Athari za kuwatunukia na kuwarudi watoto

KWA kawaida binadamu yeyote hupenda kutiwa moyo na hujisikia vibaya anaposhutumiwa, japo anaweza kukosolewa kistaarabu asijisikie vibaya. Kwa watoto wadogo umakini zaidi unahitajika kuliko ilivyo kwa watu wazima kwa vile wanahitaji kutiwa moyo kwa kila wanalojifunza ili wajenge tabia ya kujiamini. Kuwashutumu kila mara kuna madhara makubwa kuliko faida. Endelea na Mfululizo wa makala zetu kutoka kitabu cha Shirika la Uchapishaji wa Lugha za Kigeni la Beijing, China juu ya Afya.

HAMU ni mwalimu mwema. Jambo la namna ya kuchochea hamu ya mtoto ya kupenda masomo linazidi kuangaliwa.

wazazi wengi hutumia njia ya kutunukia na kuwarudi watoto wao ili kuchochea hamu yao . Lakini hawajui kwamba kuwatunukiwa na kuwarudi huweza kushusha hamu kwani hami inayochochewa kwa njia hiyo huwa ya muda tu.

Kwa nini basi inatokea hali ya namna hiyo? Kwanza, kusoma sawasawa na kucheza ni jambo la kufurahisha na linategemea hiyari ya watoto Kama watoto wanajifunza masomo yaliyolingana na kiwango chao cha akili na wanapata furaha katika wakati wa kusoma, wataweza kujifunza kwa hiyari yao. Katika hali hiyo kuwatunukia kutaweza kushusha hamu iliyowajia kwa hiyari. Uchunguzi ufuatao unaweza kuthibitisha ukweli huo. Tuwagawanye watoto wanaopenda kuchora kuwa vikundi viwili. Watoto waitwe kuingia katika chumba kidogo mmoja baada ya mwingine. Watoto wa kikundi cha kwanza waambiwe, "Mtoto anayechora picha nzuri atatunukiwa" Zawadi ni kitabu chenye picha nzuri, ambacho huwavutia sana watoto. Halafu watoto wakachora kwa furaha na kupewa zawadi.

Kwa watoto wa kikundi cha pili wasitajiwe zawadi ila waambiwe, "Napenda sana kuona picha iliyochorwa na mtoto. Je utapenda kunichorea picha moja?" Baada ya kusikia maombi ya watu wazima wataanza kuchora picha. Mwishowe tukihesabu picha picha tutagundua kwamba picha zilizochorwa na watoto wa kikundi cha kwanza ni nyingi sana. Hii inaonyesha kwamba kutunukia kunaleta matokeo mazuri zaidi. Lakini jambo linalostahili kuangalia ni kwamba wiki mbili baadaye tangu kufanya uchunguzi huo hatuna budi kuchunguza jinsi watoto wanavyocheza nje ya wakati wa masomo. Wanaweza kuchezea vipuzi vyao au kuchora picha. Wawekee kalamu na karatasi mezani na kila atakayependa kuchora, basi atachora tu. Mwishowe tutagundua kwamba picha zilizochorwa tu. Mwishow tutagundua kwamba picha zilizochorwa na watoto wa kikundi cha kwanza, yaani wanaotunukiwa zawadi ni chache sana.

Hii ni kwa sababu hamu yao ya kuchora picha imeshuka lakini, watoto wa kikundi cha pili wanaendelea kupenda kuchora picha kama zamani kwani shauku yao haikutawaliwa na zawadi, kwani shauku yao haikutawaliwa na zawadi bali na uchoraji tu.

Kwa hivyo, kutunukia kunaweza kuchochea hamu ya watoto katika muda maalum tu, na tunaposita kufanya hivyo hamu itashuka sana hata ikawa kidogo kuliko zamani.

Pili matokeo ya kusoma hayaonekani Mtu fulani anaposema "anafanya juhudi kwa ajili ya kutanzua matatizo" lakini pengine anafikiri mambo yasiyohusiana na masomo yake.

