Watanzania tunatembea kinyumenyume na siasa potofu

Na. Arnold Victor

KATIKA simulizi za Kipare, kuna hadithi moja maarufu iitwayo, "Mrisha mwenye mongo: Nguto haiyo,". Kwa Kiswahili maneno hayo yana maana " Mchungaji mwongo: Chui anakuja."

Hadithi hii inatokana na kisa kifuatacho:

Kulikuwa na mchungaji mmoja aliyekuwa akichunga ng’ombe wake nyikani. Siku moja akapiga yowe kwamba amevamiwa na chui, wanakijiji wakajitokeza kwa wingi wakiwa na kila kilichoweza kuitwa silaha ili kumwokoa. Lakini baada ya kufika katika eneo la tukio ilibainika kuwa hakukuwa na hata chembe ya dalili ya kuwepo kwa kitu kama chui.

Wakiwa wamekasirika, Wananchi walimwonya aache tabia hiyo ya uwongo. Haikuchukua siku nyingi, mchungaji huyo akapiga yowe tena na wanakijiji walipojitokeza kumwokoa wakayakuta mambo ni kama yaliyopita- hakukuwa na chui! Wakaondoka. Siku iliyofuata mchungaji mwongo alipiga tena yowe, safari hii akiwa amevamiwa kweli na chui, lakini kwa vile wanakijiji walikwisha poteza imani naye, hakuna aliyejitokeza kumsaidia wakijua ni uwongo ule ule kama wa awali. Mchungaji huyo akashambuliwa na chui bila msaada hadi akafa.

Mwenendo wa viongozi wa siasa katika Tanzania hautofautiani sana na ule wa "Mrisha mwenye mongo."

Mapema wakati Waziri wa Mambo ya Ndani na Naibu Waziri Mkuu wakati huo Bw. Augustine Mrema aliposhushwa na kuwa Waziri wa Kazi na Maendeleo ya Vijana, baada ya kupata tetesi kwamba alikusudia kuihama CCM walimuuliza endapo ana mpango wowote wa kufanya hivyo. Majibu ya Bw. Mrema yakawa kwamba asingeweza kamwe kuhama CCM kwa vile ikiwa atashindwa kuwatumikia wananchi akiwa ndani ya chama hicho, asingeweza kamwe kuwatumikia vema zaidi akiwa nje ya CCM. Hakuishia hapo; alisema yeyote ambaye anahama CCM ni mwendawazimu! Siku chache baadaye Mrema akatangaza kujitoa CCM na kujiunga na chama cha upinzani cha NCCR-Mageuzi, ambacho nacho hivi sasa amekihama tena na kwenda TLP.

Mapema tena baada ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 1995, Makamu Mwenyekiti wa CUF Bw. Seif Sharif Hamad, aliutangazia umma, (si mara moja) kwamba aliyetangazwa mshindi wa urais wa Zanzibar Dk. Salmin Amour hatafika mwaka 2000 angali rais. Majuzi katika kipindi cha Kiti Moto cha Televisheni ya DTV, Seif alipoulizwa ni vipi Dk. Salmin kafika mwaka 2000 angali rais, akasema alimaanisha kuwa hangegombea tena mwaka 2000! Hiyo haingeleta "sense" kwa vile Katiba yenyewe ya Zanzibar inasema hangegombea, hivyo siamini kwamba Seif alichojibu alikimaanisha, ila swali lilimchanganya akajibu bila kufikiri, mradi tu ajiepushe na aibu ya kutabiri mambo ambayo hayakutimia.

Utamaduni huu wa kusema lolote kwa makusudi ya kufunika mambo kwa muda (temporary solution) bila kujali athari zake si wa wapinzani peke yao. Wengi tunamkumbuka aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Nje wakati wa Serikali ya Awamu ya Pili, Mheshimiwa Hassan Diria, jinsi alivyokanusha kwa nguvu tena kwa vitisho vikali kwa vyombo vya habari kuhusu mpango wa Tanzania kujiunga na Jumuia ya Nchi za Kiislamu (OIC), lakini haikupita muda maji yalipofika shingo ikabainika kuwa mpango huo ulikuwepo na kwamba Diria alikuwa anaujua vema na kuushiriki.

