Papa awataka madaktari kutetea uhai

VATICAN CITY

BABA Mtakatifu Yohane wa Pili amewataka madaktari Wakatoliki kutetea maisha kwa kuzuia kuenea kwa vitendo vya utoaji na uzuiaji wa mimba kwa njia za kisayansi.

Akiongea mbele ya umati wa watu wapatao elfu sita, tarehe 7 Julai

Katika Kongamano la Kimataifa juu ya taaluma ya madawa na haki za binadamu, mbele ya halaiki ya watu wapatao elfu sita, hivi karibuni, Papa alisema, madaktari hawana budi kueneza mapendo kwa wagonjwa kwa moyo ili wote unaohitajika katika uponyaji.

Alisema, ili kufanikisha hilo, upendo unahitajika zaidi kwa wagonjwa wanaohitaji uponyaji na hata viumbe wengine ambao hawajazaliwa.

"Si tu kwamba wagonjwa lazima wasaidiwe kupata uzima wa kimwili, bali pia, kisaikolojia na kiroho," alisema.

Mkutano huo wa wiki moja ulizungumzia zaidi taaluma ya udaktari na haki za binadamu kama vile utoaji, na uzuiaji wa mimba, mateso na hali mbaya ya kimaisha katika nchi zinazoendelea ambako huduma za afya ni duni au hazipo kabisa.

Alisema kazi za madaktari wakatoliki, ni kutetea, kuimarisha na kupenda maisha ya kila binadamu kutokea mwanzo hadi kifo chake.

Alisema sheria zinazotolewa kwa utoaji mimba au uzuiaji mimba zinapotosha na haziwezi kuwapa moyo madaktari ambao wanatakiwa kuhifadhi haki na malengo yanayotakiwa.

Baba Mtakatifu amewataka Wakatoliki wote wanaofanya kazi katika fani ya udaktari wawe na msimamo imara kupinga mateso yanayosababishwa na vita, matatizo ya wakimbizi na magonjwa ya kuambukiza na hasa pale watu wanapinga haki za msingi wa afya.

Mkutano huo uliwakilishwa na nchi 43 zikiwakilisha ujumbe kwa Baba Mtakatifu kuhusu haki za binadamu.

Waandaaji walisema madhumuni ya warsha ni kutoa njia mpya ya kutoa huduma za kitabibu na jinsi ya kuwaendea wagonjwa na kuwahudumia.

Warsha hiyo iligharamiwa na vyama kitaaluma kwa kushirikiana na vya Ulaya ikiwa ni pamoja na Italia.

Wabunge wawili kortini kwa kuchapana makonde

BLANTYRE, Malawi

Watu 11 wakiwamo wabunge wawili na watu wengine 9 wanaowaunga mkono, wamekamatwa na kufikishwa katika Mahakama ya Malawi, kufuatia kitendo chao cha kupigana hadharani kutokana na tofauti za kisiasa.

Wabunge hao waliokamatwa baada ya kutwangana makonde hivi karibuni katika wilaya ya Kati ya Nkotakota, ni Bw. Demestrel Chikwawo na BW. William Bondwe, wanaokiunga mkono Chama cha Malawi Congress.

Habari zilizopatikana zilisema ugomvi huo ulifuatia hatua ya Bw.Chikwawo, ambaye mwenyewe pia aliliripoti kuwa alikwenda Nkotakota kuitisha uchaguzi wa viongozi wa chama chao kwenye kwenye eneo hilo lakini, Bw. Bondwe, hakufurahishwa na hatua hiyo na hivyo, alimzuia mwenzake kufanya hivyo.Wote wamekana mashitaka yaliyofunguliwa dhidi yao katika mahakama hiyo ya nchini Malawi kuwa walipigana hadharani na wameachiwa kwa dhamana.

Kesi yao inatarajiwa kusikilizwa wiki ijayo.

Obotte kuendelea kukaa Zambia licha ya pingamizi

LUSAKA, Zambia

Rais wa zamani wa Uganda, Milton Obotte, huenda akaendelea kuishi nchini Zambia licha ya pingamizi zinazoendelea kutolewa na nchi kadhaa za Afrika.

Rais Fredrick Chiluba wa zambia, ameliambia Bunge la Jumuiya ya Madola kuwa ingawa baadhi ya watu katika bara hili wamekuwa wakihoji juu ya kuwapo kwa Obotte nchini mwake, Obotte anaweza kuendelea kuishi nchini humo.

Tangu mwaka 1986, alipokimbia mapinduzi ya kijeshi yaliyofanyika nchini kwake, Obotte amekuwa akiishi uhamishoni.

Hata hivyo, mbali na kuwapo Zambia kama mkimbizi, Obotte aliwahi kuishi Tanzania na kurudi nchini mwake Uganda wakati majeshi ya Tanzania yalipofaulu kumuondoa madarakani dikteta Idd Amin, aliyeongoza nchi hiyo kimabavu.

Rais wa sasa wa Uganda, Yowel Musseven, ambaye jeshi lake limepigana vita ya msituni kwa kipindi cha miaka kumuondoa madarakani Obotte, hivi karibuni alitangaza kumruhusu Obotte kurejea nchini mwake baada ya kutangaza kuwa anaachana na masuala ya siasa