Hali hii haiwezi kutambuliwa kutoka kijuujuu. Kutunukia na kurudi kunategemea matokeo ya matendo, siyo kuzingatia kiwango cha juhudi yake. Hivyo ikatokea hali ya mtu anayetanzua tatizo atatunukiwa na asiyetanzua tatizo ataadhibiwa" Matokeo yake ni kwamba baadhi ya watoto wanafikiri : Ninajifunza kwa bidii sana, kwa nini siwezi kupata zawadi badala ya kualaumiwa? Watajihisi kuwa ni watu wasiokuwa na uwezo na hivyo kufifisha hamu yao ya kusoma.. Alikuweko mtu mmoja aliyewahi kufanya uchunguzi fulani kuhusu watoto. Watoto walifanya jihudi kubwa kutafuta lakini hawakufanikiwa baada ya kumaliza swali hilo watoto walipewa swali jingine yaani walitakiwa kutunga maneno yenye maana kwa kutumia herufi zilizotawanyika. Swali hili ni rahisi sana walakini matokeo yalionyesha kwamba watoto walioshindwa mara nyingi katika swali la kwanza walishindwa tena. kwa mujibu wa uwezo wao ilikuwa rahisi kwao kujibu swali hilo, lakini baada ya kushindwa mara nyingi walijihisi kwamba hawana uwezo tena.

wakaona kwamba hata kama watafanya kwa juhudi kiasi gani bado hawataweza kufaulu. Matokeo yatakuwa tofauti kabisa kama wakipewa swali rahisi kwanza na wanatanzua vizuri kwa juhudi zao.

Bila kuzingatia kiwango cha juhudi cha watoto tunawarudi eti kwa sababu hawawezi kutanzua swali kwa kufanya hivyo hata baadaye wakikuta swali lililoweza kutanzuliwa hawatokuwa na hamu ya kufanya hivyo jambo ambalo la kusikitisha ni kwamba katika wakati fulani mtu akikosewa kuadhibiwa atajiona yeye ni mtu asiyekuwa na uwezo. hivyo hujenga mazoea ambayo humuathiri kwa upande mwingine.

Kwa ajili ya kukuza akili ya watoto tusitumie akili nyingi katika kuwatunukia na kuwarudi watoto, bali tungefanya chini juu katika kuwafundisha watoto jinsi ya kujifanyia mambo yao kwa furaha.

Watakatifu Paulo na Petro: Mitume waliouawa kinyama mithili ya kuku asiyekuwa na mwangalizi

MANENO ya mitume hao wawili ambayo ni ya maana zaidi kuyakumbuka ni mengi. Wafilipi waliandikiwa barua na mtume Paulo akisema "Ninavyoona kila kitu ni hasara kwangu; hasara tupu, kwa ajili ya jambo bora zaidi yaani kumjua Bwana wangu Yesu Kristo"

Maneno hayo yapo kwenye kitabu cha Wafilipi 3:8.

Na tena Mtakatifu Mtume Paulo akaongeza tena maneno mengine makubwa yaliyopatikana katika (2 Tim .:12) akisema, "namjua yule niliyemwamini na nina hakika kwamba yeye anaweza kukilinda salama mpaka siku ile"

Naye Mtakatifu Petro baadhi ya maneno yake makuu ni "Bwana wewe wajua yote, wewe unajua kwamba ninakupenda" na alipomuuliza Yesu, "sisi tumeacha yote na tutakufuata tutapata nini basi?"

Akajibiwa kwamba "Ninyi mlioacha yote na kunifuata mimi mtapokea mara mia na kurithi uzima wa milele"

Labda kwa kumtazama Petro, tunambiwa alikuwa miongoni mwa mitume waliokuwa pamoja na Simoni Bin Yohane aliyekuwa mtu mwenyeji wa Betsaida mkoani Galilaya huko Israel.

Yeye Simoni Bin Yohane alikuwa mvuvi alipoitwa na Bwana Yesu ili amfuate. mara Simioni Bin Yohane alikubali akaziacha nyuma zile nyavu zake, mashua yake na hata ndugu zake.

Basi Petro tuliyemuona kuwa miongoni mwa mitume aliyekuwa wa kwanza kuungama kwamba Yesu ni Mungu akisema "ndiwe Kristo mwana wa Mungu Mzima" ndipo Bwana alipomweka kuwa mchungaji wake Mkuu wa kundi lake lote yaani kanisa, akasema.