Kukiri kwa Rais Mkapa kwamba Ilani ya CCM iliyotumika kuwashawishi wananchi wakiweke chama hicho madarakani mwaka 1995, haitekelezeki wakati ndiyo iliyomsaidia kuingia ikulu nalo ni jambo jingine la kutisha.

Utamaduni huu wa kutosema kweli hauishii kwa wanasiasa peke yao. Umewaambukiza hata watendaji wa taasisi nyingi za Serikali na mbaye zaidi hata wataalamu. Mfano mmoja ni ule wa aliyekuwa Gavana wa Benki Kuu Dk. Idrissa Rashid, ambaye baada ya vyombo vya habari kufichua kwamba Benki ya kigeni ya Meridien Biao ilikuwa imekufa na ni ya kitapeli, alijitokeza hadharani kuikingia kifua na kuwaonya aliowaita wale wote wanaotangaza uwongo na fitna dihi ya benki hiyo. Lakini kwa kuwa ukweli hubaki kuwa ukweli hata ikiwa utabadilishwa majina kwa kiasi gani, baadaye Dk. Idrissa aliaibika baada ya hali kufikia mahali ambako asingeweza tena kufunika ukweli wa jambo hilo.

Na mwishoni mwa wiki iliyopita mwana wa Hayati Mwalimu Julius Nyerere Bw. Charles Makongoro, alitangaza kurejea CCM baada ya kudumu kwa zaidi ya miaka mitano katika vyama vya Upinzani na hata kukalia kiti cha Ubunge wa Jimbo la Arusha kwa tiketi ya Upinzani.

Makongoro alikabidhiwa upya kadi ya CCM na Rais Benjamin Mkapa, na akasema amerejea CCM ili kumuenzi marehemu baba yake ambaye ni muasisi wa chama hicho.

Lakini haiwezi kusahaulika kuwa ni Makongoro huyu huyu ambaye wakati wa kampeni za Uchaguzi Mkuu uliopita alimfananisha Rais Mkapa na kipande cha chupa kinachodhaniwa kuwa dhahabu! Makongozo wakati wa Uchaguzi huo wa ’95 alizunguka karibu nchi nzima "akiwaonya" Watanzania kuwa wajihadhari na baba yake (Mwalimu Nyerere) kwani ananadi jiwe ambalo anadai ni dhahabu lakini "ukweli" ni kwamba ni kipande cha chupa. Kwa maneno mengine aliwataka Watanzania wamwone baba yake (Baba wa Taifa) kuwa ni tapeli. Hicho "kipande cha chupa" (Rais Mkapa) sasa kimemuungamisha Makongoro na pia anasema anamuenzi yule "tapeli."

Kiujumla nchini Tanzania tumejijengea vichwani mwetu kwamba kuwa mwanasiasa mzuri maana yake ni kuwa mwongo mzuri. Tunaichukulia siasa kama sanaa ya uwongo, lakini wakati huo huo tukikubali ituongoze.

Kuonyesha tumefikia mahali pabaya hapa nchini, ukimsikia mtu anamwambia mwenzake "Acha siasa zako" maana yake "acha uwongo wako". Jamii yote inaamini kuwa siasa ni uwongo, na wanasiasa wetu wanaigonga mhuri dhana hiyo kwa matendo. Lakini je, ni kweli kwamba siasa yetu inapaswa kuwa uwongo? HAPANA, NAAMINI HAPANA!

Mwanasiasa kama dira ya jamii anapaswa kwa kweli kuwa mtu mwaminifu, msemakweli, mwadilifu na kila sifa inayomfaa mtu mwema, basi hiyo haipaswi kumpungukia mwanasiasa. Hatua tuliyofikia hivi sasa Watanzania ni sawa na ile ya "Mrisha mwenye mongo" kwa vile hatuna hakika tena juu kile tunachoambiwa leo, kwamba hakitabadilishwa kesho tena na mtu yule yule. Siasa kama mfumo wa maisha ni kusonga mbele na ukweli ndio utakaotufikisha huko. Kuendekeza siasa za uwongo ni kutembea kinyumenyume, macho mbele tutatumbukia shimoni na hilo ni hakika kabisa. Mungu ibariki Tanzania.

