Mahubiri ya Moses Kulola ni kikwazo kwa waumini wa Bwana wetu Yesu Kristu

Hili ni jibu kwa Moses Kulola baada ya kusoma mahubiri yake kwenye gazeti la Nipashe Jumapili Aprili 23,2000 Uk.1 na 2.

Wafuasi wa Yesu walio waaminifu tuna mashaka sasa kadri tunavyoendelea kusikia mahubiri ya wale wanaoitwa watumishi wa Mungu, kwani wanakoelekea wameacha agizo walilopewa na kiongozi wetu Mkuu wa Imani yetu YESU KRISTO (Waebrania 12:2)

Moses Kulola ni mmoja kati ya viongozi waliopo hapa nchini ambao huongoza na kusikilizwa na wafuasi wengi, naye hufanya mihadhara mbalimbali. Hivyo chakusikitisha ni pale tunapoona baadhi ya mahubiri yake hayafundishi Imani ya YESU KRISTO badala yake huwakwaza.

Labda uaskofu wake hakuwepa na Yesu Kristo bali ni kutoka kwa wanadamu tu ambao hawajui mapenzi ya Mungu yaliyo halisi.

Kitendo alichofanya mhubiri huyo hapo Kidongo Chekundu (labda na sehemu nyingine pia) cha kufundisha watu kuwa Mwenyezi Mungu amewaweka wauguzi na madaktari ili kuwasaidia wagonjwa ni kitendo kinachomfanya asiwe mmoja wapo wa wafuasi wa Bwana wetu Yesu Kristo.

kwani watumishi aliowaweka Yesu Kristo hapa duniani wawe mawakili wa siri za mbinguni ni hawa, Waefeso 4:11-16 'Naye alitoa wengine kuwa Wachungaji na Waalimu kwa kusudi la kuwakamilisha watakatifu hata kazi ya huduma itendeke, hata mwili wa kristo ujengwe..."

Biblia inatuonyesha wazi Bwana Yesu ndiye aliyewachagua kazi yake na amewapa kielelezo jinsi ya kufanya kazi. katika kitabu cha Mathayo 9:37 -38 na 10:1,7-8..Basi mwombeni Bwana na Mavuno apeleke watenda kazi katika mavuno yake. Akawaita wanafunzi wake kumi na wawili akawapa AMRI juu ya pepo wachafu, wawatoe, na KUPOZA MAGONJWA YOTE na udhaifu wa kila aina. Na katika kuenenda kwenu hubirini mkisema Ufalme wa Mungu umekaribia. Pezoni wagonjwa fufueni wafu, tukaseni wenye ukoma toeni pepo,mmepewa bure toeni bure".

Hii ndio maana hata Moses Kulola hukiri na kusema" wagonjwa na wenye shida mbalimbali wataombewa, karibuni wote" kwanini asiache wagonjwa waende hospitali, bali anawaita kuwaombea?

Madaktari na wauguzi wamesomea na kupasishwa na wanadamu, Moses Kulola naye labda uaskofu wake amesomea; lakini wanafunzi wa Yesu Kristo au Mitume wake sio wa kusomea na kupewa shahada ya utumishi bali ni vipawa vya Roho Mtakatifu apewavyo muumini Je Moses Kulola (na kila mwenye imani hiyo) ni mfuasi mwenzetu wa Yesu Kristo? Mbona matunda yako (mahubiri) uliyonayo hayatokani na shina ambalo ni Yesu? Ikiwa wewe unamtilia mashaka Yesu kuwa hawezi au hatawaponya ukimwi eti kwa sababu umeingia kwa uzinzi je kama ni hivyo dhambi yenyewe ya uzinzi, Bwana Yesu atashindwa kuisamehe na kuifuta kabisa? kama dhambi ambayo ni kazi ya shetani itamshinda je shetani mwenyewe hatapiga goti kwa Yesu? sasa utueleze anamtumikia nani kama si imani haba!.

Sisi wanafunzi wa Yesu tulimpinga Kakobe pia aliposema ameanzisha operesheni ya kuwaombea na kuwaponya wagonjwa wa ukimwi huku akiwataka waende na vyeti toka kwa daktari, Sivyo bwana Yesu amesema 'Pozeni magonjwa yote nakila aina ya udhaifu' tena ana uwezo wa kusamehe dhambi zote kwani dawa ni maungamo tu.

Hivyo natoa wito kwa watu wate kuwa wasibabaike kusikia jina la Askofu wa Kimataifa au Askofu Mkuu mwenye vyeti kutoka kwenye vyuo vya kidunia; kwani hao hawakutumwa na Bwana wetu Yesu Kristo bali ni wasomi tu wasio na Imani ya Bwana wetu Yesu Kristo.

Hao wanaokiri kuwa wanamjua Yesu 'wenye mfano wa utumwa lakini wakikanga nguvu zake hao nao ujiepushe nao' 2Timotheo 3:5.

Katika Biblia Musa alitumwa na Mungu kuwa aweke Nyoka wa Shaba juu ya mti pindi mtu aking'atwa na nyoka mwenye sumu, amtazamapo Nyoka wa Shaba apate uponyaji. huo ndio uwezo wa Mungu wa uponyaji tangu zamani. Kadhalika hata leo wagonjwa wa kila aina na wenye dhambi wote waende kwa Yesu (aliyewafia msalabani) kwa njia ya Imani wataokoka ndio kupona Bwana Yesu hasemi kama Moses Kulola au mmojawapo wa hao wasioamini kuwa ukipata Ukimwi kwa njia ya zinaa hata ukiombewa hutapona.