"Wewe ndiwe Petro (maana yake ni mwamba) na juu ya mwamba huu nitalijenga kanisa langu na nguvu za jehanamu hazitaweza kulishinda."

Petro alikuwa mtu hodari sana na alimpenda mno mwalimu wake hata akataka kumfia. hata katika bustani ile ya kule Gestemane alijaribu kumtetea kwa upanga ingawa baadaye alikuja jionesha kuwa mwoga alipomkana Yesu mara tatu.ndiyo maana hata baada ya kufufuka kwake Bwana Yesu alimuuliza mara tatu kama kweli alimpenda kikwelikweli.

Petro ndiye aliyekuwa wa kwanza kutoa hotuba na kuanza kuwabatiza watu na ndiye yeye huyo aliyembatiza Korneli yule mtu wa kwanza ambaye hakuwa Myahudi aliyetaka kumwamini Yesu Kristo.

Petro alifanya hivyo akiitikia sauti aliyosikia katika njozi na baadaye akahudhuria katika mikutano mjini Yerusalemu ambapo Mitume waliamua kuwa siyo lazima kwa wakristo wa mataifa kushika sheria ya Musa.

Kisha Petro alipohama hapo Yerusalemu akaenda huko Antokia Uturuki na kulisimamia Kanisa la mji huo kisha baada ya miaka kadhaa Petro alihamia Roma akawa Askofu wa kwanza wa mji huo.

Tunaambiwa kuwa wakati ule wa utawala wa Kaisari Nero Wakristo waliodhulumiwa mno na ndivyo hali hiyo ilivyompata pia Petro alikamatwa na kufungwa gerezani kwa ajili ya dini yake ya kikristo.

Pia tunaelezwa kuwa kati ya mwaka 64 au 65 Petro anayekumbukwa na kanisa kila tarehe ya 29 ya mwezi Juni kila mwaka Pamoja na Mtume Paulo, alihukumiwa kifo kwa ajili hiyo ya dini yake.

Kwa kadri ya mapokeo Petro alihukumiwa akasulubiwa kichwa chini na miguu juu kwa sababu alivyoona yeye mwenyewe. hakustahili kusulubiwa sawa na na Bwana wake Yesu Kristo. Mtakatifu Paulo yeye alikuwa ni mwenyeji wa mji wa Tarso huko Uturuki na inaelezwa kuwa alizaliwa katika familia ya Wafarisayo.

Yeye mwenyewe anaelezwa kuwa hapo awali alikuwa mtesi mkali sana wa wakristo kwa kuwa aliona namna yao ya kuishi ilikuwa kinyume kabisa na Sheria za Musa.

Alipoelekea Damasko nchini Siria aliguswa na neema za bwana akaona ukweli ulivyokuwa Paulo sasa akawa hapo Paulo alikwenda Arabia na kwa kadri ya masimulizi ya mapokeo alikaa mwenyewe jangwani akifundishwa na Bwana wetu mwenyewe mambo mengi ya dini ya kikristo kwa namba ya kiroho.

Baadaye Paulo akawa muumini mzuri wa Bwana Yesu akabatizwa na Anania kisha mmisionari mkuu kwa vile mara nyingi alisafiri sana katika nchi za ng'ambo na kuunda makanisa mengi wakati wa safari tatu Korinto, Filipi, Tesalonike, Efaso, Galatia, Kolosai na kadhalika.

Kazi ya Mtakatifu Mtume Paulo ilikuwa ngumu kwa kuwa mara nyingi alipokuwa safarini alipata mateso mengi kwa ajili ya Bwana.

Mara kadhaa alitupiwa mawe akafungwa gerezani akavumilia baridi kali njaa, kiu na hata mara nyingi alikokotwa na mawimbi ya baharini.

Alipata faraja ya kiroho alipochukuliwa juu hadi uwingu wa tatu. Mwishowe alikamatwa na kufungwa gerezani kwa kuwa kwa amri ya Kaisari Nero aliuawa na kukatwa kichwa.