Shutuma hudumaza watoto

KWA kawaida binadamu yeyote hupenda kutiwa moyo na hujisikia vibaya anaposhutumiwa, japo anaweza kukosolewa kistaarabu asijisikie vibaya. Kwa watoto wadogo umakini zaidi unahitajika kuliko ilivyo kwa watu wazima kwa vile wanahitaji kutiwa moyo kwa kila wanalojifunza ili wajenge tabia ya kujiamini. Kuwashutumu kila mara kuna madhara makubwa kuliko faida. Endelea na Mfululizo wa makala zetu kutoka kitabu cha Shirika la Uchapishaji wa Lugha za Kigeni la Beijing, China juu ya Afya.

SHUTUMA zikitumiwa vibaya bila kujali wakati na hali ilivyo zitaleta matokeo mabaya. kwa hivyo inatubidi tuzuie mambo yafuatayo:

1. Tusiwalaumu Wakati wapocheza kwa Furaha

Kuna mtoto mmoja wa kiume ambaye hana tabia safi, anapenda kucheza na kokoto, mchanga na matope. Siku moja alitengeneza garimoshi kwa matofali, mama alipomwona mara akamshutumu bila kutaka kujua mchezo wake ulivyokuwa:"Nani karuhusu ucheze na vitu hivi vichafu? Rudi nyumbani kusoma!" Mtoto akarudi kwa shingo upande,mama alibaki pale akaangalia "garimoshi" la mtoto wake akaona baadhi ya "mabehewa" yamepakiwa mchanga mengine yamepakiwa kokoto, baadhi yamepakiwa "Saruji" (udongo wenye mchanga) na mengine ni matupu.

wakati huo mama akafahamu kwamba mtoto hakucheza ovyo bali mchezo wenyewe unamsaidia kupanua mawazo na ubunifu, mtoto hakika alicheza kwa furaha. mama aliona amekosa, akaamua kucheza mchezo huo pamoja na mtoto wake.

2. Tusiwe na Matakwa yanayozidi uwezo wa Watoto.

Uwezo wa kupokea mambo kwa watoto una kikomo chake. lakini baadhi ya wazazi wnawashindilia elimu kama kwamba chochote wanachofundishwa wanaweza kuelewa, kumbe kufanya hivyo kunapoteza hamu yao ya kujifunza. Mtoto mmoja siku zote huwa mchangamfu pamoja na wenzake katika shule ya kulelea watoto, lakini darasani daima hanyoshi mkono kuomba kujiba maswali. Sababu yenyewe ni kwamba wazazi wake wana haraka ya kumwelimisha ili awe mtu mashuhuri baada ya kukua. Kwa kulinganisha mtoto wao na watoto wengine wachache wenye akili za ajabu, walimfushindilia elimu kwamba kila asubuhi walimfundisha kusoma, kuhesabu, kuhifadhi mashairi.. Licha ya hayo, baada ya kurudi nyumbani kutoka shuleni inampasa mtoto kuandika kazi za nyumbani kwa saa mbili na zaidi na asipoweza kumaliza kazi zake za masomo naye hushutumiwa. Hayo yanazidi uwezo wake wa kupokea mambo, zaidi na zaidi mtoto akapoteza hamu ya kujifunza na kujaribu kujibu maswali kwa kuwa na mawazo ya kujidhalilisha ingawa anajua jawabu.

3. Tusiwashutumu Kupitia Kiasi

Shutuma zikizidi kiasi zaweza kukwamisha maendeleo ya akili za watoto. Baadhi ya wazazi wanapima watoto kwa kigezo cha "wasikivu" wanawazuia hivi na vile na kuwafanya wasiweze kufanya mambo kwa mawazo yao wenyewe wakawa wamekwamisha uwezo wao wa kufikiri na ubunifu wao. Matokeo yakawa kwamba watoto wamekuwa wasikivu, wanyamavu na mambo yote wanawategemea wazazi. wengi wa watoto hao hawawezi kujitegemea bila ya wazazi.