NI UONGO MTUPU HUO labda ni agizo la chuo chao na na sio agizo la Bwana Yesu kamwe wala sio Injili ya kweli kwani hakuna ugonjwa siotii mbele za Yesu.

Magonjwa ni kazi za shetani na waliopewa amri juu ya shetani hapa duniani sio madaktari na wauguzi bali ni wanafunzi wa Yesu tu. Bwana Yesu ameyachukua magonjwa yetu yote tena yeye ndiye Bwana atuponyae kwani ameweka wahudumu kanisani ili mtu akiugua awaite wazee (wahudumu) wamwombee wampake mafuta kwa Jina la Bwana Yesu (Yakobo 5:13-15), wazee wa kanisa sio madaktari.

Wafuasi wa Yesu hapo sio kwamba hatutaki kwenda hospitali bali ipo njia ya waaminio ambayo hutoa uzima bure kwa njia ya imani ya Yesu.

Tena ukiamini hatakuwa na haja ya madawa, kwani unao uzima wa mwili na roho katika Kristo. Mnaotegemea madawa ni wazi kuwa mmeshindwa katika imani (kiroho) na kuenenda kimwili, basi ni kweli na wazi Yesu ni yeye yule jana na leo nahata milele tena ana uwezo wa kusamehe dhambi kuponya magonjwa yote na kufufua wafu pia.

Mwamini Yesu leo utaokoka Ameni

Mchungaji Peter Mattimba

Mchungaji Msaidizi

Kanisa la Full Salvation Church

 

 

KAULI YETU

Je, Ukahaba nchini uvikwe taji la Heshima?

HIVI karibuni Shirika la Uchumi la Wanawakae Tanzania SUWATA liliendesha semina maalum kwa ajili ya makahaba jijini juu ya namna ya kuepuka kupata mimba au maambukizo ya UKIMWI.

Katika Semina hiyo iliyofanyika katika hoteli ya Ambassador Plaza na kuwashirikisha changudoa zaidi ya thelathini, mbinu mbalimbali za kinga kama vile matumizi ya Kondom na kadhalika zilifundishwa.

Mkurugenzi wa SUWATA Mama Magreth Kota alikaririwa na vyombo vya habari akisema kuwa semina hiyo ina nia njema kwani baada ya kuwafunza changudoa hao mbinu za kujihami na mimba na magonjwa ya zinaa ,hatua itakayofuata ni kuwashawishi waachane kabisa na biashara yao hiyo ya kuuza miili.

Kwa mtazamo wa juu juu Semina hiyo inaweza hasa kwa jamii inayoelekea katika upotofu kuonekana yenye manufaa. Lakini ukweli ni kwamba madhara yake ni makubwa kuliko faida.

Kwanza hatua hiyo japo inajenga uhusiano mzuri kati ya jamii ya kawaida na ile ya changudoa lakini pia inawafanya changudoa waanze kuhisi kutambuliwa kwa shughuli yao haramu ya kujiuza. Kwa nini wasihisi hivyo wakati jamii imejitolea kuwafundisha mbinu za kupunguza hatari zinazowakabili katika kazi hiyo ya ukahaba? Lipi litakalowafanya wasitafsiri hatua hiyo kama kibali cha jamii kwa 'endeleeni na ukahaba, lakini jilindeni?"

Jamii nyingi za Magharibi (nchi za Ulaya na Marekani) zimefikia mahali pa kuzitambua tabia chafu za makahaba na hata mashoga kuwa halali na hata kuwalinda kwa sheria.

Vyama vya Makahaba katika nchi hizo vimeandikishwa na vinaendesha shughuli zake na kuandikisha wanachama wapya bila matatizo na hata kufanya sherehe za maadhimisho mbalimbali ya kutukuza uovu wao.

Tunachelea kwa mafunzo haya yanayotolewa kwa Changudoa ni hatua za awali za kuelekea katika upotovu huo wa kimagharibi. Tunaamini pia kwamba jamii ya Watanzania isipopiga vita hatua hiyo ingali katika hatua za awali kwa kuwa sisi nasi si kisiwe pekee katika dunia hii iliyopunguzwa sana ukubwa wake na sayansi katika muda mfupi tutafikia pale tusipotaka kufika.

Kwa mujibu wa Mkurugenzi wa SUWATA baada ya mafunzo hayo shirika lake litawashawishi machangudoa waachane kabisa na 'kazi' yao.

Sisi tunaamini kuwa baada ya kuwafundisha changudoa namna ya kufanya kazi yao kwa 'usalama zaidi' kama waitavyo kazi ya kuwashawishi waachane na ukahaba inakuwa ngumu maradufu.

Unawezaje kumsaidia adui yako kuimarisha silaha zake kisha useme hiyo itakurahisishia kupigana naye vita? Moja ya vikwazo vinavyopambana na changudoa hivi sasa ni hofu ya ujauzito na magonjwa ya zinaa ikiwa ni pamoja na Ukimwi.

Tunaamini kuwa njia bora ya kuwasaidia ingekuwa kuwapatia semina juu ya ubaya wa kazi ya ukahaba na kuwapatia uwezo, nyenzo na mbinu za kuendesha miradi halali mbadala ya itakayowezesha kupata riziki zao.

wale walioathiriwa sana na shughuli ya ukahaba wangepatiwa huduma ya muda mrefu ya ushauri nasaha.

Lakini kuwapa semina ya namna ya kujiepusha na maambukizi ya zinaa wawapo katika uovu wao ni kuuvika taji la heshima ukahaba wao.