Hali ya utumishi katika kazi ya Mungu iliyofanywa na mitume hawa Petro na Paulo haina budi kuwa kioo na mfano bora wa maisha yetu. Tuishi kwa kadri ya mapenzi yake tukijua bila msaada wa Yesu, kwetu hakuna ahueni.

Kwa nini tunahitaji msingi wa maadili (4)

Tofauti za maoni juu ya mambo fulani fulani zisiwe sababu ya uhasama, bali ziwafanye watu kutafakari pamoja; ni katika kutafakari hivi pamoja ndio uchambuzi wa masuala kunaweza kufanyika pia mikakati na makubaliano bora kukabili masuala magumu .

Ndio kusema lazima kuwe na utaratibu wa uongozi mbalimbali kukutana mara kwa mara. Njia nyingine ni kwa kutoa maoni yao katika vyombo vya habari, jambo linaloanza kujitokeza nchini Tanzania sasa hivi.

Badala ya kukilaumu tu kitu kiitwacho 'Serikali' ni bora zaidi kupendekeza utatuzi bora zaidi wa masuala.

Kunaweza kuwa na Kongamano ili kuwapa fursa viongozi mbalimbali kutoa maoni yao juu ya mambo mengi muhimu sio tu juu ya siasa.

Mikutano ya aina hii inakosekana ingawa hapo na pale imefanyika inatakiwa iratibiwe barabara.

Mathalani kungeweza kuundwa Baraza la viongozi kwa minajili hivyo.

Hilo lingekuwa juu ya vyama vya siasa. Mabaraza ya viongozi yangeweza kuundwa katika ngazi ya wilaya, mkoa na taifa, au pia katika viwango vya wanataaluma, na wanataaluma mbalimbali kama madaktari, waandishi wa habari, wanasheria na kadhalika. Hao wangeunda vyama vyao huria (vyama huria vitazungumziwa zaidi katika kifungu kinachofuata)

Mabaraza ya aina hiyo na vyama hivyo vingepewa uhuru na madaraka kuhakikisha kuwa mapendekezo yao haya na malengo ya kisiasa.

Vyama Huria

Kuna vyama huria vingi katika Tanzania, kama Spoti,Utamaduni, biashara, haki za binadamu , kina mama n.k! Vingi zaidi vingeweza kuanzishwa katika mazingira yetu mapya kisiasa kwahitajika sana vyama kama vya biashara, vya ushirika na wakulima, vya wafanyakazi, vya wazazi n.k

Kati ya dalili nzuri ni kuanzishwa vyama katika mwelekeo tunaozungumzia hapa . itachukua muda kushamiri lakini matunda yake mema ni ya uhakika. Lazima tuhimize sana mwelekeo huo tena toka ngazi ya chini tunataka tuone kazi ya serikali ikiwa yakutegemeza juhudi za watu badala ya kutupangia vitu toka juu.

Kumbe vyama hivi havipingani na mwenye mamlaka , hivi ni vikundi vya watu wenye mielekeo sawia na wenye mambo yale yale yanayowakera.

Ni kwa kuvikubali vikundi kama hivyo na mambo inavyosimamia ndio siasa zinazoundwa nchini zitaihusisha jamii nzima. Hapa ndipo inapowezekana kupanga mambo kwa manufaa ya wote.

Mara nyingi watu hawaambiwi sheria gani zinatungwa au siasa gani zinabuniwa.

Hivyo ni kuwanyima haki yao. Lazima watu wahusishwe na maamuzi yanayogusa maisha yao, na watoe maoni yao.

Usipotafuta kujua maoni ya watu kabla ya kufanya maamuzi yanayowagusa utapata matatizo baadaye kama mgomo.

Suala la ardhi huko monduli ni mfano mmoja.

Kufanya mambo kirisiri katika mambo yahusuyo jumuia nzima ni dalili za udhaifu.

Tuchukue kwa mfano matatizo yaliyojitokeza mashuleni kama kungekuwepo na vyama vya waalimu na wazazi utatuzi wa mambo ungewezekana kabisa badala ya mikasa iliyotokea.

Hapo hoja za wahusika zingeangaliwa kwa makini zaidi.

Kutilia maanani mapendeleo na mapendekezo ya watu ni njia bora ya kuimarisha jamii na kielelezo cha utungaji sheria na kanuni.