Wengi wa watoto hao hawawezi kujitegemea vizuri. Wengi wa watoto hao hawawezi kujitegemea vizuri ni wavivu wa kutumia akili na wategemevu ambao hupenda kuwaluliza wengine "nifanyeje" wanapopatwa na shida. Kinyume chake, wale watoto watundu waliopuuzwa bila ya kuzuiwa sana huwa na akili nyingi, juhudi za kutenda mambo na hawategemei sana wengine. Kwa hiyo shutuma lazima zidhibitiwe kwa kadiri ya kufaa, zitumiwe tu zinapofikia lengo la kuwaongoa zikizidi zitaleta matokeo mabaya.

4. Tusiwaonye sana

Baadhi ya wazazi kila wakati huwaonya watoto wasifanye hivi na vile kwamba mtoto akienda haraka kidogo huambiwa "nenda polepole" akipanda juu kidogo ataambiwa "shuka haraka" anapokatia barabara huambiwa "njoo nikubebe", hivi ni 'hatari' vile 'hapana'n.k Yote hayo pia ni maonyo yasiyofaa. Siku hadi siku watoto hupoteza nafasi nyingi za kujaribu mambo, na uwezo wao utakuwa mdogo kwa kulingalisha na watoto wengine wa rika moja katika mchezo wa kuruma viunzi, baadhi ya watoto hawaoni shida, lakini wengine hulia machozi mbele ya viunzi.

Hali hii inatuambia kwamba tuwaache watoto wajifanyie mambo kwa uwezo wao, wapate maarifa ya kutatua shida na wawe washupavu wanapokutana na shida inafaa washajiishwe ili wamudu kuzitatua.

Shutuma zisizofaa ni mbaya zaidi kuliko makosa waliyoyafanya watoto .

Shutuma hizo zikizidi huwaletea watoto hasara kubwa mno.

Fransika Kabrini: Mmarekani wa kwanza kuwa Mtakatifu

Na Josephs Sabinus

Juu yake, inawezekana kutumia maneno ya Mtume Paulo kwa Timoteo, kwamba, "navumili" kila litu kwa ajili ya wateule wa mungu ili wao pia wapate ukombozi upatikanao kwa njia ya Yesu kristo na ambao huleta utukufu wa milele" {2Tim. 2:10}

Fransiska aliyekuwa kitindamimba kati ya watototo kumi na watatu wa mama yeke, alizaliwa nchini Itali, mwaka 1850.

Tunaambiwa kwamba, muda mfupi tu baada ya kuzaliwa kwake, kundi kubwa la njiwa waliokuwa wametanda angani, lilitua uani kwao amapo baba yake alikuwa ameanika nafaka. Ingwa mzee huyo alijitahidi kuwafukuza, njiwa hao walikimbia na kurudi tena mara kwa mara.

Hali hiyo ikatafsiriwa kama dalili njema kwa kichanga hicho.

Baba yake aliyemtaka awe mwalimu na hvyo kuamua kumpeleka masomoni katika shule ya bweni iliyoendeshwa na masista, kifo chake {mzee huyo} kilia mbatana haraka na cha mke wake ambao wote walifariki muda mfupi sana baada ya Fransiska kumaliza masomo yake.

Kwa kuwa alikuwa na hamu yakuwa mtawa na mmisionaari, aliomba kujiunga na masista waliokuwa wakimfindisha shuleni.

Maskini wa mungu! Wakamkatalia eti kwa kuwa afya yake ilikuwa dhaifu.

Akajaribu kutaka ajiunge na watawa wengine. Maskini wa mungu; hakujua kuwa yaliyo kwenye kundi la mbuzi, ndiyo hayo yawezayo kupatikana kwenye kundi la kondoo. Nasema hivyo maana huko nako alikataliwa tena kwa mara ya pili.

Mtakaltifu huyo anayekumbukwana watakatifu wengine wa Afrika kama karemoni, aliyekuwa askofu na Iskirion, aliyekuwa mfiadini wa Misri, kila ifikapo Desemb 22 ya kila mwaka alianza kushirikiana na paroko wake kufundisha dini kuwatembelea wagonjwa, kuwasaidia maskini, na hata hivyo ilimchukua muda mfupi tu, akaanza kuwafundisha shuleni.

