenyezi Mungu atuangazie ili tuweze kuwatambua na kuwachagua watu watakaoongoza vizuri nchi yetu katika miaka ijayo.

Tunawaalika waamini wauone uchaguzi ujao kama sehemu ya kufanikisha Jubilei Kuu na fursa ya kushirikiana na Mungu katika kujenga Taifa letu kufuatana na mipango yake.

Tunapenda kuwahimiza na kuwaelekeza raia wa Tanzania wasiogope kutoa mawazo yao katika nafasi mbalimbali hasa sasa na wakati wa kampeni za uchaguzi. Wasiogope kuwahoji viongozi juu ya kazi zao na kudai ripoti zitakiwazo.

Raia wajifunze kutetea haki na maslahi yao na kuilazimisha Serikali ijifunze kuyapa kipaumbele mahitaji ya jamii badala ya kuridhisha tabaka la wenye uwezo. Kwa mfano, mara nyingi jibu la Serikali huwa:"T unaelewa shida yenu, lakini Serikali haina uwezo". Lakini papo hapo kuna tabaka fulani la watu ambao wanapata fedha nyingi au upendeleo wa vifaa!

Ikumbukwe kwamba sauti ya Taifa siyo vyama vya siasa tu bali ni watu wote. Pia ikumbukwe kuwa mtawala yeyote ni mtumishi wa raia na analipwa kwa kodi yao.

Kugombea nafasi ya uongozi ni tendo jema kwani linampa fursa yule anayechaguliwa kutoa huduma kwa raia. Kiongozi anayetekeleza wajubu wake vizuri anampendeza Mwenyezi Mungu na ataheshimika na watu wote (Yn 12:26; Rum 14:18) Kiongozi wa aina hiyo huwa na tabia kama zifuatazo:-

v Mkweli: Hatoi ahadi za uongo wakati wa kampeni na akiwa kiongozi hadanganyi watu.

v Mwaminifu: Hukumbuka kwamba anawakilisha wapiga kura, kwa hiyo hutetea watu siyo kutetea chama tu. Kamwe hasaliti tunu za Taifa letu na maslahi ya watu.

v Kujitolea: Hujitolea na kufikiria nafuu ya wengi kuliko ya nafsi yake. Hujitolea muda wake,afya yake na hata haki zake kwa ajili ya manufaa ya wengi. Yuko tayari kupoteza cheo chake au nafasi nzuri kwa ajili ya kutetea ukweli, haki na manufaa ya wengi

v Anaongozwa na tunu za Msingi: Tunu hizi ni pamoja na uhai, utu, uhuru, amani na usawa kama zinavyodokezwa katika utangulizi wa Katiba ya Tanzania. Kisiasa tunu za msingi ni pamoja na umoja, usawa na demokrasia. Kiongozi hashughulikii mambo madogo madogo na kuyafukia yaliyo ya msingi.

KUHUSU KATIBA NA KAMPENI ZA UCHAGUZI

Katiba ndiyo sheria ya msingi inayoeleza matashi ya raia wa Tanzania na jinsi gani wanataka kutawaliwa na kuongozwa. Katiba si chombo cha kuchezewa au kupuuzwa na utawala bali utawala ni mtumishi wa Katiba.

Onyo letu ni kwamba viongozi wasibadili Katiba kimchezomchezo. Mabadiliko yasifanyike kipande kipande kufuatana na maslahi ya kisasa, au ya kundi au mtu mmoja.

Ili uchaguzi unaokuja utuletee viongozi wanaofaa, tunahimiza kila chama kiwe makini kabisa katika kupendekeza wagombea wenye sifa zitakiwazo.

Vyama viache tabia ya kutumia fedha na marupurupu kuwarubuni watu katika kampeni. Pesa zilizotengwa kwa ajili ya idara na huduma za Serikali na miradi ya maendeleo zisitumike kwa ajili ya kampeni.

HITIMISHO

Tumetoa mahusia haya kwa sababu tunataka Taifa letu lipate Viongozi wenye uwezo na uadilifu. Tunataka waongoze Taifa letu katika upendo, uhuru, haki na amani. Hiyo ndiyo sala yetu kwa Mwenyezi Mungu kwa ajili ya Taifa letu katika mwaka huu wa uchaguzi mkuu.

U Justin Samba

Rais wa

BARAZA LA MAASKOFU KATOLIKI TANZANIA

Kwa niaba ya Maaskofu Katoliki wa Tanzania

Imetolewa Makao Makuu ya Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania, Kurasini