Hivi tofuati zilizopo nchini lazima zisiwe tushio bali huchangia uboreshaji wa maisha ya jamii.

Wengi huchukulia tofauti kuwa tishio, kwa vyovyote ni lazima kuhakikisha kwamba hakuna kikundi kimoja kugandamiza vingine.

Kadiri mambo yalivyo sasa ni vikundi vya biashara ndiyo vyenye uwezo zaidi na kujitetea vyenyewe kuliko walimu au walaji.

Hui sio mwelekeo bora!

Tofauti za dini hazipewi makini unaotakiwa ili zisisababishe uhasama katika ya waumini hata kuhatarisha amani.

Tusijaribu kulikwepa suala hili.

kama wanataaluma Wakristo lazima tutoe mchango wetu wa mawazo au tuwaalike wanataaluma wa dini tofauti nao wafanye vilevile pamija tuweke msingi unaotakikana katika jamii yetu ya kitanzania.

Hapa chini tunazichambua tofauti zetu za kidini na jinsi tunavyoweza kuziishi bila matata.

3. Uwingi wa dini na athari zake kijamii na kisiasa

Tunaishi katika jamii yenye dini mbalimbali na tofauti, hivyo ni wazi athari zake zitaonekana katika nyanja za kisiasa.

Pengine masuala nyeti ya kidini hujitokeza na Mungu -bariki yakapita bila kuharibu amani.

Ila haitoshi kuridhika na kutoharibika amani lazima tuchambuue tofauti zetu kidini.

Makundi makumbwa ndio wakristu, Waislam wafuasi wa dini za jadi na yapo makundi madogo madogo kama wahindu.

Makundi hayo makubwa ya dini nayo yamegawanyika yenyewe, wapo Wakristu wa madhehebu mbalimbali yenye mitazamo tofauti kadhalika Waislamu nao wamegawanyika.

Hivi vitendo vya kundi fulani la wakristu au Waislamu haviwezi moja kwa moja kueleweka kuwa vitendo vya Wakristo au Waislamu wote.

Hivi tuanze kuelewana kwanza na wale walio karibu zaidi nasi.

Hata hivi tukubali kwamba sio kila mtu atajiunga na mazungumzo ya maelewano kati ya dini tofauti.

Tusiwakubali wale wenye lengo la kuendeleza maslahi yao huku wakiharibu maelewano wakijidai kuwakilisha dini fulani. Vikundi vya Kikristu au vya Kiislamu vinavyoelekea kuvigandamiza vingine haviwakilishi ukristu, uislamu au dini za jadi. Kupuuza tofauti zetu ni kujipambaza wenyewe. Tusidhani kwamba athari za dhambi hazigusi tabia na maoni ya dini yetu.

Mathalani tunaelewa nini na dhana kama haki, Uhuru demokrasia, dhamiri? Tuna maoni tofauti hapa na ni vema tusipuuze neno hilo.

Tena sio tofauti kati ya Wakristo na Waislamu hata kati ya Wakristo, mathalani wakatoliki na walokole wana maoni tofauti juu ya dhana hizo za msingi:

Hivi zipo tofauti kati ya Wakristo na wafuasi wa dini za Kijadi kama Wasuni na Washiha kati ya Waislamu.

Wapo wale wanaodadisi kwamba hapa Tanzania "Siasa haina dini" au "Katika ngazi ya mitaa na vijiji hakuna shida" kusema hivi ni kukosa kina katika kuyaelewa maisha ya jamii:

Jamii yahitaji kukubaliana katika yale tunayoyapa thamani ili kubuni siasa za kujenga. Tusipokuwa na msingi wa pamoja wa maadili tutawezaje kubuni siasa bora ya elimu, ya familia au kutoa miongozi ya maadili ya waandishi wa habari, wanataaluma au wanajeshi? Ikiwa dini zetu tofauti zina namna tofauti ya kuelewa dhana za msingi kama demokrasia na Uhuru wa dini tutawezaje kukubaliana, kuheshimiana kweli, pasipo kukaa pamoja na kujadiliana?

Uzoefu watufundisha wazi kwamba amani katika taifa letu itakuwa ndoto pasipokuwepo na amani kati ya dini mbalimbali.