Fransika Kabrini, aliyekuwa raia wa kwanza wa marekani kupewa heshima kuu ya kuitwa mtakatifu mwaka 1946, baada ya kifo chake kilichotokea ghafla desemba 22,1917, akiwa na umri wa miaka sitini na saba, alikubali kusaidia katika majukumu kadhaa katika nyumba ya mayatima ingawa kamwe hakuvutwa na kazi hiyo.

Akaifanya kwa majuma mawili hali amebakia hapo akisaidiana na wengine kwa miaka sita.

Ingawa Fransiska alitazamiwa kuibadili nyumba hiyo ya mayatia pamoja na walezi wake ili iwe mwanzo na shirika la kitawa, mlezi wake mkuu alimchukia na kumpinga kila mpango wake.

Hata hivyo, ushirikianao na walezi wake wengine saba walitaka kumtumikia Mungu katika nchi za misioni ulizidi kuimarika.

Mwaka 1877, watawa wote hao waliweka nadhiri zao za kwanza za kitawa hata hivyo Askofu alimtaka Fransiska ajaribu kuunda Shirika la Wamisionari mahali pengine baada ya kuamua kufungwa nyumba ile ya mayatima.

Akiwa na wenzake wakakodisha nyumba iwe Konventi ya kwanza ya Shirika jipya lililoitwa Shirika la Wamisionari wa Moyo Mtakatifu kwa ajili ya kuwalea wasichana Wakristo.

Ingawa Shirika hili lilikuwa upesi na Fransiska Kabrini akachaguliwa kuwa Mama Mkuu wa kwanza alikubwa na vizuizi na majaribu mengi toka pande zote muhimu zinazomzunguka kimazingira.

Mwaka 1887, alipooenda Roma kutafuta ruhusa rasmi ya kuwepo shirika lake. Huko alikutana na watu kadhaa na wengi walimshauri kinyume na matakwa yake hata hivyo hakuna aliyesikilizwa.

Mjini Roma alifungua nyumba mbili moja kwa ajili ya watoto na ya pili kwa ajili ya shule kwa wasichana. Mwaka uliofuata Shirika lake lilikubaliwa na wakuu wa kanisa.

Sista Fransiska alishauriwa na Papa mwenyewe kuwatuma masista waende Marekani kufanya kazi ya kitume kati ya wahamiaji wa Kiitalia akaenda mwenyewe.

Machi 31,1889 alienda New York uliokuwa mji mkubwa sana. Katika mji huo peke yake kulikuwa na wahamiaji wa Kiitalia 50,000.

Shida kubwa iliyomkabili ilikuwa juu ya yule mwanamke aliyevunja ahadi yake ya kumtayarishia Sista Fransika na wenzake nyumba.

Kwa kuwa watoto walizidi kungoja kwa wingi na hali nyumba na shule zikikosekana walijitahidi na kupata nyumba iliyokuwa katika hali mbaya sana nyumba hiyo ilijaa chawa na viroboto.

Askofu akamshauri arudi Italia, lakini Fransika alikataa kata kata akamfuata yule mfadhili mwanamke na wakasikilizana kabisa hata kufungua nyumba moja ya masista wakajishughulisha na kila namna kuifanya kazi ya Mungu kwa heshima, upendo na unyenyekevu.

Mtakatifu Fransiko Kabrini alifungua nyumba 67 huko Ulaya na Amerika. alipofariki aliacha shirika lake likiwa na masista 500 watoto 5000 hivi, waliweza kufunzwa katika shule na nyumba za mayatima na hata wagonjwa waliotunzwa katika hospitali zake walikuwa karibia zaidi ya laki moja.

Ingawa hakuruhusu kuchoka wala kukata tamaa Fransika alikabiliana na shida mbalimbali vishawishi na maumivu daima vilikuwa njiani na ilivyoonekana hakuviogopa wala kuvikwepa bali tu alitaka ashindane nanyo na hatimaye avishinde.

Kushungulikia kwake hakukuwa namna ya kukabili mtazamo fulani aliokuwa nao kitabia bali shughuli zake nyingi zilikuwa tunda la upendo mkubwa kwa heshima ya Mungu.

Upendo wake kwa Bwana ulibubujika matendo nayo aliyafanya katika muungano thabiti wa kiroho alikuwa kielelezo cha Watawa wote wenye uelekeo wa utendaji.