Pasipo majadiliano hapawezi kuwa na amani kati ya dini zetu mbalimbali.

Majadiliano hayatawezekana tusipokubali kuwapokea na kuwaheshimu wenzetu wa dini tofauti wawe Wakristu, Waislamu au wafuasi wa dini za jadi. Tusipotambua kuwa Mungu yuko kati ya wengine na kwamba nao hushika dini yao kwa moyo hatuwezi kuheshimiana.

Bila kutakiana mema na kuvumiliana hakuna uwezekano wa kuwepo na mawasiliano ya kina. tunalazimika kuishi kwa kujihami.

Hapo jamii inakosa maelewano ya kweli na kuishi maadili ya nipe nikupe badala ya kuaminiana na kutenda pamoja kwa manufaa ya wote.

Hii ina maana kwamba lazima tujifunze kuwaeleza watu wengine tofauti zilizopo kati yetu nao katika lugha wanayoielewa. Lazima tuepuke lugha ya majigambo au mantiki ya 'jahad' kuwashinda wengine kwa mabavu, mapesa au kwa kutumia jeuri.

Wapo watakaodai kwamba Wakristu, Waislamu na Wafuasi wa dini ya jadi ni awali ya yote Watanzania ni kweli, tunao umoja hapa Tunaweza kujenga jamii juu yake.

Ila lazima tukiri pia kwamba tunazo tofauti kati yetu. Zinazotungwa Imani za dini hukua na kuharibu tabia na mitazamo yetu kijamii na kisiasa. Kupuuza tofauti hizi ni kufanya mambo juu juu.

Tuendeleze udadisi huu kwa kuangalia mifano miwili Uhuru wa dini na mtazamo wa imani za kidini mintarafu haki za binadamu. Athari zake kwa siasa ni wazi.

Uhuru wa Dini na Uhuru wa Dhamira

Ukristo na Uislamu kila imani moja hufundisha kwamba zinashika ukweli wote. Hivi wale wanaofuata imani tofauti ni kuishi katika makosa ya imani au kwa vyovyote kupungukiwa na ufunuo.

Kumekuwa na mang'amuzi mapya kati ya Wakatoliki katika kuelewa mafundisho ya Uhuru wa dini na Uhuru wa dhamiri.

Kabla ya mtaguso wa pili wa Vatikano (1962-1965)Kanisa Katoliki kimsingi lilifundisha kwamba ukweli tu ndio ulikuwa na haki ya kuzingatiwa. Kosa lingeweza kuvumilika tu katika mazingira fulani fulani kama pale tokeo jema zaidi lilipotarajiwa kama kutarajia lingetunza amani katika Taifa.

Baada ya mtaguso wa Vatikano II Kanisa Katoliki limekubali kwamba Uhuru wa Dhamiri na Uhuru wa dini ni haki ya mwanadamu. Watu wanao uhuru wa kufuata dini yoyote ikiwa wanatafuta ukweli kwa dhati na wapo wazi kupokea maongozi ya Mungu.

Waislamu hawakubali msimamo huo mpya wa kanisa katoliki.

Hao wapo tayari kuwapa Uhuru na haki watu wa "Dini za kitabu" (wayahudi, Wakristu Wazoroa striani) katika nchi za Kiislamu hao hulindwa. Lakini wanawezekana mipaka na pengine hata wanatanguliwa. Mathalani Muislamu anaweza kumwona Mkristu lakini sio Mkristo kumwoa Muislamu. Kumwingiza Muislamu dini nyingine ni marufuku.

ZIJUE IMANI ZA WENGINE

Ziwa Orra: Sehemu ya 'utakaso' kwa Waethiopia

Na Masha Otieno JR.

MWENDO wa masafa mafupi kutoka jiji la Addis Ababa, mji Mkuu wa Ethiopia unalifikia ziwa mashuhuri kabisa la Orra Arsedi.

Ukilitazama kama mandhari ya kawaida ni kweli laonekana kuwa ziwa zuri la kuvutia hasa kwa maumbile yake ya asili na maji yake matulivu. Kwako kama mtalii, ziwa hili lina maana ya maumbile ya asili tu aliyoyaumba Mwenyezi Mungu, na wala si zaidi ya hapo.

Lakini hivyo sivyo, Ziwa Orra - Arsedi, lilivyo kwa dini ya Oromo inayokusanya kabila la Wa - Oromo ambalo ni mojawapo kati ya makabila makubwa kabisa nchini Ethiopia.

Wa - Oromo ambao kwa asili ni wafugaji na wafanyabiashara wanaamini kuwa Ziwa Orra, ni la utakaso na pia ndilo chimbuko la jinsia mbili za binadamu zilizopo leo juu ya uso wa dunia wakimaanisha mume na mke.

Dini ya Oromo kulingana na kumbukumbu za wanahistoria imekuwepo yapata miaka 1000 kabla ya kuzaliwa Kristo.

Profesa Thomas Vilatman, ni Mtaalamu wa Elimu ya Sayansi ya Jamii katika Khuo Kikuu cha Addis Ababa, yeye anayo yafuatayo ya kusema kuihusu dini ya Waoromo.

"Waoromo wanaamini dini yao ni dini ya Mungu mmoja isipokuwa ina mambo yafananayo na Uislamu na Uyahudi"

Waoromo huja kwenye Ziwa Orra, ili kujitakasa katika kipindi cha mwisho wa mwaka na kile cha mwanzo wa mwaka. Waoromo hujitakasa kwa kuoga ziwani, kitendo wanachoamini kuwa kinasafisha dhambi zao na kuwawezesha kupata nguvu za uzazi.

Lakini si Waoromo peke yao waliotambika kwenye ziwa hili , Jarida la Africa Now , toleo la Agosti ,mwaka 1982, lilichapisha makala kuhusu viongozi wa mataifa ya Kiafrika na imani za uchawi ambapo ndani ya makala hiyo ilielezwa kuwa aliyekuwa Mfalme wa Ethiopia na mwanzilishi wa umoja wa Nchi Huru za Kiafrika, hayati Haille Sellasie, zama za utawala wake alipata kufukia kichwa cha binadamu kwenye ufukwe wa ziwa hilo la utakaso ili kujikinga kwa imani ya ushirikiana kulinda dola yake.

Haille Sellasie pamoja na jitihada hizo zote baadaye alipinduliwa na kuondolewa madarakani. Alitawala kwa mkono wa chuma akiacha uchumi wa Ethiopia ukiwa taabani; wananchi wakidhoofu kwa njaa na kukata tamaa ya maisha.

Miaka mingi baada ya kufa Haille Sellasie, Dini ya Waoromo ingali ikiendelea kwa kasi huku wakiendelea kujitakasa kama kawaida yao kwa kuoga maji ya ziwa Orra.

Waoromo wanaamini kuwa Mungu aliumba kwa siku 2. Baadaye aliibuka kiumbe mtakatifu aitwaye Ora kutoka ndani ya ziwa la Utakaso. Kiumbe huyo baada ya kuibuka ndani ya maji akagawanyika sehemu mbili sehemu moja ikawa mwanamke na sehemu nyingine ikawa mwanaume. Waoromo wanaamini kiumbe huyo aliyeasisi jinsia mbili za binadamu aliibuka kutoka ziwani siku ya 21.

Waoromo pia wanaamini juu ya unajimu na nyota. Siku zote huabudu chini ya mkuyu wakiamini ndiyo sehemu ya ibada. Dini yao imewapelekea kujenga imani kuwa Mungu husikia kilio zaidi akiitwa chini ya mti wa Mkuyu.

Pamoja na kuamini yote hayo ipo imani iliyojengeka miongoni mwa jamii zingine za Waethiopia kuwa Waoromo ni wapagani wanaoamini juu ya dini za jadi na siyo Mungu, kama wanavyodai.

Waoromo binafsi wanazikanusha tshutuma hizo na wanadai kuwa hawako kama watu wanavyofikiri wala hawaamini dini ya jadi, bali imani hiyo imekuja kwenye hisia za watu kwa sababu Waoromo wanathamini sana uhai na mali za a sili kama mimea na wanyama.

Hivyo wao wanajitetea kwa kudai wanaamini juu ya uwepo wa Mungu mmoja, muumba mbingu na nchi.