ZIJUE IMANI ZA WENGINE

Dini iliyopigania uhuru

Na Masha Otieno JR.

JINA la Simon Kimbangu bado halijasahaulika katika rekodi za kumbukumbu za kihistoria ya Afrika ya kati.Mwanadini huyu mashuhuri ametajwa kwenye vitabu vingi vya historia kuanzia vile vilivyoandikwa kwa minajili ya watu kujisomea kuongeza maarifa ya kawaida mpaka vile vile vinayotumwa na wanafunzi katika shule na vyuo.

Mwaka 1956 Simon Kimbangu aliiibuka nchini Zambia wakati huo ikiitwa Northern Rhodesia ambapo alianzisha dhehebu la aina yake lililowatia kiwewe wazungu hasa wakulima walowezi waliokuwa wakishikilia sehemu kubwa ya ardhi.

Dhehebu hili la Simon Kimbangu iliitwa 'dini asilia ya mtu mweusi' lengo lake la kuianzisha ilikuwa ni kuhakikisha kuwa 'Masettler' wote wa kizungu waliokuwawakishikilia ardhi ya Wazalendo nchini Zambia kwa wakati huo wanafukuzwa na kuondolewa kwenye ardhi ya waafrika.

Simon Kimbangu aliweka kituo chake cha kwanza huko 'Kitwe' Zambia huko alisajili idadi kubwa ya vijana wenye nguvu ambao walijiunga na dini yake tayari kwa kupambana na mtu mweupe.

Pamoja na makanisa ya dhehebu lake yaliyo mengi kujengwa kwa ushirikiano na wazalendo ambao ni waumini wake, pia aliwapa vijana wake mafunzo ya kivita kuwawezesha kujihami dhidi ya Waingereza.

Walowezi wa Kiingereza walianza kuhofu kwenye mashamba yao . Ulipofika mwaka wa 1957 Simon Kimbangu alikuwa amezidisha mapambano ambapo alikuwa ameanza kushambulia wazungu toka Shamba moja hadi jingine.

Imani ya dini yake iliyowatia nguvu vijana wake ilikuwa ni kwamba ardhi ya Afrika ilikumbwa Mahususi na Mungu kwa ajili ya Mwafrika siyo kwa ajili ya mtu mweupe.

Kwa vile wakati huo vuguvugu la Uhuru lilikuwa limeishaanza huko 'Norther

 

n Rhodesia' Waafrika wengi waliokuwa na ari ya kujikomboa kutoka makucha ya wakoloni walijiunga ka wingi na dhehebu la Simon Kimbangu.

Wazalendo wengi nchini Zambia waliamuona Kimbangu kama ni mkombozi wao. Hata hivyo wazungu wao walijizatiti vilivyo kuhakikisha kuwa mwafrika huyo aliyeanzisha dhehebu la Kipagani Uhuru anauawa mapema iwezekanavyo.

Kabla ya kujitosa kwenye mapambano ya kupigania uhuru kwa kuanzisha dini ya Ualimu nchini Uingereza. Alirejea Zambia ambako alikuwa ni mwalimu kwenye shule za misheni.. lakini baada ya kufundisha kwa miaka kadhaa alipata wazo la kujianzishia dhehebu lake lililokuja kuleta mtafaruku baadaye baina yake na Waingereza.

Ilibidi Waingereza waanze Msako maalum dhidi ya Simon Kimbangu baada ya kuona kuwa walowezi wengi kwenye mashamba yao wanauawa walianzisha msako maalum dhidi ya Simon Kimbangu.

Mwanzilishi huyu wa Dhehebu linalopinga wazungu aliona maji yamekuwa marefu na ilibidi akimbie kuja pande za kaskazini kwenye mpaka wa Tanzania na Zambia.

Hata hivyo Kimbangu hakuweza kuishi muda mrefu mwezi Agosti mwaka 1957, wazungu wa Kiingereza walimkamata kwenye kituo chake alichokiweka mpakani kabala hakaingia Tanzania.

Hakuonekana tena toka hapo na historia yaeleza alihukumiwa kifo, hata hivyo alisaidia kuchochea vuguvugu la Uhuru nchini Zambia